Kambi ya upinzani yasikitishwa na kesi za wakubwa kusikilizwa kwa kasi

30 06 2009

Na Leon Bahati, Dodoma

KAMBI ya upinzani bungeni imesema inasikitishwa na mtindo wa kesi zinazowahusu watu wenye uwezo kuendeshwa haraka na za walala hoi kuchukua muda mrefu mahakamani bila kusikilizwa.

“Kuna watu wengi ambao wamekaa mahabusu kwa muda wa miaka mingi wakisubiri kesi zao kusikilizwa, lakini kuna baadhi ya kesi ambazo uendeshaji wake umekuwa ukifanywa kwa kasi ya ajabu-Super-sonic speed,” alisema jana Msemaji wa Kambi ya Upinzani Bungeni (Sheria na Katiba) Fatma Mussa Maghimbi (Chake Chake- CUF).

Maghimbi alikuwa akichangia makadirio na matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka 2009/10 na kufafanua kuwa kesi zinazoendeshwa kwa kasi, zimekuwa zikizikilizwa kila wiki na mara nyingine kwa zaidi ya siki moja kwa juma.

Alisema tabia hiyo, inaashiria ubaguzi wa sheria nchini na kusabababisha wananchi kuhoji maswali mengi kuhusiana na kesi za watu wenye uwezo zinavyoendeshwa kwa kasi.

“Watanzania wanajiuliza je, kasi ya aina hii inafanyika kwenye kesi za wakubwa tuu au ndio kusema kuna double standards katika utoaji wa haki,”alihoji Maghimbi.

Maghimbi alisema tatizo la ucheleweshaji wa kesi nchini, limekuwa sugu na kwamba kitendo hicho kimekuwa kikiathiri haki.

Alitaja baadhi ya sababu zinazochangia kuchelewa kwa kesi hiyo kwamba ni idadi ndogo ya mahakimu na majaji na kwamba serikali inapaswa kuongeza mahakimu na majaji ili kuleta ufanisi zaidi katika idara hiyo.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe katika hotuba yake, alisema kesi zinazosikilizwa hivi sasa zinarekodiwa tofauti na hakimu au majaji kuandika wakati kesi zikizikilizwa.

Jaji Mkuu Augustino Ramadhan aliwahi kuliambia gazeti hili kuwa wakipatiwa vifaa vya kurekodi, kasi ya kusikiliza kesi itaongezeka na hivyo kuondoa mlundikano wa kesi mahakamani.

Alisema mtindo huo, umekuwa ukitumika katika nchi zilizoendelea na umeonyesha mafanikio makubwa tofauti na sasa.

Chanzo: http://mwananchi.co.tz





CUF wasema kauli ya Waziri Seif kuhusu Jumbe ni ya mfa maji

30 06 2009

Na Salim Said

SIKU moja baada ya Waziri Mohammad Seif Khatib kudai bungeni, Maalim Seif Sharif aliyesababisha kufukuzwa kwa rais wa awamu ya pili wa Zanzibar, Aboud Jumbe Mwinyi, baadhi ya viongozi wa CUF wamesema waziri huyo, ameshindwa kujibu hoja iliyokuwa mbele yake.

Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere alimfukuza Mzee Jumbe kwa tuhuma kwamba alikuwa na ajenda za siri za hatima ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwamba aliandaa ajenda ya kudai serikali tatu badala ya mbili zilizopo hivi sasa.

Akizungumza Bungeni mjini Dodoma juzi, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Mohammed Seif Khatib alisema fitna za kishushu za Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) maalim Seif Sharif Hamad, zilisababisha Jumbe aondolewe madarakani.

Wakizungumza na Mwananchi kwa nyakati tofauti jijini Dar es Salaam jana, viongozi wa CUF walisema Wazir Khatib alitoa tuhuma hizo baada ya kushindwa kujibu hoja ya msingi iliyokuwa mezani.

Naibu katibu Mkuu wa CUF Zanzibar, Juma Duni Haji alisema baada ya kujibu hoja husika, Waziri Khatibu aliamua kusambaza fitina ambazo zinaweza kujenga chuki na uhasama katika jamii.

“Hoja iliyokuwepo mezani ni kero za Muungano ambazo zinasababishwa na mkataba wa muungano. Aliambiwa aipeleke hoja hiyo mezani ili ijadiliwe, lakini alishindwa kujibu hoja hiyo na ndio maana akaamua kutoa porojo na maneno ya mfa maji,” alisema Duni.

