Lipumba: Mkapa hana kinga

31 12 2008

Na Asha Bani, Masasi

Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, amesema Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, hana kinga, hivyo anastahili kushtakiwa kwa mujibu wa katiba ya nchi.

Alisema hayo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari walioko kwenye msafara wa ziara ya kukagua uhai wa chama chake mjini Masasi.

Profesa Lipumba alisema kutokana na kifungu namba 46(3) cha katiba ya nchi, Mkapa anastahili kushtakiwa kama ushahidi wa kosa litabainika.

Alisema maovu mengi yalifanyika wakati wa utawala wake, hivyo kuna haja ya kuangalia kwa makini na kufanya uchunguzi endapo itagundulika kuna mkomo wake katika kuliingizia taifa hasara kutokana na mikataba mibovu; na ubinafsishaji usiofuata taratibu, anastahili kushtakiwa.

Alisema kifungu hicho cha sheria kinasema kinga ya rais ni pale ambapo amefanya jambo lililofuata taratibu za nchi.

“Kwa mfano, kama sehemu ina fujo, halafu Rais ameamuru jeshi kwenda kutuliza na kuua, hapo rais hatashtakiwa, lakini si kuipa nchi hasara, kuliingiza taifa kwenye umaskini kwa kushiriki kwenye makosa ya ufisadi na rushwa inabidi ashtakiwe!

“Rais hayuko juu ya sheria na kinga yake ni sheria, hivyo naye achunguzwe endapo itabainika kama alihusika kwenye rushwa katika ununuzi wa rada ambao umeliingizia taifa hasara ya sh bilioni 40, basi hana budi kushtakiwa,” alisema.

Profesa Lipumba alisema hakuna haja ya kuumiza kichwa kwani katika utawala wa Mkapa wizi wa fedha kwenye Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), ulifanyika kwa kuchota mabilioni ya fedha na kutafunwa na wachache.

Katika hatua nyingine, chama hicho kimesema Mkapa haheshimu haki za binadamu kama ilivyodaiwa na Askofu wa Kanisa la Anglikan, John Ramadhan, katika ujumbe wake wakati wa mkesha wa ibada ya Sikukuu ya Krismasi iliyofanyika katika Kanisa la Mkunazini, mjini Zanzibar.

Taarifa iliyotolewa na Naibu Mkurugenzi wa Haki za Binaadamu na Mawasiliano ya Umma, Salim Bimani jana, ilisema kumbukumbu za utawala wa Rais Mkapa zinaonyesha kulitokea mauaji ya kutisha yaliofanywa na vikosi vya ulinzi na usalama dhidi ya raia wasiokuwa na hatia visiwani Zanzibar.

“Wakati mauaji hayo yanafanyika si tu Rais Mkapa alikuwa ndio Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, bali pia alithubutu kuwapandisha vyeo askari waliohusika na mauaji hayo,” alisema Biman.

Alisema CUF haikubaliani na kauli ya askofu huyo kuwa Mkapa alikuwa kiongozi aliyeheshimu utu wa mtu wa kuishi kwa vile hakupitisha adhabu hata moja ya kifo katika utawala wake licha ya watu kadhaa kupatikana na hatia na kuhukumiwa kifo.
Alisema kwamba wananchi wa Zanzibar kila Januari 26 na 27 wamekuwa wakiadhimisha kumbukumbu ya mauaji ya kutisha yaliofanywa na vikosi vya ulinzi na usalama chini ya amiri Jeshi Mkuu Benjamin Mkapa.

Akitoa mahubiri katika ibada ya mkesha wa sikukuu ya Krismasi katika Kanisa la Anglikana Mjini Zanzibar, Askofu alisema Rais Mstaafu, Mkapa, katika uongozi wake atakumbukwa kwa kuheshimu haki ya mtu ya kuishi kwa vile hakuidhinisha adhabu ya kifo licha ya watu kadhaa kupatikana na hatia wakati wa uongozi wake.





CCM walalamikia maofisa ZEC

31 12 2008

Na Mwanne Mashugu, Zanzibar

Chama cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimesema baadhi ya makamishna wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) na watendaji wameanza kupotosha sheria ya uchaguzi kwa maslahi yao.

