Friday, 25 September 2009 16:58
* Msekwa ahofia yaliyotokea Kenya, Zimbabwe
* CUF yasema hatudanganyiki, huo ni usanii
Na Reuben Kagaruki
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimezinduka na kutangaza kuwa hakitasubiri machafuko yaliyotokea Kenya na Zimbabwe yatokee Zanzibar ndipo kiunde Serikali ya Umoja wa Kitaifa visiwani humo.
Kauli hiyo ya CCM imetolewa huku zikiripotiwa vurugu za mara kwa mara visiwani humo za kupinga utaratibu wa uandikishaji wananchi kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga kura kutokana na vikwazo katika utoaaji wa vitambulisho vya ukaazi, kiasi cha kusababisha Jeshi la Polisi kutumia mabomu kutuliza hali hiyo.
Akihojiwa katika kipindi cha Jambo Tanzania kilichotangazwa Dar es Salaam jana na Televisheni ya Taifa (TBC1), Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara), Bw. Pius Msekwa alisema kuwa chama chake kinatambua kuwa Zanzibar kuna tatizo.
“Tunafikiria kuwa na Serikali ya Umoja wa Kitaifa. Tatizo ni mfumo tulionao mtu akishindwa kwa kura chache anabaki nje ya Serikali,” alisema Bw. Msekwa na kutahadharisha kuwa;
“Msingojee matatizo yatokee kama ya Zimbabwe na Kenya ndipo iundwe Serikali ya kitaifa…hayo ndiyo tunayozungumzia.”
Alitolea mfano uchaguzi wa mwaka 1995 ambapo mgombea wa CCM, Dk Salmin Amour (Komandoo) ilipata ushindi wa asilimia 50.2 na chama kilichofuatia (CUF) kilichoapata asilimia 49.8 kikawa nje ya Serikali. “Hii siyo hali nzuri,” alionya Bw. Msekwa.
Bw. Msekwa lizidi kutolea mfano tofauti iliyokuwepo kwa upande wa Baraza la Wawakilishi akisema chama kimoja (CCM) kilikuwa na wawakilishi 29 na kingine (CUF) 24.
Hata hivyo, alisema matatizo ya Zanzibar hayakuanza leo bali ni ya tangu nchi hiyo inatawaliwa Uingereza ambapo kwenye uchaguzi wa kwanza zilitokea vurugu na kwa kumbukumbu zake watu 30 walikufa.
Bw. Msekwa alisema hali ya kutokubali matokeo iliendelea na utulivu uliokuwepo uliletwa na mfumo wa chama kimoja uliokuwa umeanzishwa.
“Mfumo huu wa vyama vingi ulipoanzishwa matatizo ndipo yalipoanzia, mwaka 1995 tukapata muafaka lakini haukuleta mafanikio, mwaka 2005 muafaka haukutusaidia, tunaendelea,” alisema Bw. Msekwa.
Lakini kauli hiyo ya Bw. Msekwa ilipokewa kwa shingo upande na chama cha CUF na kuibatiza kuwa ni usanii wa kisiasa.
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Umma wa CUF, Bw. Salim Biman, alisema, “Mpango huo ni usanii wa kisiasa, kwanza hatuwezi kumwamini (Msekwa) kwa kuwa anatofautiana na mwenyekiti wake.”
Bw. Biman alisema CUF haiwezi kukaa kwenye mazungumzo tena kwa kuwa muafaka ulishafikiwa na kinachosubiriwa ni utekelezaji. “Tulishakubaliana muundo wa Serikali ya umoja utakavyokuwa, wao (CCM) walienda Butiama wakarudi na pendekezo la kura za maoni, kama wanataka wakutane makatibu wakuu wa vyama kwa ajili ya utekelezaji,” alisema Bw. Biman
Muafaka ulitolewa na chama cha CUF kikidai ndiyo makubaliano ya kamati ya muafaka na CCM, unaitaka katiba ya Zanzibar iwe na kifungu kinachoainisha kuwa Naibu wa Kwanza wa Rais ni Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi/Baraza la Mawaziri.
Kwa mujibu wa makubaliano hayo, ambayo CCM iliyakana, kutakuwa na Msaidizi Mkuu wa Rais kuhusu mambo yote ya Zanzibar ambaye atamsaidia Rais kufuatilia utekelezaji wa siku hadi siku wa Mambo ya Muungano katika Zanzibar.
Pia, kikatiba, ndiye atafanya kazi zote atakazoagizwa na Rais, na atakaimu urais wakati Rais hayupo nchini.
Pia kutakuwa na Manaibu wawili wa rais, Naibu wa Kwanza anakayetoka chama cha pili katika uchaguzi na Naibu wa Pili atakayetoka chama sawa na kilichomtoa rais.
Pia iliainishwa kuwa Rais atashirikiana na Naibu wa Kwanza wa Rais katika uundaji wa Baraza la Mawaziri, Baraza la Mapinduzi na nafasi zipi chama chake kinazostahiki kupata.
Muda wa kushika madaraka wa mtu aliyechaguliwa kuwa Naibu wa Kwanza wa Rais utakuwa sawa na ule wa Rais na mazingira ya kuacha madaraka yatakuwa sawa na yale yanayomhusu Rais.
Ikitokezea kwamba kiti cha Naibu wa Kwanza wa Rais kikawa wazi kutokana na masharti hayo ya kikatiba, Rais atamteua mtu mwingine atakayependekezwa na chama cha siasa alichotoka Naibu wa Kwanza wa Rais aliyekuwa akishikilia nafasi hiyo kuwa Naibu wa Kwanza wa Rais kwa muda uliobakia.
Mbali na kuzungumzia umuhimu ya serikali ya umoja wa kitaifa, Bw. Msekwa alisema malumbano ambayo yamekuwa yakiendelea ndani ya Baraza la Wawakilishi na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, yanadhohofisha nguvu za chama na kukifanya kishindwe kuelekea kinapotaka kwenda.
“Malumbano yanadhohofisha nguvu ya pamoja ya kutaka kuelekea kule tunapotaka kuelekea,” alisema Bw.Msekwa.
Alisema kutokana na hali hiyo, ndiyo maana Mwenyekiti wa CCM (Rais Jakaya Kikwete) kwa kutumia busara zake aliamua kuunda kamati ili kufuatilia hali hiyo na kutoa mapendekezo ya kuiondoa.
Aliongeza kuwa hatua ya kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kukutana na kuunda kamati ambayo yeye ni mjumbe ni utaratibu wa kawaida ndani ya chama. Wengine wanaounda kamati hiyo ni Bw.Abdulrahaman Kinana na Rais Mstaafu, Mzee Ali Hassan Mwinyi anayeiongoza.
“Hii siyo kwamba imetokea mara ya kwanza kwenye NEC, miaka yote tumekuwa tukizungumzia hali ya siasa, katika kikao kilichopita tukaelekeza macho yetu katika malumbano yaliyotokea katika Baraza la Wawakilishi na Bungeni,” alisema
Chanzo: Majira
Maoni