Duni ambaye pia ni Mkurugenzi wa Fedha na Uchumi wa CUF alisema suala la kutimuliwa kwa Jumbe ni mfano mzuri wa kero za Muungano zinazolalamikiwa na Watanzania wengi.

“Ok, kama hivyo ndivyo, Jumbe alifukuzwa pekee, lakini maalim Seif alifukuzwa na wenzake saba, je alitiliwa fitna na nani,” alihoji Duni.

Mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa wa CUF, Jussa Iismail Jussa, alisisitiza kuwa waziri Khatib alikwepa kujibu hoja ya msingi kuhusu kero za Muungano na kuamua kuingiza malumbano ya kisiasa katika hoja ya msingi ili kutimiza malengo yake.

“Waziri Khatib anataka kugombea urais Zanzibar na ndio mana anajipendekeza sana kwa viongozi wa CCM bara, kwa sababu Halmashauri Kuu ya CCM ndiyo inayochagua wagombea. Hivyo anawaheshimu na kuwatetea sana na kuwavunjia heshma wazanzibari ambao anataka kuwaongoza huku akidharau maslahi yao, lakini je atawaongoza vipi watu asiowaheshimu.

“Wazir Khatib anakwepa kujibu hoja ya msingi na kuingiza malumbano ya kisiasa katika hoja ya msingi yenye maslahi kwa Watanzania waliowengi ili kutimiza malengo yake,” alisema Jussa.

Naye Mbunge wa Wawi Kisiwani Pemba (CUF) Hamad Rashid Mohammed alisema anasikitika kuwa maalim Seif si mbunge, kwa sababu kama angekuwa mbunge angelidai ushahidi wa tuhuma zilizozungumzwa na Waziri Khatib.

“Lakini hata hivyo anaweza kutumia vyombo vingine vya kisheria na kikatiba kudai ushahidi wa tuhuma hizo,” alisema Mohammed.

Mohammed ambaye pia ni kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni alisema, kilichomfukuzisha Jumbe ni kudai serikali tatu jambo ambalo lilipingwa vikali na Itikadi, Sera, Ilani na msimamo wa CCM.

Chanzo: http://mwananchi.co.tz





Muungano watikiswa tena Bungeni

30 06 2009

Wapinzani wautikisa Muungano bungeni
• Wadai ofisi za Pinda, Vuai hazina mamlaka sawia

Na Martin Malera, Dodoma

CHOKOCHOKO za kuutikisa Muungano zimeanza tena baada ya wabunge wa kambi ya upinzani kutaka kuundwa kwa Serikali ya Tanganyika pamoja na kutaka mkataba wa uanzishwaji wake upelekwe bungeni ujadiliwe ili kuondoa kero zilizopo.

Msimamo huo wa kambi ya upinzani ulitangazwa bungeni jana na msemaji wa kambi hiyo, Riziki Omar Juma (CUF), wakati akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), kwa mwaka wa fedha 2009/2010.

Kambi hiyo ilisema, inajua kuna vikao vya kutatua kero za Muungano, lakini hawaoni uhalali wake pamoja na utayari wa kulitatua tatizo lenyewe kwa kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Waziri Kiongozi wa Zanzibar hazina mamlaka ya kulizungumzia.

“Tungependa mkataba wa makubaliano ya waasisi wa Muungano uletwe bungeni ili tuanze kuujadili kwa lengo la kutatua kero za Muungano kwa nia ya dhati kuliko kuendelea na vikao ambavyo hatuvioni kama vina uhalali,” alisema Riziki.

Aidha, kambi hiyo pia imeliomba Bunge kuiagiza serikali isitishe mara moja vikao hivyo na badala yake mkataba wa Muungano upelekwe bungeni kama mwanzo mkuu wa kutekeleza kwa vitendo dhamira ya kutatua kero za Muungano.

Kwa mujibu wa kambi hiyo, tatizo la Muungano si mgawo wa asilimia 4.5 kutoka Serikali ya Muungano kwenda kwa Zanzibar; si Zanzibar kuwa na au kutokuwa nchi ndani ya Muungano; si nishati za gesi na mafuta kuwa au kutokuwa za Muungano; si Zanzibar kujiunga na au kutokujiunga na Jumuiya ya Nchi za Kiislamu Duniani (OIC).