Hayo yalielezwa na Katibu Mwenezi wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai, alipozungumza na waandishi wa habari katika Ofisi ya CCM, Kisiwandui, Zanzibar.

Alisema makamishna hao wamekuwa wakipotosha sheria ya ukaazi kuwa mtu anaweza kujiandikisha hata bila ya kuwa na sifa ya Uzanzibari ukaazi katika eneo husika.
Alisema sheria ya ukaazi katika majimbo lazima izingatie kitambulisho cha Mzanzibari mkaazi kwa sababu ni kielelezo cha Mzanzibari mwenye sifa ya kushiriki uchaguzi wa Zanzibar.

Vuai alisema CCM itaingia katika zoezi la uandikishaji wapiga kura katika daftari la kudumu kwa kuona katiba na sheria za uchaguzi zinafuatwa.

”Hatupo tayari kuona baadhi ya makamishna na watendaji wakitaka kupindisha sheria kwa maslahi yao,” alisema na kusisitiza sheria ya ukaazi katika majimbo inaheshimiwa.
Alisema tayari CCM imeanza kupokea malalamiko kutoka kwa wanachama wao kuwa baadhi ya makamishna wameanza kupotosha sheria za mpiga kura anazopaswa kuwa nazo kabla ya kuandikishwa katika jimbo husika.

Hata hivyo, aliwataka wanachama wao kujitokeza kwa wingi katika zoezi la uandikishaji wapiga kura lililopangwa kuanza Januari mwakani.
Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ina makamishna saba, wawili kati ya hao wanatoka chama cha Wananchi (CUF).

Aidha, alitanabahisha CUF hakina hati miliki za majimbo ya Pemba kwa hivyo kila chama kina haki ya kufanya kampeni ya kushinda viti Pemba.

Alisema kwa mujibu wa tathmini iliyofanywa na CCM, mabadiliko ya kisiasa hayakwepeki kisiwani Pemba kwa kuwa mambo yaliyokuwa kero kubwa kwa wananchi yametafutiwa ufumbuzi.

Alizitaja baadhi ya kero kuwa ni usambazaji wa umeme vijijini, mradi wa maji vijijini na uhifadhi wa mazingira, miundo mbinu ya barabara na kuunganisha umeme katika gridi ya taifa kutoka Tanga hadi Pemba.

Alisema CCM imesikitishwa na watu wanaopotosha historia ya Zanzibar na kuwataka kuacha mara moja tabia hiyo kwa vile mapinduzi ya Januari 12, mwaka 1964, ndiyo yaliyowakomboa Wazanzibari.

Alisema kusheherekea uhuru wa Desemba 10, mwaka 1963 ni sawa na kupoteza muda kwa sababu ulikuwa hauna faida yoyote kwa taifa.

Alisema Mapinduzi ya Zanzibar ndiyo yaliyomkomboa mnyonge kwa kupata elimu na kumiliki ardhi.

Hivi karibuni, Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Shariff Hamad alidai kuwa CCM kwa kushirikiana na vikosi vya ulinzi na usalama vimeandaa njama ya kuchafua zoezi la uandikishaji wapiga kura kwa lengo la kuisaidia CCM kushinda viti sita Pemba.

Hata hivyo, Waziri wa Nchi Afisi ya Waziri Kiongozi, Hamza Hassan Juma alipinga madai yaliyotolewa na Hamad kwa kusema “Hamad anaota ndoto za mchana na homa ya uchaguzi imempanda mapema





