Furushi la maafikiano likwekwe wazi

18 11 2009

Na Ally Saleh

Leo Jumatano itakuwa ni wiki mbili tokea Rais Amani Karume na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi CUF ambao wamekuwa mahasimu wakuu wa kisiasa walipokutana katika tukio ambalo kwa wengi wetu halikuwa likitarajiwa kabisa. Na ukweli ni kuwa hadi sasa jambo hilo bado halijatulia katika akili za wengi.

Sababu ya kutotarajiwa kukutana kwao huko ni kwa vile juhudi za kuwakutanisha huko nyuma zilishindwa na hata sababu ya kuwakutanisha ambayo ilikuwa ni kuzungumzia maafikiano ya kisiasa ilikuwa imeshapigwa kumbo na Mkutano Mkuu Maalum wa Chama cha Mapinduzi CCM.

CCM ilisema wazi wazi kuwa maamuzi yoyote yale ya hatma ya kisiasa ya Zanzibar lazima yapelekwe kwa wananchi kwa njia ya kura ya maoni na wazo la kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa kama vile ya mpito kuelekea Uchaguzi wa 2010 si jambo linalokubalika.

Na kwa hivyo juhudi za miezi 14 za mazungumzo ya vyama hivyo viwili zikawa zimezikwa katika kaburi, lakini kumbe inavyoelekea hazikubali jambo hilo, na ndipo likatokea hili lilotokea la Wazanzibari wenyewe kwa wenyewe kuona kuwa ni lao na ni wao ndio walipe nguvu na kulifufua.

Kila Mtanzania na kila Mzanzibari na hata marafiki na washirika wa nchi hizo walikuwa wakiamini kuwa hakuna litalofanyika kwa kipindi hiki cha chini ya mwaka mmoja zaidi ya kusubiri Uchaguzi Mkuu wa 2010 ambao pia kila mtu ana kila imani kuwa utakuwa wa kupimana nguvu mno kwa vyama vikuu kinzani CUF na CCM.

Dalili za kuwa tumekuwa tukielekea katika Uchaguzi wa Damu ( Bloody Elections) zilikuwa zimeshakuwapo. Kukataliwa kuandikishwa watu, kukataliwa watu kupewa Vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi, madai ya kuandikishwa vikosi katika sehemu ambazo wana vikosi wanapelekwa kwa madhumuni hayo na si kwa uhamisho wa kawaida wa kikazi, kuwepo kwa madai ya watu kuandikishwa zaidi ya jimbo moja, kuandikishwa watu wa chini ya umri wa kisheria kuchomewa nyumba watu, kuharibiana mali na kadhalika na kadhalika.

Kwa hivyo kuja ghafla kwa kile ambacho sasa Maalim Seif amekuwa akikipa jina la “maridhiano ya Wazanzibari” kumekuwa na upepo na mwanga mwiki kiasi ambacho kinaweza kutilika shaka. Waingereza wanasema usemao “ It is too good to be true” kwa maana yake ni kuwa uzuri wake ni mno kiasi cha kutilia shaka.

Inawezekana sisi tutapigwa muhuri au kunyooshewa kidole kuwa ni watu wenye shaka au tena tuazime msemo wa Kiingereza kuwa ni “Doubing Thomases” lakini tunahisi ni vyema kuwa na shaka sasa hivi kabla ya kuja kujiuliza masuala yasiojibika hapo baadae.

Ninachokiogopa mimi ni kile ninachokiona na kukisikia hivi sasa na ambacho kinanikerereketa akili yangu ni kule kuongezeka kwa matumaini ya watu kwa kuamini kauli za viongozi wao wa kisiasa, ambazo si ngeni na wala si za mara ya kwanza.

Kumekuwa na msemo wa kuwa “ Sasa ni wakati wa kujenga Zanzibar Mpya” na nyuma ya msemo huo watu wamekuwa wakisema mambo kadhaa kama vile kuamini kuwa kila kitu kimekubaliwa na mambo yataenda vizuri na kwa maridhiano ya Wazanzibar ( Zanzibari consensus).

Kumekuwa na tafsiri nyingi ya hiyo dhana ya Zanzibar Mpya. Nyingi ya hizo ni zile ambazo zinaamini kuondolewa kwa vikwazo ambavyo vimekuwa vikikwaza mfumo wa demokrasia na upigaji kura hapa Zanzibar na ambapo vikwazo hivyo pia vimepelekea kumwagika kwa damu.

Pia wengi wameanza kujenga matumaini kuwa ujenzi wa Zanzibar Mpya utakuwa na maana iwapo matokeo ya kura yataheshimiwa na kwamba uenedeshaji wa Serikali utajali ushirikishwaji wa umma na kila mmoja atapata fursa kwa mujibu wa uwezo wake na si kwa kujali mtizamo wake wa kisiasa.

Tumeambiwa kuwa mazungumzo ya Karume na Seif yalilenga kuhakikisha suala la amani na usalama katika nchi ambalo kwa tafsiri ni pana na kwa kweli linaweza kumeza mambo yote ambayo tumeyataja hapo juu yanayotiwa katika vunge la mtizamo wa kujenga Zanzibar Mpya.