Aliongeza kuwa, tatizo si Wazanzibari kushikilia nafasi katika Serikali ya Muungano katika mambo ambayo si ya Muungano wakati ambapo Watanganyika hawawezi kufanya hivyo katika Serikali ya Zanzibar, bali ni kutoheshimiwa kwa mkataba wa Muungano tangu mwanzo.

Riziki alisema namna Serikali ya Muungano inavyofanya kazi kushughulikia matatizo ya Muungano, ni kama haitaki kusikia upande mwengine wa mawazo, kwani inapenda kujifungia chumbani na kujisikiliza yenyewe ndani ya viambaza vinne.

“Mheshimiwa Spika, tunasema hivi kwa kuwa zile hoja za msingi tunazozitoa kuhusu matatizo ya Muungano, hazionekani kabisa kupewa nafasi katika maamuzi ya vipi Muungano huu uendeshwe,” alisema Riziki.

Alibainisha kuwa, mara kadhaa huko nyuma wameshawahi kueleza kuwa, tatizo kubwa la Muungano huu ni kutokuheshimiwa kwa mkataba wake uliouunda, Katiba ya Jamhuri ya Muungano kukiuka kwa kiasi kikubwa, makubaliano hayo, hivyo ni katiba iliyokwenda kinyume na msingi iliyoiunda.

“Muungano huu haukuundwa, na wala hautakiwi uongozwe na katiba zote mbili – ya Muungano na ya Zanzibar, zilichotakiwa kukifanya, ni kuutafsiri mkataba ule tu, na si vinginevyo,” alisema Riziki.

Kwa mujibu wa kambi hiyo, asili ya Muungano ilitokana na sababu tatu kuu, ambazo ni udugu wa kihistoria baina ya watu wa Tanganyika na Zanzibar, vuguvugu la kulileta pamoja Bara la Afrika, maarufu kama ‘Pan-Africanism Spirit’, na zile hisia kwamba umoja ni nguvu (United We Stand), na sababu nyingine inayotajwa ni kuipatia ulinzi Zanzibar, ambayo siku 100 tu kabla ya Aprili 26, 1964 ilikuwa imefanya mabadiliko ya utawala kwa njia ya mapinduzi.

Aliongeza kuwa, mkataba wa Muungano ulisainiwa na mwakilishi wa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, Marehemu Rais Abeid Karume na wa Jamhuri ya Tanganyika, Marehemu Rais Julius Nyerere ambapo walioutia saini ni wawakilishi wa Tanganyika na Zanzibar na ndiyo unaojenga hoja ya ukosefu wa uhalali kwa kikao chochote cha kuujadili Muungano ambacho hakihusishi pande husika za mkataba wenyewe.

“Sisi wa kambi ya upinzani tunaamini kwamba, ni kosa kubwa dhidi ya sheria zinazolinda mikataba ya kimataifa na kwa hakika, ni hatua ya hatari kwa hatma njema ya Muungano huu, kwa ofisi za Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (ambayo Zanzibar ni sehemu yake) na Waziri Kiongozi (ambayo ni ya Zanzibar tu) kama mwasisi wa Muungano wenyewe, kujadili mustakbali wa Muungano.

“Tunajenga hoja hii kuhusiana na hili: kwanza, wanaostahili kuujadili na kuutolea maamuzi Muungano ni Serikali ya Zanzibar na mwenzake aliyetiliana saini mkataba wa Muungano, ambayo ni Serikali ya Tanganyika. Uongozi wa serikali hizo ndio waliokuwa washiriki wa mazungumzo ya kuunda Muungano kwa niaba ya nchi zao.

“Pili, kilichotokea mwaka 1964 ni Kiongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na Kiongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Tanganyika kukubaliana kuanzisha ushirika wao unaoitwa Muungano.

“Katika kulinda heshima za mataifa yao, viongozi hao waliweka saini mkataba wa makubaliano yao, ambao una kila sifa ya kuwa mkataba wa kimataifa unaostahiki kuheshimiwa na pande husika na, tatu, kutokana na kwanza na pili hapo juu, kwa hivyo, ni upotoshaji wa makusudi kuuchukua mjadala wa nchi mbili zilizoungana na kuukabidhisha mikononi mwa vyombo visivyohusika na kuvipa vyombo hivyo mamlaka ya kufanya maamuzi yote,” alisema Riziki.