Mauaji ya 2001: Muafaka wa Kisiasa wa Oktoba, 2001

17 12 2008

SURA YA NANE

MUAFAKA WA KISIASA WA OKTOBA 10, 2001

Baada ya mauaji na unyanyasaji kama tuliouelezea kusita kidogo, Watanzania tulijkaa na kutafakari nini faida tulioipata katika purukushani ambazo baada ziligeuka madimbwi ya damu.  Aidha tulitafakari nini la kufanya baada ya pale.  Pamoja na kwamba muafaka wa kwanza wa tisa tisa, tisini na tisa ulivia, bado tuliona dawa ni ile ile iliyokataliwa na wenzetu mara ile ya kwanza.  Sasa ukaja muafaka wa pili wa kumi kumi, elfu mbili na moja ambao madhumuni yake ni kama ya ule wa kwanza uliokataliwa.  Baada ya matukio haya, Rais Mkapa alitanabahi kwamba byombo bya dola haviendeshi na kwamba kinachohitajika ni umoja wa watu.  Kwa hivyo, alimuagiza Katib Mkuu wake aanze kukaa na wenziwe.  Kwanza iliundwa kamati ya Makatibu Wakuu wa vyama vya CUF na CCM ili kupita Zanzibar nzima kujaribu kurejesha imani na utulivu kwa watu kwa mintarafu ya kuurejesha umoja uliokwisha vunjika.  Baada ya hapo Tume ya Muafaka ikaasisiwa tena kufuatia kutiwa sahihi kwa Muafaka huo wa pili.  Muafaka ulitanguliza vipengele ya kutekelezwa ili chaguzi zijazo ziwe huru, haki na kusitokee tena migogoro na mauaji.  Muafaka haukusema kuwa historia yetu ndio msingi wa matatizo yetu kwani kufanya hivyo kungetufanya tusiwe na jengine la kufanya.  Kwa hivyo, kwa mara nyengine tena, ilionekana kuwa historia si tatizo bali kubwa ni chaguzi.  Nini kilikusudiwa katika muafaka na utekelezaji umefika wapi ndio maelezo ya sura hii.

Sehemu 1: Nama Mwafaka ulivyokuja

8.1.1    Usuli wa Muafaka

Muafaka wa kisiasa kati ya CUF na CCM ni hatua iliyofuata baada ya vyombo vya dola kufanya mauaji kutokana na madai ya haki ya kuwa na nchi yenye kufuata demokrasia ya kweli.  Hivyo, twaweza kusema muafaka tuliuleta kwa damu, baada ya kipindi chote cha miaka mitano ya mwanzo kuutaka kwa amani bila mafanikio.  Walituuwa katika maandamano ya amani kwa kudai ya kurejewa kwa uchaguzi pamoja na madai ya kusitisha unyanyasaji uliokithiri baada ya kuvurugwa kwa uchaguzi wa 2000.  haikuwa lazima kuuteketeza umma kwanza ili kuwe na maelewano na umoja wa Zanzibar, lakini watu ndio wameshauliwa.  Watanzania wamejifunza kwamba Serikali za CCM hazileti ufumbuzi wa matatizo kwa hiari hadi maafa yatokee na yawe makubwa.  Huu nii udhaifu mkubwa ambao hatukuuona (tulipotukichambua historia yetu)  jinsi yake hata katika hizo zama zinazolaaniwa kuwa zilikuwa za mateso, dhulma na unyanyasaji.

Ingawa kitendo cha mauaji kilikuwa ni tukio baya la kuhudhunisha, lakini lilifahamisha CCM katika nchi ambayo ni yetu sote.  Damu ilibidi imwaggike kutokana na ukaidi na ubabe wa Serikali unaochonga ukatili wa vyombo vya dola.  Haikuwa hiari kufa lakini ndio CCM imewafikisha Watanzania hapo.  Kadri viongozi walioleta uhuru waking’atuka madarakani, wale waliorithi mamlaka wanazidi kuitia nchi katika misukosuko inayoipotezea dira na sifa njema Tanzania.  Kwa kweli ingawa si mwahala mwingi haki ilisimama bila ya mikiki na mara nyingine hata kumwaga damu, lakini hili si jambo la lazima kama Taifa litaongozwa kwa misingi ya haki na usawa badala ya chuki na hasama kama ilivyo Tanzania ya leo.  Tunamkumbuka Mwenyekiti wetu katika mwaka 1996 hapo uwanja wa Tibirinzi Pemba aliposema haki haitakuja kama halua kisahanini.  Ni kweli tuliimba sana haki sawa, lakini tulipuuzwa na wenzetu hadi nchi ilipoingia katika vurumai na migogoro.  Heshima yetu Watanzania ya kuwa wasuluhishi wa matatizo ya wenzetu imepotezwa kabisa na viongozi wa leo wa CCM.  Burundi na Rwanda waifahamu vipi Serikali ya Tanzania ikiwa wao wasuluhishi ndio kwanza wanamwaga damu kwa raia wao!