Viongozi wakuu hao wa kisiasa wanataraji tuunge mkono na kubariki kile walichokizungumza bila ya kujua undani wake, misingi yake na hata mipaka yake. Tunatakiwa tushuhudie kitu ambacho hatuwezi kukisoma popote pale. Hivi sasa imekuwa ukihoji juu ya hilo unapigwa muhuri wa “Doubting Thomas.”

Ni wiki mbili sasa tokea tukio hilo kutokea kama nilivyotangulia kusema na hatuna mwanga wowote wala popote pale pa kushika juu ya kile kilichojiri chini ya paa la Ikulu lakini wakati huo huo tukitakiwa kuwa Wazanzibari wazuri tunaoitakia mema Zanzibar na kwa hivyo kuamini kuwa walikubaliana yalio na kheri na sisi.

Ni wiki mbili ambapo hatujaona hatua yoyote ile ya kuelekea katika kutatua kero za kisiasa na kidemokrasia ambazo kwa sasa ndio kabili na ambazo kama hazijakabiliwa sasa basi utatuzi wake unazidi kuwa mgumu kila siku moja inayokwenda. Kero hizo mbili ni uandikishaji wapiga kura na vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi.

Sisi “Doubting Thomas” tupo kwa sababu tunajua wakati huu upande wenye uwezo wa kupenyeza wapiga kura, unafanya kila bidii kuifanya kazi hiyo ili ikija ikitoka kauli ya kusimamishwa au kurekebishwa iwe wamefika mbali. Hatari iliopo ni kuwa huko mbali watakako kuwa wamefika, inaweza ikatokea upande ambao ulisusia kuandikisha ukashindwa kuridhi.

Tungetaraji kwa nia njema ya maridhiano hayo, ndani ya muda huu wa wiki mbili kungekuwa na matamshi mazito kutokea upande wa Serikali kuhusiana na mambo hayo mawili, ingawa Rais Karume aliwaambia waandishi wa habari kuwa Uchaguzi Mkuu wa 2010 iwapo utawaacha watu wenye sifa, utakuwa si uchaguzi kitu, lakini hiyo si kauli ngeni, hata ndani ya mwaka huu.

Kwa hakika, ingawa baadhi ya watu watasema hilo si la muhimu, lakini inaonekana kuwa ni upande wa CUF peke yake ndio uliokwenda kwa umma kuelezea kilichotokea na kuwataka wanachama wake waunge mkono maridhiano hayo, lakini bado hatujaona upande wa CCM kufanya hivyo.

Najua hoja itakuja kuwa CCM haina haja ya kufanya hivyo kwa sababu wao ndio wenye Serikali na wao ndio waliotambuliwa na walikuwa wakiitaka CUF ifanye hivyo kwa muda mrefu, lakini tatizo langu ni ile picha ninayoiona sasa hivi ya baadhi ya watu ndani ya CCM kuona kuwa hayo hayawahusu wanachama, bali ni ya Serikali.

Hatari ninayoiona mimi hapa ni kuwa iwapo umma wa wanachama wa CCM haujatayarishwa, na tunavyowajua wanachama hao kwa misimamo yao ya asili, kuna uwezekano mkubwa wa kutofika mbali pamoja na kuwa na nia nzuri.

Maana ukweli ni kuwa hivi sasa kumekuwa na kauli kadhaa wa kadhaa za pembeni, ambazo mimi sitaki kuwa zionekane ni za mlango na hazimughasi aliyelala, ila zichukuliwe kwa umuhimu wake kwa CCM Zanzibar kuzitolea kauli za wazi wazi. Bahati mbaya kauli nyengine ni za watu wenye madaraka.

Kwa fikra zangu, kuendelea kuwataka watu washikilie kamba ya matumaini bila ya kuwaonyesha wanachotarajiwa kukitumaini, ni kujenga matumaini ambayo yana shaka katika kile kinachotumainiwa. Isichukue muda tena, kama hatuambiwi kilichomo kwenye furushi la maridhiano, basi angalau tuone vitendo vyenye ishara za wazi, na ikibidi kuwepo na maandishi juu ya kilichoridhiwa.

Tunataka kauli thabiti au maandishi ili tujue tunapimaje utekelezaji wa udhati wa maridhiano haya. La sivyo, tutajuaje kuwa tunasonga mbele na sio dangaya toto na kupoteza muda?