Alisisitiza kuwa, Ofisi ya Waziri Mkuu haina sifa ya kuuwakilisha upande wa pili wa Muungano, maana hii ni Ofisi ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambayo Zanzibar ni sehemu yake.

Alisema kambi yao inasema haya ikijua wazi kwamba, kumekuwa na kisingizio kutoka upande wa Serikali ya Muungano, kwamba hakuna Serikali ya Tanganyika, hivyo, haiwezekani kwa Serikali ya Zanzibar kufanya mazungumzo na serikali isiyokuwepo.

“Kwa hivyo, kilichofanywa na Bunge la Tanganyika tarehe 25 Aprili 1964, siku moja kabla ya Muungano, ‘kuifuta’ Serikali ya Tanganyika kwa kutumia Sheria Na. 22 iliyoitwa ‘Union of Tanganyika and Zanzibar’, kilikuwa kinyume na makubaliano ya Muungano. Bahati mbaya, kitendo kile mpaka leo kimebakia kikiongeza shaka, kwamba Tanganyika ilijiingiza kwenye Serikali ya Muungano na kujifanya nchi mpya yenye jina jipya la Tanzania na yenye mipaka mipya ya kijiografia,” alisema.

“Tunasema haya tukijua uzito na uchungu wake. Ni vigumu kukiri kwamba tulifanya makosa, ikiwa kosa hilo linaonekana kuwa na maslahi. Lakini ukweli ni kuwa, kosa haliwezi kuwa na maslahi ya kudumu, hata kama linajaribiwa kufifilishwa kila mara. Kufuta Katiba ya Tanganyika kulikofanywa na vifungu vya sheria hii kulikuwa ni kosa.

“Kuifuta Serikali ya Tanganyika kulikuwa ni kosa. Na kosa hilo ndilo leo hii lililozaa kosa jengine la kiumbe kuzungumza na mmoja wa waumbaji kuhusiana na hatima ya kiumbe hicho. Na hivi ndivyo tunavyohoji uhalali wa vikao baina ya Ofisi ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano (ambayo inawakilisha kiumbe, Muungano) na Ofisi ya Waziri Kiongozi (ambayo inawakilisha Muumba, Zanzibar),” alisema msemaji huyo.

Alibainisha kuwa, kutekelezwa kwa azimio lile ndiko ambako kungetoa maana kwa vikao vinavyofanyika hivi sasa baina ya Ofisi za Waziri Mkuu na ile ya Waziri Kiongozi, lakini bila ya kuwapo kwa Serikali ya Tanganyika iliyo hai na inayotambulika, vikao hivi vya mazungumzo vinabakia kuwa vya mazungumzo tu na katiba inasema, matatizo ya Muungano yatatatuliwa kwa kupitia Mahakama ya Katiba na si vikao.

Msemaji huyo pia alizungumzia umuhimu wa kuitumia Mahakama ya Katiba, kumesababisha kushindwa kuanzishwa kwa Mfuko wa Pamoja wa Fedha wa Muungano, kuwa na chombo kinachoshughulikia michezo, mgawano wa mapato ya Muungano, kuondolewa kwa nafasi ya Rais wa Zanzibar kuwa Makamo wa Rais au mbadala wake na mambo mengine.

“Sisi wa kambi ya upinzani tumekuwa wazi sana katika hili. Hatutafuni maneno kusema kwamba tatizo kubwa na la msingi ni kutokuheshimiwa kwa mkataba wa Muungano, ambako kunatokana na ukosefu wa dhamira njema. Tulilisema hilo mwaka juzi, mwaka jana, na mwaka huu tunalirudia. Kwamba wa kujadiliwa ni Mkataba wa Muungano tu (Article of Union),” alisema msemaji huyo.

Aliongeza kuwa, mjadala wa kina juu ya mkataba wa Muungano ndiyo utakaothibitisha kuwa Serikali ya Tanganyika haikutakiwa kufa na kama imekufa iliuliwa kimakosa, na kosa hilo linaweza kurekebishwa kwa kutangazwa rasmi kuwapo kwa Serikali ya Tanganyika kama yalivyokuwa maamuzi ya Bunge hili tukufu mwaka 1992.