Tulikaa miaka minne kuyaangalia maneno ya Profesa iwapo yalikuwa na kweli ndani yake.  Baada ya uchaguzi wa mara ya pili, tulifahamu kwamba CCM hawakuwa na nia ya mfumo wa mageuzi, isipokuwa walikubali ili kupata fedha na huruma za wafadhili tu.  Hatukungoja kukumbushwa tena maneno ya Mwenyekiti.  Tulijitolea muhanga sio kufa, bali kupambana na vitisho vya ukandamizaji, pamoja na kudai haki si kwa vita bali kwa sauti ya juu ili uporaji wa haki yetu umalizike kabisa kwa siku zijazo.  Tulikubali mazungumzo kwani ndio sera yetu ya „amani ya kweli“ ambayo haiji ila kwa kukaa na kuzungumzia matatizo yetu kw apamoja.  Rais Mkapa ambae alikuwa na sera alizozitangaza kwamba hatakutana na washenzi, sasa akamuagiza Katibu Mkuu wa CCM, Ndugu Philip Mangula akutane na Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif ili waanzishe mazungumzo.  Tunakumbuka kikao cha kwanza kilifanyika miezi mitatu baadae huko jijini Dar es Salaam kwenye hoteli ya Sea Cliff.  Kikao kilimalizika kwa kutoka na tamko la pamoja kwamba sasa ni kweli kumekuwepo mgogoro wa kisiasa tokea kuharibika kwa uchaguzi wa 1995 na kuzidishwa na kufeli kwa utekelezaji wa muafaka kwa kwanza wa 1999.  kitu kimoja tukitaje kwa sauti maalum.  Nacho ni; ingawa uchaguzi wa kwanza uliharibiwa na muafaka ulikuja kuvia, lakini roho za watu hazikupotea.  Hili la baada ya uchaguzi wa 2000 ni kubwa zaidi katika kumbukumbu zetu na hatusahau, kwani tukifanya hivyo linaweza kurudia tena.

Kwa hivyo, tunaungana kwamba hali hii ya mgogoro wa kisiasa ya kuanzia mara baada ya uchaguzi wa kwanza ilipelekea kuchafuliwa kwa uchaguzi mkuu wa 2000 na baadae kuishia katika maandamano yaliyopelekea kuuliwa kwa wananchi wasio hatia na kulitia Taifa letu katika aibu kubwa.  Kwa hivyo, vyama vyetu vimeingia katika mazungumzo kwa nia njema ya kumaliza mgogoro wenyewe.  ikaelezwa kwamba ajenda kuu za muafaka zitakuwa katika maeneo manne makuu.  Ingawa sisi tulipoteza dai kubwa la kurudia uchaguzi 2000, tulikubali wenzetu walivyotaka kwani „iliyopita si kondo“ na hasa tulijuwa kuwa muafaka ni swa na „nipe nikupe“.  Kwa hivyo maeneo manne ya muafaka ni kama haya yafuatayo:

?          Utekelezaji wa muafaka wa Juni 9, 1999

?          Uchaguzi mkuu wa Zanzibar wa mwaka 2000

?          Matukio ya mauaji ya tarehe 26 na 27 Januari, 2001

?          Watanzania waliokimbilia Kenya.

Kitu kimoja tu walisahau kwamba Zanzibar haikuwa na uchaguzi mkuu mwaka 2000,, tofauti na miaka yote ya nyuma.  Mwaka huu sheria zilivurugwa na kufanya uchaguzi Tanzania nzima kuwa siku moja ili kumpa nafasi Mkapa kutumia namna apendavyo, vyombo vya dola kuudhibiti uchaguzi wa Zanzibar.  Hivyo, bila kujali ugumu wa kupiga kura waliwafanya Wazanzibari wapige kura 5 wakati mmoja, wakati Bara wao walipiga kura 3.  Uchaguzi ulifanyika chini ya udhibiti na ukandamizaji mkali wa vyombo vya dola.  Hii ya kuchanganya chaguzi ilikusudiwa kuwa mwanzo wa jaribio la kuwa na uchaguzi mmoja tu Tanzania kwa siku zijazo ili kuimaliza Zanzibar kisiasa.  Bila shaka kurudiwa uchaguzi maana yake ingerejesha uchaguzi mkuu Zanzibar ambao ulishapigwa kumbo.  Hili lilikataliwa lakini Muafaka ulipatikana.