Chanzo: Mwananchi, 18 Nov 2009





Zanzibar Daima, yasema risala ya wanawake wa CUF

15 11 2009

RISALA YA JUMUIYA YA WANAWAKE WA THE CIVIC UNITED FRONT (CUF – CHAMA CHA WANANCHI) KWA MAKAMO MWENYEKITI WA CHAMA, MHE. MACHANO KHAMIS ALI, KWENYE MAANDAMANO YA KUUNGA MKONO HATUA ZA KATIBU MKUU WA CUF NA RAIS WA ZANZIBAR KUWALETA WAZANZIBARI PAMOJA

15 Novemba 2009,
Viwanja vya Demokrasia,
Zanzibar

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, Makamo Mwenyekiti wa The Civic United Front (CUF – Chama cha Wananchi), Mhe. Machano Khamis Ali,

Mheshimiwa Katibu Mkuu wa The Civic United Front (CUF – Chama cha Wananchi), Maalim Seif Sharif Hamad,

Waheshimiwa wajumbe wa Baraza Kuu la Taifa la CUF, Wakurugenzi na Manaibu Wakurugenzi, wanachama na wanawake wenzangu na, juu ya yote, waheshimiwa Wazanzibari, Asalaam Alaykum!

Awali ya yote naomba niitambulishe salamu mpya ambayo sisi wa Jumuiya ya Wanawake wa CUF tumeamua iwe inatumika kusalimiana baina yetu kila tunapokutana, hasa katika muktadha wa shughuli kama hizi na wakati tulionao. Kuanzia sasa, tungelipenda Wazanzibari wenzetu wote, baada ya kuamkiana maakizi yetu ya kawaida ya Asalaam Alaykum – Alaykum Salaam, basi waongeze na Zanzibar na mwengine aitikie Daima! Kwa hivyo, iwe Zanzibar Daima!

Kwa heshima, naomba tusalimiane hivi sasa:

Zanzibaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaar! Daimaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaa!

Zanzibaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaar! Daimaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaa!

Zanzibaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaar! Daimaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaa!

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, waheshimiwa Wazanzibari wenzangu, waheshimiwa waalikwa,

Jumuiya ya Wanawake wa CUF inaichukulia hii kuwa ni siku ya aina yake kwa Zanzibar. Ni siku ambayo wanawake wa Zanzibar wameamua kufanya maandamano ya kuwaunga mkono viongozi wakuu wa Chama chetu kwa maamuzi makubwa na mazito waliyoyachukua, ambayo maslahi yake kwa nchi yetu hayana mithali.

Ni jambo la fakhari kwamba, sisi wanawake ndio ambao tumekuwa jumuiya ya mwanzo kuuona umuhimu wa maamuzi hayo yaliyofanywa na uongozi wetu na, hivyo, tukaamua kuingia barabarani kuthibitisha uungaji mkono na utayarifu wetu wa kufanya kila lililo ndani ya uwezo wetu, kusudi dhamira ya pamoja tunayoisimamia iweze kutimia.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, waheshimiwa Wazanzibari wenzangu, waheshimiwa waalikwa,

Kuna ambao wanajiuliza kwa nini wanawake hawa hawa ambao wiki iliyopita kwenye viwanja hivi hivi walilia kwa uchungu na hasira pale Katibu Mkuu wao alipowafahamisha msimamo mpya wa Chama chao wa kumtambua Rais Amani Karume, na leo ndio hawa hawa ambao wanaandamana kumuunga mkono! Ndiyo, tulilia kwa mengi. Kumbukumbu za mateso na madhila, za unyanyasaji na dhuluma, za kupoteza na kudhalilishwa ndani ya nchi yetu wenyewe. Tulilia pia kwa upya wa habari yenyewe na wingi wa maswali ambayo kwa muda ule mchache hayakuwa na majibu. Tulilia tukijiuliza, hivi sasa Habibi Kipenzi Chetu, Maalim Seif Sharif Hamad, anatupeleka wapi mama zake, dada na shangazi zake, binti na wakwe zake?

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, waheshimiwa Wazanzibari wenzangu, waheshimiwa waalikwa,

Leo hii tuna jawabu kwa kila swali tulilojiuliza na tunaona fakhari kwamba uongozi wa Chama chetu ulikuwa wa mwanzo kuja hadharani kunyoosha mkono wa ushirikiano, umoja na mshikamano kwa ajili ya nchi yetu ya Zanzibar, Tanzania, Afrika Mashariki na dunia kwa ujumla. Tunaona fakhari kwamba sisi sasa ni sehemu ya kuibadilisha nchi hii, na kwa hilo hatuna la kujutia wala hatuna la kupoteza. Wanawake wa Zanzibar hatuna cha kupoteza zaidi ya minyororo ambayo nchi yetu ilikuwa imefungwa kwa zaidi ya miaka 50 sasa!

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, waheshimiwa Wazanzibari wenzangu, waheshimiwa waalikwa,

Ni sisi wanawake ndio ambao tumekuwa tukibeba sehemu kubwa ya machungu yanayosababishwa na kufeli kwa mfumo wa siasa za Zanzibar kwa miaka yote hii 50. Hatukusudii kuwalaumu wanaume, ambao kwa miaka yote hiyo wamekuwa ndio vinara wa siasa zetu, lakini tunakusudia kusema kwamba sifa zetu za kuwa mama, dada, wazazi na walezi, ndizo zinazotufanya tuumie zaidi pale maafa yanayosababishwa na kufeli kwa siasa zetu yanapotokea.