“Naliomba Bunge hili tukufu na Watanzania waniwie radhi kwa kusema kwamba, wakubwa wetu wameufanya Muungano huu ushabihiane sana na kile kisa cha Mfalme Jeta aliyemo kwenye riwaya ya Kusadikika ya Marehemu Sheikh Shaaban Robert. Mfalme huyu alikutwa na mjumbe wa Kusadikika akiwa amekaa katika eneo ambapo mto uliokuwa unakokozoa kila kitu – mawe, magogo, majengo, n.k. – unatiririkia kinywani na kuishia tumboni mwake, lakini kila mara alisikikana akilia: “Njaa! Njaa! Kiu! Kiu!

“Hivyo ndivyo Muungano wetu ulivyofanywa, kwamba uwe unakula na kunywa kila kitu na bado kila siku uwe unalalamika kufa njaa na kiu. Na ili kuufanya usife, wakubwa wanaamua kuulisha kila cha Zanzibar na kila cha Tanzania Bara.

“Ikiwa hali ni hii, je, si sawa kusema kwamba tunatoka kwenye serikali mbili zilizopo sasa kuelekea serikali moja? Je, jukumu la vikao hivi vya Ofisi za Waziri Mkuu na Waziri Kiongozi ni kuratibu na kusimamia mchakato wa kubadilisha muundo wa Muungano? Na je, hivyo ndivyo Wazanzibari na Watanganyika walivyotaka yawe matokeo ya vikao hivi vya kunywa chai na kahawa?” alihoji.

“Kambi ya upinzani iliweka bayana kuwa, kutokana na kupuuzwa na kudharauliwa kwa makusudi kwa matatizo ya Muungano huu, hakujawahi kupita muongo ambapo Muungano hautikiswi na kutikisika na kila unapotikisika, machoni mwa wakubwa huonekana kama kwamba unatikisika kwa kuwa hauna mambo ya kutosha.

“Hilo ni kosa kubwa katika sayansi ya utatuzi wa migogoro. Wahenga husema: ‘Ganga shina, matawi hayagangika!’ Kwa maana ya kuwa, kutibu maradhi ni kukitibu chanzo chake na sio dalili zake. Ni kosa kutokujiuliza kwa nini Muungano huu unatikisika na kujiuliza tu vipi unatikisika?” alihoji Riziki.

“Tumekuwa tukionesha mara zote kwamba chanzo cha matatizo ya Muungano huu ni kutokuheshimiwa kwa mkataba wake uliouunda. Tunarejea tena kusema hapa kwamba Muungano huu hauongozwi na Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977, bali unaongozwa na Mkataba wa Muungano wa mwaka 1964. Katiba ya Muungano na ile ya Zanzibar zinatakiwa zitafsiri tu yale yaliyomo kwenye mkataba na sio kuongeza wala kupunguza.

“Kwa hivyo, basi kama ni suluhisho, sisi wa kambi ya upinzani tunatoa jibu kama lile alilowahi kulitoa aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Ali Hassan Mwinyi, mwaka 1985, alipoulizwa ni kipi kipaumbele chake katika kuijenga Tanzania. Mzee Mwinyi alijibu: ‘Barabara!’ Alipoulizwa kipi chengine, akajibu: ‘Ni barabara!’, na alipoulizwa kipi chengine akasema: ‘Ni barabara!’

“Ikiwa Bunge lako hili tukufu litataka kujua ni kipi ambacho sisi wa kambi ya upinzani tunaamini kuwa ni suluhisho la matatizo yote ya Muungano huu, tutajibu kuwa ni ‘kurudi kwenye Mkataba wa Muungano!’ Tukiulizwa ni kipi chengine, tutasema ‘ni kurudi kwenye Mkataba wa Muungano!’ Na hata tukiulizwa mara ya tatu, tutasema ‘ni kurudi kwenye Mkataba wa Muungano!’” alisema.

Chanzo: http://freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=6331





Wabunge wachachamaa

30 06 2009

Imeandikwa na Halima Mlacha, Dodoma
30 Juni 2009

Suala la Muungano limeleta kizaazaa bungeni kwa baadhi ya wabunge wa CCM na wapinzani kutaka mkataba wa Muungano wa mwaka 1964 upitiwe na pande zote mbili husika na kuheshimika, kwa kuwa ndilo suluhisho pekee la kero zilizopo.