8.1.2    Kamati ya Mazungumzo

Ilikuwa vigumu kwa wananchi hasa wanachama wa CUF kuamini kwamba, CCM ingeweza kutekeleza ahadi kwa vile ilishavunja kila kipengele cha muafaka wa mwaka 1999.  kwanza iliundwa kamati ya mazungumzo iliyokuwa na wajumbe sita kutoka kila chama, wakiwemo Makatibu Wakuu wa kila chama.  Kwa CUF, waliowakilisha kwenye kamati ni Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad, pamoja na Wajumbe wa Kitaifa ambao ni: Waheshimiwa Ali Haji Pandu, Ismail Jussa, hamad Rashid Moh’d, Shaibu Akwilombe na Mheshimiwa Abubakar Khamis Bakary.  Kwa upande wa CCM, wajumbe wa Kamati walikuwa na Katibu Mkuu Mhe. Philip Mangula pamoja na Waheshimiwa Kingunge Ngombale Mwiru, Omar Ramadhan Mapuri, Salum Juma Othman, Moh’d Aboud Moh’d na Dr. Masumbuko Lamwai.

Kazi kubwa ya Kamati hii ilikuwa ni kuchambua kwa undani na kwa umasikini zaidi katika kila eneo la kutekelezwa mambo ya msingi ya kurejesha umoja wetu na kuweka misingi bora ya kidemokrasia kwa siku za baadae.  Katika kila eneo kati ya hayo manne tuliyoyazungumza, kamati ilifanya uchambuzi zaidi wa vipengele vya msingi.  Haikuwa rahisi kufikia maamuzi ya mambo hayo ambayo kwayo ndio yaliyotarajiwa kufanya ajenda za kutambulika rasmi kwa mgogoro wenyewe.  Mara nyengine ilifikia hadi Kamati kutaka kuvunjika kwa ugumu wa madai ya kila upande.  Mara kwa mara mori wa wanachama wa kila upande ulikuja juu kwa kusikia tu kwamba ama upande mmoja umepata zaidi kuliko mwengine, au upande mmoja hautaki kutoa kitu.  Hata hivyo, mwishowe lilipatikana jambo lililotafutwa la vipengele vya utekelezaji wa muafaka.  Tunaishukuru Kamati hiyo kwa kazi kubwa ya kufanikisha mazungumzo ambayo ndio msingi wa umoja wetu.

Picha No. 8 chini: Wajumbe wa Kamati ya Mazungumzo.  Waliosimama kutoka kushoto ni Waheshimiwa Ismail Jussa, Omar Mapuri, Hamad Rashid, Salum J. Othman, Shaib Akwilombe, Abubakar Khamis,  Dr. Lamwai na Mohd Aboud.  Walioketi kutoka kushoto ni Mzee Kingunge, Maalim Seif, Rais Amani Karume, Mhe. Mangula na Jaji Ali Haji Pandu.

Sehemu 2: kutambuliwa Rasmi kwa Mgogoro

8.2.1    Mambo yaliyokubaliwa

Baada ya Kamati ya Makatibu Wakuuk ya kuratibu mazungumzo kukutana kwa majuma kadhaa, mwishowe walikubaliana na agenda za mazungumzo ambazo baadae ndio zilizofanya kiini cha makubaliano yaliyoundiwa Tume ya Rais ya Uratibu wa utekelezaji wa muafaka.  Muafaka wa kisiasa baina ya CUF na CCM unaanza kwa kutambua kuwepo kwa mgogoro wa kisiasa.  Vyama hivyo vilikubaliana kimsingi kwambo:

?          Kumekuwepo kwa Mgogoro wa kisiasa hapa nchini ambao chimbuko lake ni Uchaguzi Mkuu wa 1995na kuendele katika Uchaguzi wa 2000 hadi kufikia matukio ya tarehe 26 na 27 Januari, 2001 yaliyosababisha watu kadhaa kupoteza maisha yao na wengine kujeruhiwa.

?          Vyama vyetu vinakubaliana kuwa matukio hayo yameliletea Taifa letu aibu kubwa.