Hapana shaka, huu si wakati wa kukumbushana wapi na vipi yalitupata yaliyotupata, lakini itoshe kunukulu msemo wa wenzetu Wanyarwanda, ambao baada ya kuangamizana kwenye mauaji ya kutisha ya miaka ya ’90, sasa wenyewe wameinuka na kusema ”NO MORE!” Basi tena! Nasi kwa pamoja, tunasema NO MORE. Basi tena!

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, waheshimiwa Wazanzibari wenzangu, waheshimiwa waalikwa,

Tunasema basi, basi tena! Basi tena kugawanywa na tugawanyika kwa misingi ya asili zetu. Basi tena kugombanishwa na tukagombana kwa misingi ya vyama vyetu. Basi tena kupiganishwa na tukapigana kutetea itikadi zetu. Basi tena kutishwa na tukaogopana kwa misingi ya visiwa vyetu. Basi tena kumpa nafasi mtu wa kando asimame baina yetu. Basi kwa kila jicho la adui na la hasidi dhidi ya nchi yetu. Basi tena kwa yote hayo, na mengine maovu zaidi ya hayo, dhidi ya nchi yetu.

Sasa, tunachokitaka sisi wanawake wa Zanzibar ni nchi yetu tu. Zanzibar hii ambayo kwa miaka 50 sasa imekuwa ikichinjwa na kukatwa vipande vipande, tuna jukumu leo hii la kuikusanyakusanya na kuileta pamoja. Na tafauti wanavyosema watu kwamba La Kuvunda Halina Ubani, Zanzibar yetu haijavunda. Bado inawezekana kuiunda tena, ikasimama kuchukua nafasi yake iliyokuwa imeshikilia kwa karne kadhaa huko nyuma, yaani kitovu cha elimu, ustaarabu na maendeleo. Na kama alivyokuwa akinadi kampeni zake Barack Obama, ambaye hata babu yake Bwana Onyango Hussein Obama, alipitia Zanzibar na kufaidika na ustaarabu wa watu wa nchi hii, YES WE CAN! Ndiyo, na sisi Wazanzibari tunaweza, na lazima tuweze.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, waheshimiwa Wazanzibari wenzangu, waheshimiwa waalikwa,

Wewe ni mtu mzima. Umeishi na kuona mengi na inshallah utaendelea kuishi na kuyashuhudia mengine tele yanayokuja. Waswahili husema Mtu Mzima Dawa, na kwamba penye Wazee hapaharibiki Jambo. Kwa hivyo, kwa kutumia utu uzima wako, nafasi yako kama kiongozi mkubwa wa Chama na nchi yetu ya Zanzibar, na juu ya yote Uzanzibari wako, tungekuomba tutumie nafasi hii tukiwa mbele yako kufikisha salamu hizi zifuatazo:

Kwa Mwenyekiti wa Chama chetu, Profesa Ibrahim Haruna Lipumba, tuna wingi wa shukrani na heshima ya hali ya juu. Ni unahodha wake imara kwa Chombo chetu ndio ambao umetuwezesha kuvuuka dhoruba na mawimbi ya kutisha katika safari yetu. Prof. Lipumba amekuwa akithibitisha uprofesa wake na kila mmoja wetu ni shahidi ya vile anavyolitimiza jukumu lake la kuwa kiongozi kwetu. Tunampongeza sana kwa kulisimamia hili hasa la kuwaona ndugu zake Wazanzibari wanakuwa kitu kimoja na kwa kujitolea kwake daima kwa ajili ya Chama na nchi yetu. Ushindi wa karibuni katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa huko Tanzania Bara usingelipatikana ikiwa si uimara wa uongozi wake.

Kwa Katibu Mkuu wa Chama chetu, Kipenzi chetu, Maalim Seif Sharif Hamad, ambaye Chama kilikupa jukumu zito la kuja hadharani kutangaza msimamo mpya kwa maslahi ya nchi yetu, tunakwambia kwamba sisi wanawake wa Zanzibar tuko pamoja nawe. Tuko pamoja na uongozi wa Chama chetu katika kuizamua Zanzibar kutoka miaka 50 ya siasa za mgawanyiko ambazo hazijawahi kuwa na faida kwa yeyote kati yetu. Tunakuomba utusamehe kwa hisia kali tulizozionesha wiki iliyopita katika viwanja hivi hivi. Tulikuwa hatujakuelewa. Sasa tumekuelewa na kutoka kwetu tegemea mashirikiano yasiyo masharti katika hili. Kwako ujumbe wetu ni mmoja tu, nao ni kwamba TULIKUPENDA, TUNAKUPENDA NA TUTAENDELEA KUKUPENDA MAANA NAWE DAIMA UMEKUWA UKITUPENDA!