Aidha, wabunge wametaka serikali itambue na kurejesha Serikali ya Tanganyika ambayo ndiyo iliyohusika katika utiaji saini wa Muungano na hivyo kwa pamoja Serikali hiyo na ya Zanzibar ndio watakaokuwa na mamlaka ya kuujadili mkataba mzima na kuondoa kero zilizopo.

Kutokana na hilo, serikali imesema tayari imeanza kuchukua hatua za kutatua baadhi ya kero za Muungano, likiwamo suala la malalamiko ya wafanyabiashara wa Zanzibar ya kutozwa kodi mara mbili.

Akiwasilisha mapendekezo ya Kambi ya Upinzani bungeni jana juu ya makadirio na matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani bungeni na Mbunge wa Viti Maalum, Riziki Omar Juma (CUF), alisema Muungano haukuundwa na Katiba yoyote, bali mkataba, hivyo kero zote zitaondoka kwa mujibu wa mkataba huo.

“Sisi kambi ya Upinzani tukiulizwa suluhisho la Muungano ni nini, tutasema tena mara tatu, kuwa ni kurudi kwenye mkataba wa Muungano na wala si kitu kingine,” alisema Juma. Alisema jambo la msingi ni kuutafsiri mkataba huo na kuutekeleza ipasavyo, lakini pia kuuheshimu, ndipo itakuwa suluhisho na si vikao vinavyoendelea vya Makatibu Wakuu wa Serikali.

Alisema tatizo kubwa lililopo la Muungano linatokana na kutoheshimika kwa mkataba wake, kwa sababu katiba zote mbili zinaingilia kwa kiasi kikubwa makubaliano yaliyopo ndani ya mkataba huo na hivyo kwenda kinyume. Juma alisema kambi ya Upinzani inaona kuwa ni kosa kwa Ofisi ya Waziri Mkuu na Waziri Kiongozi ambao ni kama waasisi wa Muungano huo, kuujadili mustakabali wake.

“Ukweli ni kwamba Muungano ulifanyika na mkataba wake kusainiwa na mwakilishi wa Zanzibar, Rais Abeid Amaan Karume na wa Tanganyika, Mwalimu Julius Nyerere, hivyo kikao chochote hakina uhalali wa kuujadili mpaka kihusishe pande zote mbili,” alisema. Hata hivyo, Spika Samuel Sitta, mara baada ya hotuba, alimtaka msomaji kuzingatia kuwa mkataba wowote wa kimataifa ili ufanye kazi lazima utafsiriwe kwenye Katiba na Sheria.

Akichangia mjadala huo, Mbunge wa Chwaka, Yahya Kassim Issa (CCM), alisema Wazanzibari wameshindwa kuvumilia na wameamua kuzungumza kutokana na maudhi yanayotokana na Muungano ambayo hayawatendei haki.

“Mwalimu Nyerere aliwahi kusema mtu akikanyagwa akanyamaza wengine hawatajua, lakini akipiga kelele basi wote watajua kuwa ameumia na sisi tunaumia, ndiyo maana tunasema tunataka haki kwa Wazanzibari, mambo mengi ya Muungano hayaridhishi,” alisema.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Sheria na Katiba, Ramadhani Maneno (CCM), alisema kamati hiyo inapendekeza serikali ikamilishe kazi ya kugawana mapato na matumizi ya fedha za Muungano ambayo yanashugulikiwa na Tume ya Pamoja ya Fedha ya Tanzania.

Alisema pia uwekwe utaratibu ulio wazi na ulioandikwa baada ya makubaliano, kuhusu ushirikiano wa wizara na mambo mengine ambayo si ya Muungano, ikiwa ni pamoja na kurekebisha sheria za kibiashara ili kuwe na uwiano.

Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Dk Batilda Buriani, wakati akiwasilisha makadirio ya matumizi ya fedha kwa mwaka 2009/10, alisema katika hatua za kutatua kero za Muungano, masuala matatu yanaendelea kufanyiwa kazi, ambayo ni utaratibu wa kuchangia gharama na kugawana mapato yanayotokana na utafutaji na uchimbaji wa mafuta ya gesi asilia.

Alisema pamoja na hayo, tayari hatua zimeanza kuchukuliwa na Kamati ya Pamoja ya Serikali zote mbili kwa kushughulia malalamiko ya wafanyabiashara wa Zanzibar kuhusu kutozwa kodi mara mbili, hisa za SMZ zilizokuwa Bodi ya Sarafu ya Afrika Mashariki, faida ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na uwezo wa SMZ kukopa nje ya nchi.

