Salma Said, Zanzibar
BAADHI ya wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM Zanzibar, wameshtushwa na matokeo ya utafiti wa masuala ya kisiasa, kijamii na kiuchumi yanayoonyesha kuwa katibu mkuu wa CUF, Seif Sharif Hamad anapewa nafasi kubwa ya kushinda kiti cha urais wa visiwa hivyo mwakani.
Ripoti hiyo iliyotolewa juzi na kampuni ya Synovate, pia inaonyesha kuwa waziri kiongozi wa zamani wa Zanzibar, Gharib Mohammed Bilal wa CCM ndiye anayefuatia kwa karibu Maalim Seif kumrithi Rais Amani Abeid Karume, ambaye anamalizia muda wake wa miaka 10.
Ingawa kamati hiyo kuu ya CCM upande wa Zanzibar ilikuwa ikiendelea na kikao chake cha kawaida jana, ripoti ya matokeo ya utafiti huo haikujadiliwa, lakini wajumbe walioongea na Mwananchi nje ya ukumbi wa mkutano wa ofisi kuu ya CCM Kisiwandui, walionekana kutofautiana.
Wengi walionyesha kushtushwa na matokeo yanayompa nafasi kubwa Bilal kwa upande wa CCM, wakisema chama hicho hakiwezi kumteua mtu kwa sababu ya umaarufu wake.
“Kwanza mimi ni maarufu kuliko yeye kwa sababu mimi nimeshawahi kushika nyadhifa mbalimbali katika chama chetu nikianzia chini hadi juu,” alisema mjumbe mmoja nje ya ukumbi wa mikutano wa chama hicho ulio Kisiwandui.
“Nimeanza siasa tangu nikiwa mdogo. Tumuulize yeye (Bilal) anatoka wapi na amefanya nini katika chama,” alihoji mjumbe huyo ambaye yeye pia anatajwa kutaka kuwania urais Zanzibar.
Alisema licha ya Bilal kuwahi kuwa waziri kiongozi na kwa sasa kuwa mjumbe wa NEC, uzoefu wake katika siasa ni mdogo na pia hana jambo kubwa aliloifanyia CCM.
Mjumbe mwingine wa NEC ambaye ni waziri katika Serikali ya Muungano alisema haiwezekani utafiti umpe nafasi kubwa Dk. Bilal, ambaye ni mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma.
“Wewe ngoja huo uchaguzi uje utashangaa kitakachotokea,” alisema waziri huyo ambaye kama wengine aliomba jina lake lihifadhiwe.
Katika utafiti huo, Synovate walihoji ni kiongozi gani ambaye wananchi wa Zanzibar wanampa nafasi ya urais baada ya Karume kustaafu mwakani na asilimia 28 ilionyesha kuwa ni Maalim Seif, wakati asilimia 24 ilionyesha ni Bilal. Waziri kiongozi wa sasa, Shamsi Vuai Nahodha alipata asilimia 10 na Makamu wa Rais Mohamed Shein alipata asilimia 2.
“Sidhani kama huo utafiti upo sawa kwa sababu kwanza umefanywa wapi, katika mazingira gani na akina nani waliohojiwa maana inawezekana ukaenda sehemu moja; ukawauliza watu 1,000 kuhusu mtu mmoja ambaye ni wa kwao na ana nafasi kubwa. Unategemea watu hao wakuambie nini, hawamtaki,” alihoji mmoja wa wajumbe wa NEC Zanzibar.
Mjumbe mwingine alisema kuwa, suala la umaarufu halina nafasi katika siasa za Tanzania kwa kuwa huko nyuma imeshawahi kutokea mtu asiyekuwa maarufu kushinda na kuchaguliwa kuwa rais kuliko aliyekuwa maarufu.
“Ngoja nikuambie unakumbuka mgombea wa urais wa Zanzibar mwaka 2000 alikuwa nani? Unakumbuka kama Dk Bilal ndiye alikuwa maarufu, je, alipata?” alihoji mjumbe huyo.