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, waheshimiwa Wazanzibari wenzangu, waheshimiwa waalikwa,

Kupitia hadhara hii ya leo pia, tunamuomba Katibu Mkuu wetu, Maalim Seif, atufikishie salamu zatu kwa Rais wa Zanzibar, Mhe. Amani Karume. Uongozi wa Chama chetu umetutaka tumtambue kama rais halali wa Zanzibar. Mwanzoni tuliupinga uongozi wetu si kwa kuwa tu hatukufahamu, lakini pia kwa sababu ya kutokuiamini dhamira ya Mhe. Karume na wenzake panapohusika khatima ya Zanzibar. Tumefahamishwa na sasa tunaelekea kufahamu na kwa hivyo, sisi wanawake wa Zanzibar tunamtambua Mhe. Karume kwamba ndiye Rais wetu. Kwamba yeye ndiye mwenye jukumu la kuikoa nchi hii. Lakini tungeomba ujumbe wetu kwake uwe mfupi na wa moja kwa moja, nao ni kwamba SISI MAMA, DADA, BINTI NA WAKWE ZAKO WA ZANZIBAR TUNAKUPA IMANI YETU, TAFADHALI USIJE UKAIBWAGA CHINI!

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, waheshimiwa Wazanzibari wenzangu, waheshimiwa waalikwa,

Kwa viongozi wote wa Zanzibar kutoka pande zote mbili kuu, tupelekee ujumbe wetu kwao kwamba Waingereza husema IT TAKES TWO TANGO, na Waswahili husema kuwa KIDOLE KIMOJA HAKIVUNJI CHAWA. Ikiwa kuna sehemu yoyote duniani ambayo imethibitisha misemo hii ya Wahenga, basi ni Zanzibar. Licha ya viongozi hao kuongoza siasa za nchi hii kwa miaka yote hiyo 50, kwa kuwa kila mmoja alisimama kivyake, basi ndiyo maana Zanzibar imekwama. Kwao ujumbe wetu ni wa wazi, nao ni kwamba HESHIMA YAO KAMA VIONGOZI ITATAFSIRIWA TU KWA KUJITOLEA KWAO KWA AJILI YA ZANZIBAR. Nasi tutawaheshimu kwa kuiheshimu kwao Zanzibar, Wazanzibari na Uzanzibari!

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, waheshimiwa Wazanzibari wenzangu, waheshimiwa waalikwa,

Kwa wenzetu wa Tanzania Bara, katika wakati kama huu ambapo Wazanzibari wanatafuta njia za kuwaleta pamoja, wao ni ndugu ambao msaada wao unahitajika. Zanzibar iliyo pamoja na inayoshirikiana ina maslahi zaidi kuwa nayo kwenye Muungano kuliko Zanzibar iliyogawika. Zanzibar imara ni kwa Muungano imara na Zanzibar dhaifu ni kwa Muungano dhaifu. Kwa hivyo, ndugu zetu hawa wa damu wawe ni sehemu ya utatuzi wa matatizo yetu na wasiwe sehemu ya tatizo. Ujumbe wetu kwao ni mfupi tu, nao ni kwamba UDUGU NI KUFAANA, UDUGU SI KUFANANA!

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, waheshimiwa Wazanzibari wenzangu, waheshimiwa waalikwa,

Salamu zetu za mwisho, lakini za muhimu na za lazima ziende kwa Wazanzibari wote walio ndani na nje ya nchi. Tunakuomba Mgeni Rasmi pamoja na viongozi wenzako wote, popote mutakapokutana nao, muwape ujumbe wa wanawake wa Zanzibar kwamba milango ya nchi yao inafunguka. Ombi letu kwao ni kuwa tushirikiane ili kuhakikisha kuwa hivyo vinavyoingia ndani wakati milango hii ikifunguka, ndivyo vile vyenye kheri kwa nchi yetu. Kwa pamoja tuwe mawakala wa kuibadilisha Zanzibar na sio mawakala wa kuibakisha Zanzibar hapa ilipo au kuirudisha nyuma zaidi. TUSHIRIKIANE KUIJENGA ZANZIBAR MPYA.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, waheshimiwa Wazanzibari wenzangu, waheshimiwa waalikwa,

Sisi wanawake wa The Civic United Front (CUF – Chama cha Wananchi), kwa kusema haya tunatarajia kwamba tumemsemea kila mwenye kuitakia mema Zanzibar, Wazanzibari na Uzanzibari. Kwa hivyo, tunataka tukuhakikishie tena na tena kwamba TUNAIUNGA MKONO KAMATI YA ULINZI YA TAIFA AMBAYO KWA NIABA NA BARAKA ZA BARAZA KUU LA UONGOZI LA TAIFA LA CHAMA CHETU LIMEFANYA MAAMUZI HAYA MAZITO YA KUUTAMBUA RASMI URAISI WA MHE. AMANI KARUME. Tunaahidi kwamba tuko tayari kuyafanyia kazi maamuzi haya kwa kadiri ambavyo inatustahikia.

Zanzibaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaar! Daimaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaa!

Zanzibaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaar! Daimaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaa!

Zanzibaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaar! Daimaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaa!