Burian alisema pia kanuni za utekelezaji wa sheria ya mamlaka ya uvuvi katika ukanda wa bahari kuu iliyofanyiwa marekebisho na kupitishwa na Bunge Februari mwaka juzi, zimekamilika na kuthibitishwa na serikali zote mbili, kwa ajili ya utekelezaji na kwa sasa mamlaka ya kusimamia uvuvi wa bahari kuu ni moja.

Pia miradi mingine minane ya SMZ ambayo imeingizwa kwenye jumuiya ya Afrika Mashariki kwa ajili ya kuombewa ufadhili, inaendelea kufanyiwa kazi, alisema. Alisema miradi minne ya kikanda kati ya minane imepewa kipaumbele kwa ajili ya kuandaliwa andiko la mradi, usanifu na thamani ya gharama kwa ajili ya kuondoa fedha za utekelezaji.

Kuhusu kasoro za ajira kwa watumishi wa Zanzibar na kwa Taasisi za Muungano, alisema zinaendelea kufanyiwa kazi, na mapendekezo ya kuimarisha ajira katika taasisi hizo yalijadiliwa na makatibu wakuu wa pande mbili za Muungano na kuwasilishwa katika kikao cha Kamati ya Pamoja ya Serikali ya Tanzania na SMZ kushughulikia masuala ya Muungano Mei mwaka huu kwa ajili ya utekelezaji.

Chanzo: http://habarileo.co.tz/kitaifa/?n=2401





Wabunge CCM, CUF Zanzibar waungana, washambulia Muungano

30 06 2009

*Wadai Pinda, Nohodha hawana mamlaka kujadili kero
*Wataka mkataba wake sasa ujadiliwe bungeni
*Wahoji kufutwa Serikali ya Tanganyika
*Serikali yasema wenye Tanganyika walishakufa
*Spika Sitta amtimua John Cheyo bungeni

Na John Daniel, Dodoma

KATIKA hali isiyotarajiwa wabunge wote wa Zanzibar (wa Chama Cha Mapinduzi -CCM na Chama cha Wananchi-CUF),jana waliungana kuushambulia Muungano huku wakidai kuwa Waziri Mkuu Bw.Mizengo Pinda na Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar(SMZ) Bw. Shamsi Vuia Nahodha hawana mamlaka kujadili kero za Muungano huo.

Akichangia hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Makamu wa Rais iliyowasilishwa bungeni jana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Dkt. Batilda Burian, Mbunge wa Chwaka Bw. Yahya Kassim Issa (CCM), alisema Tanzania Bara inawanyonya na kuwarudisha nyuma Wazanzibar katika nyanja mbalimbai ikiwemo elimu na biashara.

“Wenzetu (Watanzania Bara) mnatuwekea vikwazo, bandari ya Zanzibar imekufa, watu walikuwa wanachukua vitu kwenda na kurudi lakini sasa hakuna, vikwazo wanavyowekewa ni matatizo, leteni vitu vya kiuchumi vitakavyosaidia Zanzibar ,hatutaki kusikia hadithi.

“Mafuta ni haki ya Zanzibar, sisi hatujaomba, sisi tulikuwa nchi kamili kama ilivyokuwa Tanzania Bara, mtu akikukanyaga ukanyamaza hatajua amekukanyaga, sisi Wazanzibari tunashindwa kujizuia kuhusu mambo ya Muungano,” alisema Bw. Issa na kusisitiza kuwa mwaka 2011 watakaporudi bungeni, hawataelewa mambo yakienda mrama.

Kwa upande wake msemaji wa Kambi ya Upinzani katika masuala ya Muungano Mbunge wa Viti Maalum Bi. Riziki Omar Juma, (CUF), alilitaka Bunge kuiagiza Serikali kuvunja haraka mazungunzo kati ya Waziri Mkuu, Bw. Pinda na Waziri Kiongozi Bw. Nahodha na kuwasilisha Mkataba wa Muungano bungeni ili ujadiliwe kwa lengo la kumaliza matatizo yaliyopo.

