Seif ataja sababu za CUF kudhulumiwa Z’bar

Na Mwajuma Juma, Zanzibar

MGOMBEA urais wa Zanzibar kwa tiketi ya Chama cha Wananchi (CUF) Maalim Seif Sharif Hamad, amesema chanzo kikuu cha kudhulumiwa chama hicho kila baada ya uchaguzi visiwani humo, ni kukosekana umakini wa kulinda kura.

Kutokana na kubaini tatizo hilo, mwaka huu amewataka mawakala wa chama hicho kutoondoka vituoni wakati wa kuhesabu kura ili wawe tayari hata kujisaidia kwenye chupa ili kuziba mianya yote ya wapinzani wao kuiba kura.

Maalim Seif alitoa kauli hiyo wakati akihutubia wanachama wa Jumuiya ya Wanawake wa CUF katika ufunguzi wa Tamasha la Wanawake lilofanyika Jamatkhan mjini hapa.

Alisema wakati shughuli ya kuhesabu kura ikifanyika, mawakala wa chama hicho wachukue chupa za maji ambazo watatumia kujisaidia ili kuhakikisha kura zao haziibwi.

Alisema kwamba kumekuwepo udhaifu mkubwa kwa wasimamizi wa chama hicho kutokana na kujaribu kutoka kila mara hali inayosababisha kutoa mwanya wa kura kuibwa.

“Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu
na kuombeni mchukue chupa, ili mjisaidie hapo hapo ili kulinda kura zenu”, alishauri Maalim Seif.

Hata hivyo aliwataka wanawake hao kuwa makini katika kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu, kwa kuteua mawakala waaminifu katika mchakato huo.

“Nimesikia toba shikio eti wenzetu wanataka kuwanunua mawakala wetu ili kupata urahisi wa kutuibia kura, lakini akinamama muwe macho na mkimuona wakala ambaye mna wasiwasi naye mtupe taarifa,” alisema Maalimu Seif.

Aliwataka wanawake hao kujiandaa kikamilifu kwa kupanga mikakati itakayofanikisha shughuli nzima ya upigaji kampeni ili ziwafikie walengwa.

Aliwataka kujiamini na kufanya kazi kwa ajili ya kukipa ushindi chama hicho kwa kufanya kampeni za nyumba kwa nyumba na kuwashawishi wananchi kukipigia kura ndiyo chama hicho

“Wanachama wetu mnatabia ya kujiamini sana kwamba chama chetu kishashinda, lakini msichukulie hali hiyo bali fanyeni kazi ili kuweza kukipatia ushindi”, alisema.

Naye Makamu Mwenyekiti wa CUF Bw. Machano Khamis Ali aliwataka wanawake hao kutokubali kurubuniwa kwa maneno ya watu ambao wamekuwa wakisema kwamba mwanamke hana haki ya kushiriki katika uchaguzi, kwa madai kuwa ni haramu.

Alisema kwamba mwanamke anahaki sawa na mwanaume kushiriki katika hali zote, kwa lengo la kujikomboa na kuwataka wajipange kuhakikisha wanakipigia kampeni chama chao na kukiingiza ikulu.

“Mkae chini mjipange kisha mhakikishe mnakiingiza ikulu chama chenu, na kwa hili wanawake mnaweza, lakini cha kusisitiza ni kuwaendea hasa wanawake wa vijijini kuwaelimisha juu ya umuhimu wa kushiriki katika uchaguzi na upigaji kura”, alisema.

Tayari chama hicho kimeshazindua Ilani yake ambapo Septemba 16, kinatarajiwa kuzindua kampeni kwa upande wa Unguja na Pemba itakuwa Septemba 18 mwaka huu.

Chanzo: Majira, 14 Septemba 2010

Leave a comment