Maandamano kuunga mkono Seif, Karume

14 11 2009

Friday, 13 November 2009 08:33
Mwajuma Juma, Zanzibar na Rabia Bakari, Dar

SIKU chache baada ya wafuasi wa Chama Cha Wananchi (CUF) kutaka kumshambulia Katibu Mkuu wao, Maalim Seif Sharif Hamad kwa kukubali kumtambua Rais wa Zanzibar, Amani Abeid Karume, jumuiya za chama hicho zimetangaza kuunga mkono hatua inayoashiria muafaka mpya.

Wakati Jumuiya ya Wanawake wa chama hicho (UWCUF) Zanzibar imeandaa maandamano ya kuunga mkono mazungumzo hayo, ile ya vijana imempongeza Maalim Seif kwa hatua hiyo.

Maandamano ya wanawake hao yamepangwa kufanyika Jumapili na kupokewa na Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho, Machano Khamis Ali, yakiwa na ujumbe wa kuwaeleza wafuasi hao faida ya muafaka huo.

Mkurugenzi wa Uenezi na Mawasiliano ya Umma Bw. Salim Bimani aliwaambia waandishi wa habari jana, matayarisho yote yameshakamilika na mzungumzaji mkubwa atakuwa Maalim Seif Sharif Hamad.

“Lengo kubwa ni kuunga mkono mazungumzo ya viongozi ambayo yamesaidia CUF kuondosha mpasuko wa kisiasa siku nyingi na sasa Wazanzibari wameamua kuungana na kusahau tofauti zao,” alisisitiza Bw. Bimani.

Alisema mbali na maandamano hayo viongozi wa kitaifa wameanza kufanya ziara za kutembelea majimbo na kukutana na wanachama ili waweze kuwafahamisha sababu zilizofanya Baraza Kuu la Uongozi wa CUF kumtambua Rais Karume.

Maandamano hayo yataanzia Uwanja wa Komba Wapya, kupitia Mikunguni na kumalizikia Viwanja vya Kibandamaiti.

Wakati hayo yakiripotiwa Zanzibar, jijini Dar es Salaam, Sekretarieti ya Vijana wa CUF imetoa pongezi kwa Bw. Hamad kwa hatua aliyofikia.

Mwenyekiti wa Sekretarieti hiyo, Bw. Mohamed Babua alisema kuwa hiyo ni njia muafaka ya kufikia suluhisho la amani visiwani humo.

“Kitendo cha kukutana kwa Maalim Seif na Rais Karume na hatimaye CUF kuitambua serikali ya Rais Karume ni ishara njema ya kulimaliza tatizo la Zanzibar,” alisema Bw. Babu.

Aliongeza kuwa matatizo ya kisiasa visiwani Zanzibar yamefikia katika hali mbaya sana na ni viongozi pekee wanaotakiwa kuchukua hatua madhubuti za kumaliza tatizo hilo.

“Watu wamekuwa wakipigwa mara kwa mara, kujeruhiwa vibaya, kukamatwa na kukoseshwa haki yao ya msingi ya kuandikishwa kupiga kura. Vijana wa chama cha CUF tunaamini matatizo haya na mengine yatamalizika kutokana na kitendo cha CUF kuitambua serikali ya Rais Karume na tunatoa wito kwa wanachama wote kwa ujumla kutoa nafasi kwa viongozi wetu wafikishe mwisho hatua waliyoanza ili kumaliza kabisa mtafaruku wa kisiasa Zanzibar,” alisema.

Novemba 5 mwaka huu, Rais Karume alikutana na Maalim Seif kuzungumzia mpasuko wa kisiasa wa Zanzibar ambayo pende zote mbili zilisema ni ya mafanikio makubwa.

Chanzo: Copied from Zanzinet.net





Dk. Karume: Hakuna masharti tuliyowekeana na Seif

14 11 2009

Na Mwanajuma Abdi

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Amani Abeid Karume, amesema hakuna masharti waliyowekea na Katibu Mkuu wa Chama cha CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, walipokutaka hivi karibuni, Ikulu ya Zanzibar.

Amesema hakuna masharti isipokuwa sharti lao kubwa ni kusameheana na kusahau yalitopita kwa kurejesha udugu katika kudumisha utulivu na amani kwa ajili ya kuwaletea maendeleo ya wananchi wa Zanzibar.

Rais Karume aliyasema hayo jana, wakati akizungumza na waandishi wa habari wa vyombo mbali mbali katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Zanzibar mara baada ya kuwasili akitokea Dar es Salaam, kwa ajili ya kutunukiwa Shahada ya Heshima ya Falsafa ya Udaktari wa Sayansi na Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Hubert Kairuki, shehere zilizofanyika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.

Aidha alimpongeza Maalim Seif Sharif kwa ujasiri mkubwa wa kwenda kuwatangazia wanachama wake katika mkutano wa Jumamosi iliyopita uliofanyika Kibandamaiti ya kumtambua Rais Karume.

Alifahamisha kuwa Seif baada ya kukaa na Baraza kuu la CUF, na kuona kuona Wazanzibari wote ni wamoja na inafaa washirikiane kuleta maendeleo na kulinda utulivu na amani nchini.

