JANA Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, akijibu swali bungeni lililotaka kujua ni lini viongozi wa kiserikali kama rais wataacha kutumia ziara za kiserikali kufanya shughuli za kichama, kama alivyofanya Rais Jakaya Kikwete hivi karibuni huko Pemba, alisema rais ni mkubwa wake wa kazi na yeye asingeweza kutoa kauli ya kile kinachodaiwa kuwa alikisema, kwa sababu hakuwepo, na hajui ni nini rais alisema, zaidi ya kusoma tu kwenye vyombo vya habari.
Zaidi ya majibu hayo ya Pinda, Spika wa Bunge, Samuel Sitta, aliingilia kati kumsaidia waziri mkuu na kusema kwamba hakukuwa na haja ya swali hilo kujibiwa, kwani liko wazi.
Kwamba haiwezekani kutenganisha kofia mbili alizonazo rais, yaani ile ya urais na ile ya kuwa mwenyekiti wa chama chake, na kusisitiza kuwa hata katika nchi zilizoendelea sana kama Marekani, rais wao hutumia ndege ya serikali ‘Air Force One’ kufanya ziara ya kichama.
Kwanza, sisi tunasisitiza tena kuwa si sahihi kwa rais wala kiongozi yeyote wa serikali kutumia ziara za kiserikali ambazo kimsingi zimegharamiwa na kodi za Watanzania wote kutoa hotuba, kauli, kufanya shughuli au jambo lolote kwa masilahi ya chama chake cha siasa.
Si sahihi, kwa sababu mtu anapokuwa kiongozi wa kiserikali, wajibu wake ni kuwatumikia Watanzania wote bila kujali chama chake.
Pili, kiongozi wa kiserikali kufanya shughuli kwa masilahi ya chama chake cha siasa wakati akiwa kwenye ziara ya kiserikali, ni kuruhusu mgongano wa kimasilahi kati ya masilahi ya chama chake na masilahi ya taifa, ambayo ndiyo hasa anayopaswa kuyasimamia wakati huo akiwa kwenye ziara hizo za kiserikali.
Tatu, hatukubaliani na upotoshaji wa Spika Sitta kuwa haiwezekani kwa rais kutenganisha majukumu yake kama rais na kama mwenyekiti wa CCM, kwani sisi tunaamini kuwa inawezekana, kinachotakiwa ni kwa mhusika (Rais Kikwete) kuwa na utashi na utayari wa kutodharau misingi ya utawala bora wala kuwa mwepesi wa kubagua wafuasi wa vyama vingine vya siasa pindi awapo kwenye ziara za kiserikali.
Nne, Rais Kikwete anapaswa kupanga muda wa kufanya ziara za kichama ambao utakuwa ni tofauti na ule wa ziara za kiserikali, na anapaswa kutumia ruzuku ya CCM kwa ziara za kichama, badala ya kudoea usafiri wa kiserikali halafu anakwenda kuzungumzia mambo ya CCM kama alivyofanya Pemba hivi karibuni.
Akiona ni vigumu, basi aache ziara zake za kichama zifanywe na Makamu Mwenyekiti wake, Pius Msekwa, au Katibu Mkuu wake, Yusufu Makamba, pale inapolazimu.
Tano, kauli ya Pinda kuwa hawezi kutoa kauli kuhusu kile alichokisema Rais Kikwete, eti kwa sababu ni mkuu wake wa kazi, ni ya upotoshaji.
Pinda kwa nafasi yake kama Waziri Mkuu, ndiye mtu wa mwisho anayepaswa kujibu au kutoa ufafanuzi wa jambo lolote linalohusu serikali na maadili ya viongozi wake, akiwemo rais.
Kwa nini Pinda anasema hakuwepo na hajui alichokisema rais? Kama vyombo vya habari viliandika uongo kuhusu kile alichokisema Kikwete kule Pemba, serikali iliyo chini ya Pinda kama Waziri Mkuu, ilishindwa vipi kutoa taarifa ya kukanusha kile kilichoripotiwa kupitia mwandishi wake, Salva Rweyemamu?
Kwa nini Pinda anaviamini tu vyombo vya habari pale vinaporipoti mambo mazuri ya viongozi lakini haviamini pale vinaporipoti kauli zisizofaa za rais?
Tunautaka umma wa Watanzania uelewe kuwa majibu yaliyotolewa bungeni na viongozi hawa ni ya upotoshaji, ni wajibu wa kila mwananchi kutochoka kuwarudisha kwenye mstari viongozi wetu pale wanapofanya ndivyo sivyo.
Chanzo: http://freemedia.co.tz
Maoni