?          Nia na madhumuni ya vyama vyetu viwili ni kuutatua mgogoro huo kwa njia ya majadiliano na mazungumzo.

?          Vyama vyote vimeingia katika mazungumzo haya kwa nia njema ya kuondosha uhasama, chuki na kutiliana shaka kati ya wana CCM na wana CUF nchini na kujenga mazingira mazuri ya ushindani wa kisiasa na kuaminiana.

?          Vyama vyetu viwili vimejifunza kwamba kuna haja ya kutekeleza makubaliano yanayofikiwa kwani kinyume cha hayo ni wananchi kupoteza imani imani na njia ya mazungumzo kama ndio njia sahihi ya kutatua migogoro katika jamii.

?          Lengo na madhumuni makubwa ya kufikia muafaka huu ni kusahau yaliyopita na kutekeleza kwa makusudi kabisa, makubaliano yetu ili kujenga demokrasia ya kweli na kwa hivyo kuleta maendeleo ya kiuchumi na ustawi wa jamii katika nchi yetu.

?          Katika kufikia makubaliano yenye lengo la kuupata ufumbuzi wa kudumu wa mgogoro wa kisiasa ulioikumba nchi yetu, vyama vyetu viwili vitaongozwa na maslahi ya taifa ambayo yatazingatia Umoja wa Kitaifa, Amani na Utulivu kwa wananchi. Maendeleo ya Wananchi katika Uhuru na Demokrasia na Utawala wa Sheria na Haki.

?          CCM na CUF wanautambua na kuuthamini mchango wa TAMKO LA PAMOJA LA MACHI 2001 katika kuandaa mazingira yaliyowezesha dira ya mazungumzo yaliyotufikisha kwenye Muafaka huu.

?          Ajenda kuu katika mazungumzo yetu ni kama zilivyokubaliwa na Makatibu Wakuu wa vyama hivyo katika kikao chao cha tarehe 17 Machi, 2001.  Ajenda hizo ni:

1          Utekelezaji wa Muafaka wa CCM na CUF wa Juni 9, 1999

2          Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa mwaka 2000

3          Matukio ya tarehe 26 na 27 Januari, 2001

4          Watanzania waliokimbilia Kenya

Kwa hivyo, kufuatia kutambulika kwa mgogoro katika hali hiyo, hatua za utekelezaji wa muafaka zilianzia kwa utekelezaji wa muafaka wa Juni 9. 1999 ambao kwa muhtasari ulihusu mambo yafuatayo:

?          Kuifanyia marekebisho Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ili kuifanya iwe huru na ikubaliane na sura ya Tume katika nchi za Jumuiya ya Madola.

?          Kuanzishwa kwa Daftari la Kudumu la Wapiga kura.

?          Kufanyiwa mapitio, katiba ya Zanzibar na Sheria za Uchaguzi ili zilingane na matakwa ya mfumo wa vyama vingi.

?          Kurekebisha vyombo vya habari vya Serikali ili virpukane na upendeleo wa kiukereketwa.

?          Kuhakikisha kwamba vyama vya siasa vinafanya shughuli zake bila ya kubughudhiwa na vyombo vya dola.

?          Kufanya marekebisho kwa mahakama za Zanzibar ili kutoa haki kwa uhuru zaidi na kukuza heshima zake mbele ya jamii.

?          Kuhakikiwa kwa madai ya wafanyakazi na wanafunzi waliofukuzwa na wale waliovunjiwa majumba au kuathirika kwa namna nyengine.

?          Viongozi wa zamani wa kisiasa katika Serikali kupewa heshima na haki sawa baada ya kustaafu.

?          Vyama vya siasa kuheshimu katiba na sheria za nchi na kuepuka kutumia lugha zinazochochea chuki baina ya vyama vya siasa, ukabila, uhasama na kutovumiliana.