“Wazanzibar wote ni ndugu wasikubali kutofautishwa na visiwa vya Unguja na Pemba, na visiwa vidogo vidogo vya Tumbatu, Kojani, Fundo na Uzi, kwa vile kila mmoja anazunguka katika familia hizo hizo na wengine kuoana”, alisisitiza.

Dk. Karume alieleza siku zote anaomba dua nchi hii iendelee kuwa ya amani na utulivu, ambapo hadi sasa hakuna mtu anayebughudhiwa.

Alifahamisha kuwa, anaomba dua uchaguzi wa mwakani ufanyike kwa utulivu na amani, ambapo mtu atakayeshindwa au kushinda wapeane mikono kwa kupongezana kwa ajili ya maendeleo ya mustakabali wa Zanzibar.

Hata hivyo, aliongeza kuwa yupo tayari kuteuwa nafasi mbili za wajumbe wa CUF kuingia katika chombo cha kutunga sheria cha Baraza la Wawakilishi iwapo atapelekewa majina.

Rais Karume akiwa na mke wake, Mama Shadya Karume, walipokewa na viongozi mbali mbali wa serikali, Chama Cha Mapinduzi na vyama mbali mbali vya upinzani katika uwanja wa ndege wa Zanzibar.

CHANZO: ZANZIBAR LEO





Maalim Seif amsindikiza Karume kupokea Shahada

14 11 2009

UHUSIANO kati ya Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) Dk Amani Karume na Chama cha Wananchi (CUF), unaonekana kuendelea kuimarika baada ya viongozi wa chama hicho jana kumsindikiza rais huyo katika hafla ya kutunukiwa Shahada ya Heshima ya Uzamivu.

Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba na Katibu Mkuu Maalim Seif jana walimsindikiza Karume katika kutunukiwa shahada hiyo iliyotolewa na Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Hubert Kairuki.

Baada ya rais huyo wa Zanzibar kutunukiwa shahada hiyo, mshereheshaji alitangaza makundi ya picha za pamoja ambapo kundi la kwanza lilikuwa la Karume na viongozi wa siasa; Kundi hilo ndilo lililowashirikisha pia viongozi wa CUF.

Kabla ya kupiga picha Maalim Seif alikwenda kumpa mkono wa kumpongeza Karume akafuatia Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba na wakafuatia wengine.

Hata hivyo, viongozi hao wote jana hawakuwa tayari kuzungumzia kwa undani walichozungumza wakati walipokutana.

Rais Karume alisema tofauti kubwa iliyokuwepo visiwani humo ni ya kiitikadi za kisiasa hali ambayo alibainisha kuwa sasa imekuwa historia kutokana na CUF, kutangaza kumtambua rais huyo.

Novemba saba mwaka huu, Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif aliwatangazia mamia ya wafuasi wa chama hicho kisiwani Pemba kwamba chama hicho kimeamua kumtambua rasmi Rais Karume.

Pamoja na hatua hiyo ya CUF, kupongezwa na watu mbalimbali zikiwamo taasisi za kimataifa na mabalozi, ilikuwa mwiba kwa wanachama wa CUF, ambao wengi wao waliangua vilio baada ya kusikia kauli ya Seif.

Kauli hiyo mpaka sasa imeibua makundi miongoni mwa wanachama wa CUF, huku baadhi ya wanachama hao wakimuunga mkono Seif na wengine kumpinga.

Akizungumzia hali hiyo jana, Seif alisema kulikuwa na chuki ya dhahiri miongoni mwa Wazanzibari kwa misingi ya kisiasa na kuwa hali hiyo ndiyo iliyofanya watu wakalia kama watoto wadogo, baada ya kusikia kiongozi wao huyo kutangaza kumtambua Rais Karume.

“Kwa hatua tuliyofikia tutaiepusha nchi yetu na mambo mengi mabaya, hatua hii imefikiwa kwa maslai ya Zanzibar, tumechoswa na migogoro Zanzibar, nyiye waandhisi simnajua kuwa sisi wazanzibar tuna matatizo yetu wenyewe,… basi hayo ndo tunataka tuyamalize,†alisema Karume.

Alisema anaamini kuwa yeye na Seif ndio viongozi wakubwa Zanzibar hivyo hatua yao ya kuamua kumaliza tofauti zao za kisiasa itasaidia kuchochea maendeleo ya visiwa hivyo.

Katika hali ambayo haikuzoeleka hapo awali kwa viongozi hao wa CUF wote kwa pamoja walimpongeza Rais Karume kwa kutunukiwa shahada hiyo ya heshima na kusema kuwa alistahili kutokana na juhudi zake za kuvipatia visiwa hivyo amani na maendeleo.

Katika siku za nyuma viongozi hao wa CUF, walionekana kupinga na kukejeli kila kitu kilichokuwa kikifanywa na Serikali ya Mapinduzi na wakati mwingine hata vilivyokuwa vikifanywa na Serikali ya Muungano.