“Na je, nani alitarajia kama Amani Karume atakuwa rais? Yeye si aliangushwa kwa kura nyingi sana na watu pia hawakumtaka, lakini je, hakuwa rais? Kwa hivyo kigezo cha kuwa maarufu kisitumike kabisa!”
Bilal pia alichukua fomu za kuwania urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM mwaka 2005, lakini alienguliwa katika uteuzi wa mwisho mjini Dodoma kutokana na utamaduni wa chama hicho wa kumwachia mshindi wa kiti cha urais amalizie kipindi chake cha miaka 10.
Mwenyekiti wa Vijana wa CCM, Hamad Masauni Yusuf alisema ingawa hajui vigezo vilivyotumika katika utafiti, anaamini kuwa wananchi wengi bado wana kasumba kwamba CUF bado ina ngome kubwa kisiwani Pemba wakati hali sasa ni kinyume.
Alisema sio kweli kwamba, CUF wana nafasi kubwa ya kushinda urais kwa Zanzibar na pia huko Pemba na kwamba hali imebadilika kwa sasa akidai kuwa, wananchi wengi wamekata tamaa na viongozi wao na hivyo, CCM ina nafasi kubwa ya kushinda.
“Nimetoka Pemba hivi karibuni na hali ilivyo sasa sivyo kama ilivyokuwa awali,” alisema Masauni.
Hata hivyo, Masauni alisema CCM haiwezi kumteua mtu asiyekuwa safi na kwamba lazima awe na sifa zinazokubalika.
Aliyekuwa Afisa katika ubalozi wa Tanzania nchini Geneva, Mohammed Yusuf alisema tafiti zinazofanywa katika nchi za Afrika huwa zinatumia vigezo vya nchi za Magharibi, jambo ambalo alisema halitoi picha halisi ya kile kinachokusudiwa.
Jijini Dar es salaam, wasomi na wanasiasa walikuwa na maoni tofauti kuhusu utafiti huo wakizungumzia sababu za Rais Jakaya Kikwete kukubalika huku watendaji wake wakionekana hawafai.
“Katika siasa, hili ni tatizo kubwa na linatakiwa litafutiwe ufumbuzi kwani hatuwezi kuangalia uzuri wa mtu mmoja katika taasisi nzima. Taasisi ni muhimu kuliko mtu mmoja kwani mtu huyo anaweza kuondoka na kuiacha taasisi,” alisema mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Audax Kweyamba.
Lakini alisema inashangaza kuwa mfumo mzima wa uongozi kuanzia bunge na baraza la mawaziri wanakabana koo, isipokuwa pale inapofikia suala linalomhusu rais ambalo hufanya pande zote kumtetea, jambo linalomfanya awe maarufu.
“Haiwezekani wabunge na mawaziri wakabane koo, lakini inapofikia suala linalomhusu rais, wanamlinda na kumfanya kama malaika wakiwa na lengo maalumu na sio kufichua uovu wake,” alisema Kweyamba.
Mhadhiri mwingine wa UDSM, John Jingu alisema matokeo ya utafiti huo yanategemeana na watu waliohojiwa.
Hata hivyo, utafiti huo katika kipengele cha viongozi wa kisiasa uliangalia umaarufu wa viongozi na ulihoji watu 2,000 walio Bara na Visiwani, wakati katika kipengele cha urais wa Zanzibar uliangalia nani mwenye nafasi kubwa ya kumrithi Rais Karume.
Aidha, baadhi ya wahadhiri ambao hawakutaka kutajwa majina yao walisema upande wa upinzani, hasa Chadema, umepata asilimia kubwa kutokana na kuibua kashfa nyingi za mikataba mibovu bungeni na kuwataja mafisadi.
Nao viongozi waandamizi wa vyama vya CCM, Chadema, TLP na CUF wameeleza wazi kwamba, hawakubaliani na mfumo uliotumika katika kupata matokeo ya utafiti huo.
Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM- Itikadi na Uenezi, John Chiligati alisema anakubaliana na utafiti huo kuonyesha kwamba, Rais Kikwete anaongoza kwa umaarufu, lakini akasema watafiti wamepotoka upande wa Zanzibar, ambako katibu mkuu wa CUF, Seif Sharif Hamad ameonekana ndiye anayeweza kushinda uchaguzi wa mwaka 2010.
Chiligati, ambaye pia ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, alisema ni sahihi kwa utafiti huo kuonyesha kuwa Rais Kikwete anaongoza kwa kukubalika, lakini akapingana na kipengele cha mrithi wa Rais Karume akisema CCM imefanya makubwa visiwani humo.
“CCM imefanya mengi mazuri Unguja na Pemba na ukienda kumuuliza Mzanzibari yeyote, atakueleza safari hii CCM wameleta mabadiliko,” alisema Chiligati ambaye ni mbunge wa Manyoni Mashariki.
Alitaja miongoni mwa mambo ambayo anafikiri yanampa nafasi kubwa ya ushindi mgombea yeyote watakayemsimamisha kuwa ni ujenzi wa barabara, usambazaji wa maji safi na umeme.
Mwenyekiti wa vijana Chadema, John Mnyika, alisema utafiti huo haukuzingatia suala la ufisadi wala rushwa na kwamba kama ungezingatia masuala hayo, CCM isingepata kura za juu.
“Hii taasisi haikutenda haki kwani maswali mengi katika utafiti wao yalikuwa yanahusu elimu, jambo ambalo lazima CCM ipate kura nyingi, lakini ingegusia masuala ya rushwa na ufisadi, hali ingekuwa nzuri zaidi kwa vyama vya upinzani na haki ingeonekana kutendeka pia,” alisema.
Alisema taasisi zinatakiwa kujitokeza kwa wingi ili kufanya utafiti wa kina wa kura za maoni, na sio kutegemea zile zinazotumiwa na serikali ambazo zinaipandisha juu bila ya kuzingatia ukweli uliopo.
Mkurugenzi wa uenezi na mawasiliano wa CUF, Ashura Mustafa alisema matokeo hayo yanalenga kuifanya jamii ya Kitanzania iamini kuwa, CUF ina nguvu upande wa Zanzibar pekee na pia kuwafanya wananchi wa visiwa hivyo wasiwe na imani na Prof Lipumba.
“Wameonyesha kuwa, Maalim Seif ndiye anayekubalika kwa upande wa Zanzibar ili wananchi wasiwe na imani na rais wetu mtarajiwa Lipumba, lakini pia wanataka kuonyesha kuwa CUF inakubalika Zanzibar tu ili hata wananchi wasimchangue mgombea wetu kwa upande wa urais,” alisema Mustafa.
Alisema CUF ina nguvu kubwa ya kisiasa kwa upande wa Tanzania Bara kutokana na kuwa na uongozi kuanzia ngazi ya mtaa mpaka taifa tofauti na Chadema ambayo alisema haina uwakilishi kuanzia ngazi za chini.
Pia alipinga ripoti hiyo akidai kuwa idadi ya watu 2,000 waliohojiwa haiwezi kuwakilisha idadi ya Watanzania zaidi ya milioni 40.
Naye mwenyekiti wa TLP, Augustine Mrema alichukulia matokeo hayo ya umaarufu kuwa ni kielelezo cha wanasiasa watakaogombea urais mwaka 2010 na hivyo kuielezea kampuni hiyo ya utafiti kuwa si wakweli kwa kuwa ameshatangaza kuwa hatagombea urais mwakani.
“Kwanza wamenidhalilisha kwa kuwa nimeshatangaza kutokugombea tena urais na hata chama changu kinajua hilo, sasa inakuwaje tena leo utafiti umhusishe Mrema?” alisema na kuunga mkono asilimia za Kikwete akisema kuwa amejitahidi kupambana na ufisadi.
Chanzo: www.mwananchi.co.tz
Maoni