“Hatuoni kwamba vikao hivi vya pamoja (Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano na waziri Kiongozi wa SMZ ) vinakuja na suluhisho la tatizo la Muungano, vyenyewe ni sehemu ya tatizo, ili kutimiza wajibu wetu kama Bunge la watu lenye jukumu la kusimamia matumizi ya fedha za walipa kodi, liitake Serikali ya Muungano isitishe mara moja vikao hivi, badala yake Mkataba wa Muungano uletwe hapa bungeni kama nukta kuu ya mjadala, hapo ndipo tuanzie na tumalizie kero za Muungano.

“Ofisi ya Waziri Mkuu na Waziri Kiongozi hazina uwezo wa kujadili Muungano, hapa ni kizungumkuti kinachofanyika. Katika Mkataba wa Muungano, hakuna sehemu inayosema kufutwa kwa Serikali ya Tanganyika,”alisema Bi. Juma.

Alisema Kambi ya Upinzania inaona kazi inayofanywa sasa na Waziri Mkuu na Waziri Kiongozi kujadili Muungano, ni kama sehemu ya kuongeza kero kwa kuwa ajenda kuu wanayoina ni ukiukwaji wa Mkataba wa Muungano hivyo kero zinazojadiliwa ni matokeo ya tatizo na si tatizo lenyewe.

“Watanznzania waniwie radhi kusema kwamba wakubwa wetu wameufanya Muungano huu ushabihiane sana na kile kisa cha Mfalme Jeta aliyemo kwenye riwaya ya Kusadikika akiwa amekaa katika eneo ambapo mto uliokuwa unakokozoa kila kitu, mawe, magogo, majengo, unatiririka kinywani na kuishia tumboni, lakini mara alisikika akilia ‘njaa !njaa!’ kiu!kiu!”alisema Bi. Juma.

Alisema katika suala la Muungano hakuna mkubwa wala mdogo na kusisitiza kuwa nchi zilizoungana zilikuwa nchi kamili na suala la udongo halipaswi kuwepo na kuongeza kwamba Serikali ya Muungano ndio inayopaswa kubeba lawama kuhusu Muungano.

Alidai kuwa mazungumzo yanayofanywa kati ya Waziri Mkuu na Waziri Kiongozi ni sawa na watu wanaokutana kunywa kahawa au chai na si kufanya jambo la maana.

Naye Mbunge wa Mkanyageni, Bw. Mohamed Habib Mnyaa (CUF),alisema timu ya Waziri Mkuu na Waziri Kiongozi hazitoshi kujadili suala la Muungano kwani linawagusa Watanzania wengi hivyo lilipaswa kushirikisha nyanja mbalimbali.

Bw. Mnyaa alikwenda mbali zaidi na kutoa mfano wa swali la mwanawe kuhoji uhalali wa kiongozi mmoja (marehemu Mwalimu Julius Nyerere) kuonekana akichanganya udongo peke yake,jambo linalotia dosari kwenye misingi ya Muungano humo.

Bw.Mnyaa alisema tangu mwaka 1990 hadi 2000 zimeundwa tume 12 kushughulikia matatizo ya Muungano lakini hadi sasa hakuna muafaka uliopatikana.

Hivi karibuni Serikali iliweka wazi mambo matatu yaliyopatikana kupitia mazungumo kati Waziri Mkuu na Waziri Kiongozi kuwa ni pamoja na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Uvuvi katika bahari kuu na shughuli za biashara ya meli.

Katika Hotuba yake, Dkt. Burian alisema Serikali imepiga hatua katika mazungumzo kati ya viongozi hao wawili na kueleza kwamba vikao hivyo vitaendelea kwa kasi zaidi ili kuboresha Muungano.

Akijibu hoja hizo Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano) Bw.Muhammed Seif Khatib alisema suala la Serikali ya Tanganyika kwa sasa halina nafasi kwani wenye Tanganyika walishakufa.

Alisema wakati wa Muungano Tanzania ilikuwa na watu milioni 10 tu na sasa wapo zaidi ya milioni 40.

Alisisitiza kuwa Waziri Mkuu na Waziri kiongozi wana uhalali kujadili kero za Muungano kwani mwenyekiti suala hilo ni Makamu wa Rais.

Chanzo: http://majira.co.tz/index.php?option=com_content&view=article&id=828:-wabunge-ccm-cuf-zanzibar-waungana-washambulia-muungano-&catid=34:kitaifa-tanzania&Itemid=57