Kwa upande wake Karume alisema kwa sasa wameamua kuachana na siasa ya zamani na kuwa lengo lao ni moja tu la kuipigania Zanzibar na wananchi wake.

Alisema wameamua kushirikiana ili kuhakikisha kuwa chaguzi mbalimbali zinazo fanyika visiwani humo, haziwi chanzo cha mitafaruku bali kuwaunganisha wazanzibari.

Chama cha Wananchi CUF kila wakati kimekuwa kikipinga matokeo yatokanayo na chaguzi mbalimbali hali ambayo wakati mwingine ilisababisha umwagikaji wa damu visiwani humo.

Katika siku za hivi karibuni kulikuwa kunamsuguano mkubwa uliohusu uandikishwa katika daftari la kudumu la wapiga kura, hali iliyofanya CFU kutisha umwagikaji mwingine wa damu endapo matakwa yake yasingetekelezwa.

Kutoka Dodoma, Umoja wa wanafunzi wa vyuo vikuu Mkoani Dodoma jana walifanya maandamano ya kukipongeza Chama Cha Wananachi (CUF) kwa uamuzi wa kumtambua rais wa Zanzibar huku kukiwa na ulinzi mkali wa Polisi.

Maandamano hayo yalianzia katika viwanja vya bunge mjini Dodoma

yalipokelewa na kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni Hamad Rashid Mohamed katika viwanja wa Mwalimu Nyerere maarufu kama Nyerere Square.

Hata hivyo tofauti na ilivyotarajiwa wakati maanadamano hayo yalipotangazwa na vyombo vya habari, jana wanafunzi waliojitokeza katika maanadamano hayo walikuwa ni wachache sana idadi ambayo haikuzidi wanafunzi 50.

Katika maanadamano hayo wabunge wanne chama cha CUF walifika kwa ajili ya kuwaunga mkono wanafuzni hao ambao walikuwa pamoja na wananchi wachache waliojitokeza.

Wabunge waliokuja mjini hapa jana ni pamoja na Dk Ali Taarabu Ali (Konde),Habibu Juma Mnyaa (Mkanyageni) Salimu Hemedi (Chambani) pamoja na kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni ambae alikuwa mgeni rasmi.

Wabunge hao licha ya kuzungumzia mustakabali mzima wa mazungumzo ya Karume na Seif Shalifu Hamadi, walitumia muda mwingi katika kusifia chama  kwa madai kuwa ndicho chama pekee cha upinzani Tanzania.

“Tangu kuingia kwa mfumo wa siasa za vyama vingi CUF tumekuwa tukiongeza idadi ya wakilishi pamoja na kuibuka na ushindi mkubwa katika uchaguziwa serikali za Mitaa katika ameneo mbalimbali nchini hiyo ni dalili kuwa sisi ndio wapinzani pekee hapa Tanzania,†alisema Dk Taarabu.

Kwa upande wake Mnyaa alisema kuwa chama hicho kinachohitaji siasa safi na sio siasa za kuibiana kura kila unapofika uchaguzi.

Mnyaa pia alikosoa mapungufu ya vyama vyote ikiwemo CCM na Cuf kwa kusema kuwa hayana tija kwa wananchi wan chi masikini kama Tanzania.

Kwa ccm alisema kosa lao kubwa ni kitendo cha chama hicho kuamini kuwa kinaweza kila kitu na kwamba hakuna chama kingine kinachoweza kufanya jambo lolote isipokuwa wao hali ambayo alisema inatokana na mawazo finyu.

Aliyataja mapungufu ya cuf kuwa ni pamoja na imani kuwa hakuna kilichofanyika ndani ya ccm wakati yapo mambo mazuri ambayo chama hicho tawala kilishayafanya na hivyo akaomba hayo yaliyofanywa mazuri ni budi yaheshimiwe na kuenziwa.

Akizungumza katika mkutano huo kioongozi wa kabi ya upinzani bungeni aliwataka wanafunzi kutumia elimu yao na maarifa kwa ajili ya kudai mabadiliko ya katiba.

“Tanzania tunahitaji mabadiliko makubwa sana na kusema kweli ninyi wasomi ndio mtakaoleta mabadiliko hayo hivi inawaingia akilini kweli uchaguzi kama huu uliofanyika hivi karibuni kusimamiwa na ofisi ya Waziri Mkuu katiba hii inamapungufu makubwa sana,†alisema Mohamed.

Alitumia muda huo pia kuwataka wanafunzi pamoja na Watanzania kuendelea kumpigia debe mwenyekiti wa chama hicho Prof Ibrahim Lipumba kuwa bado anazo sifa za kugombea urais wa nchi.

Kiongozi huyo alisema kuwa Lipumba ameshaanza kufahamika na wananchi hivi sasa na hivyo wawapuuze wale wanaosema kuwa asigombee urais kwa kisingizio cha kuwa ameishiwa sera jambo alilosema kuwa hata Viongozi wengi barani Afrika huingia kwa kutambulika kwanza.