TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 18 Septemba 2009
”NEC NI SEHEMU YA UCHAFUZI UNAOFANYIKA Z’BAR”
Kufuatia habari iliyochapishwa katika gazeti la leo la Mwananchi ambayo imemnukuu Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Lewis Makame, akisema kwamba Tume yake haihusiki na matatizo yanayojitokeza katika zoezi la uandikishaji wapiga kura kisiwani Pemba kwa kuwa jukumu hilo linasimamiwa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) peke yake, Chama cha Wananchi (CUF), kinatoa kauli ifuatayo:
Kwanza, Jaji Makame anaudanganya umma wa Tanzania na ulimwengu kwa ujumla kwa kuzitenganisha Tume hizi mbili (ZEC na NEC) kama vile ni taasisi zisizo na uhusiano wowote kikazi. Ukweli ni kuwa, NEC inaitumia ZEC kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano kama wakala wake kwa chaguzi za Rais na Wabunge wa Jamhuri ya Muungano zinazofanyika Zanzibar na, kwa hivyo, uchafu wowote unaofanywa na ZEC visiwani Zanzibar ni uchafu pia ni wa NEC.
Uandikishwaji unaofanywa na ZEC hivi sasa Pemba na Unguja, unafanywa pia kuwaandikisha wapiga kura kwa ajili ya chaguzi za Rais na Wabunge wa Jamhuri ya Muungano kinyemela, huku NEC ikifahamu hilo. Maana yake ni kwamba wanaoandikishwa na ZEC ndio watakaopiga kura kwenye uchaguzi unaosimamiwa na NEC. Inachofanya NEC baada ya kupokea data za wapiga kura kutoka ZEC ni kuwajazia wale wachache ambao ZEC haikuwaandikisha kwa ajili ya uchaguzi wa Muungano. Kwa hivyo, kama kweli Jaji Makame anataka kuivua Tume yake na uchafu huu, afuate Katiba ya Jamhuri ya Muungano (Kif. Na. 5) kwa NEC yenyewe kuratibu uandikishaji na upigaji kura kwa ajili ya chaguzi za Muungano zinazofanyika Zanzibar. Bila ya kufanya hivyo, NEC itaendelea kuwa sehemu ya uharamia unaoratibiwa na ZEC na inabeba lawama zile zile ambazo ZEC inazibeba.
Pili, chini ya Jaji Makame, NEC imekuwa nyenzo kubwa ya kuvunja Katiba na kuwagawa Watanzania baina ya wale wa Tanzania Bara na wa Zanzibar kwani inatumia taratibu mbili tafauti inapowaandikisha kutumia haki yao ya kupiga kura. Ambapo mpiga kura wa Rais na Mbunge wa Jamhuri ya Muungano aliye upande wa Bara hatumii kitambulisho cha uraia wala cha ukaazi kujiandikisha, yule wa Zanzibar analazimishwa kuandikishwa kwa sheria iliyokwenda kinyume na Katiba ya Zanzibar ambayo inatambua kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi kama sharti la pekee la kuwa mpiga kura.
Matokeo yake ni kuwa Watanzania hawa wawili wanamchagua Rais na Mbunge wa Jamhuri katika uchaguzi mmoja lakini kwa kutumia taratibu tafauti. Huo ni upotofu wa kimakusudi ambao NEC inaujua, lakini inaufanya kwa kuwa imeamua kuwa sehemu ya uharamia unaofanyika Zanzibar.
Tatu, kutokana na kwanza na pili hapo juu, tunataka yafuatayo yafanyike:
i. Kama kweli Jaji Makame anakiamini anachokisema, basi Tume yake isitishe mara moja kuifanya ZEC kuwa wakala wake na pia iwache kutumia Daftari la Kudumu la Wapiga Kura linaloratibiwa na ZEC, kwani kuendelea kufanya hivyo ni kuvuja Katiba zote mbili na kujipaka uchafu.
ii. Kwa kuwa hapa pana uvunjwaji wa wazi wa Katiba ya nchi, tunaiomba juumuiya ya wanasheria nchini wauone ukiukwaji huu na washirikiane nasi kulipatia tatizo hili ufumbuzi wa kisheria. Ni aibu kwa nchi yenye wasomi wa Sheria kama yetu na kwa taasisi inayoongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu kama NEC kuendelea kuvumilia uvunjaji wa Katiba na ukiukwaji wa sheria.
iii. Kwa kuwa jumuiya ya kimataifa ndiyo ambayo inafadhili uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura pamoja na shughuli zote za chaguzi, tunaiomba ifikirie upya namna kodi za wananchi wao zinavyotumiwa na ushirikiano wa ZEC/NEC katika kuizika demokrasia nchini Tanzania.
iv. Kwa kiwango hiki cha udhaifu kinachooneshwa na NEC, msimamo wa Profesa Haruna Lipumba wa kwamba Tume hii ijiuzulu unaendelea kuthibiti.
Imetolewa na:
Salim Bimani,
Mkurugenzi wa Uenezi na Mahusiano na Umma, CUF
Simu: +255 777 414 112
E-mail: cufhabari@yahoo.co.uk
Weblog: www.hakinaumma.wordpress.com
Maoni