Sehemu 3: utekelezaji wa Muafala

8.3.1    Mwanzo Mgumu au Mbaya?

Hadi tunapoandika kijitabu hiki sasa ni karibu miezi 18 tokea muafaka utiwe saini.  Kuna mambo mengi ambayo yametekelezwa kama ilivyokubaliwa, hata hivyo yale machache ambayo hayajatekelezwa bado yanaturejesha kwenye ile hali ya kutiliana shaka iliyotajwa katika muafaka.  Muafaka hautahesabiwa kwamba umetekelezwa kwa kuacha kipengele chochote katika muafaka, maana si tabia ya makubaliano kutekelezwa nusu nusu, wala si tabia ya makubaliano kucheleweshwa kutekelezwa.  Wasi wasi mkubwa utakaoikumba jamii na kurejesha yaliopita ni kutotiliana maanani wakati na ukamilifu katika utekelezaji.

Katika kuhakikisha kwamba muafaka unatekelezwa kwa wakati uliopangwa.  Tume ta Rais ya utekelezaji Muafaka yenye wajumbe watano watano kutoka kila chama (CUF na CCM) iliundwa.  Wenyeviti wenza wa Tume hiyo ni Mhe. Abubakar Khamis kutoka CUF na Mhe. Omar Ramadhan Mapuri kutoka CCM.  Utekelezaji ulikumbwa na matatizo kutokea siku ya kwanza ya utekelezaji, kutokana na ukweli kwamba sheria zilizokuwa zinajadiliwa ili kuunda Tume hiyo kihalali zilikua zinajadiliwa na chama cha CCM tu.  Hii ni kutokana na kwamba Wawakilishi wa CUF walifukuzwa na kutokuwepo katika mijadala ya Baraza.  Kulikuwa na upinzani mkubwa kati ya Wajumbe wa CCM.  Kulikuwa na wengine ambao walionesha dhahiri kutopendelea kuwa na maridhiano na mashirikiano na upinzani, ingawa bado sera za chama kwa muda wote imebakia ile ile ya „amani, utulivu na mshikamano“.  Hali hii iliwashangaza wengi sio tu Tanzania lakini hata katika dunia.  Jambo pekee ambalo lilitekelezwa mara moja ni kuwaachia watuhumiwa wa kesi ya uhaini, jambo ambalo lilikuwa ndani ya uwezo wa Rais.

Kwa hali hiyo, ratiba ya utekelezaji ambayo ilitakiwa kukamilika katika miezi 18, ilicheleweshwa kutokana na tabia ya baadhi ya wanasiasa hao walioshindwa mata moja kuona umuhimu wa umoja wa Wazanzibari katika maendeleo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi.  Jambo hili lilitafsirika kwamba nia njema miongoni mwa wana CCM ilikuwa  ikikosekana.  Katika uundwaji wa Tume ya Utekelezaji, tiakumbukwa kwamba, kabla ya kujadiliwa katika Baraza, Mswad uliotayarishwa na Tume hiyo kufanyiwa marekebisho na Kamati ya Katiba ya Katiba na Sheria ya Baraza la Wawakilishi bila hata ya kukihusisha chama cha CUF0.  CCM iliwakilishwa moja kwa moja kwani Wajumbe wote waliohusika na marekebisho ni viongozi wakuu wa CCM.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti Mwenza wa Tume Mhe. Abubakar Khamis, ni Juhudi za Rais wa Jamhuri Benjamin Mkapa na Rais wa Zanzibar Amani Karume, ndio baadae walitumia madaraka yao ya kikatiba na kuufanya Mswada uridhiwe na Wajumbe.  Hata hivyo, baada ya dosari hizi, Tume uliundwa na yako mambo mengi yametekelezwa ingawa hayo machache yaliokuwa hayajatekelezwa si ya kudharau.  Hata hivyo, pamoja na kusitasita huko kwa Wajumbe wa CCM, baadae walipitisha marekebisho ya Katiba na Sheria yaliyohitajika na kuuweka muafaka pahala pake pa kuutekeleza.  CUF – Chama cha Wananchi kinatoa pongezi maalum kwa wajumbe hao wa CCM.

8.3.2    Mambo yaliyokwisha tekelezwa

a)         Ilikubaliwa kufanyiwa marekebisho Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) ili chaguzi zote zinazofuata ziwe wazi, zinazoheshimika na bila utata.  Kwa hivyo, ili Tume iwajibike na iweze kutenda haki, ilitakiwa kuwa huru (isiingiliwe na Serikali) na muundo wake ukubaliane na muundo wa Tume za uchaguzi katika nchi za Jumuiya ya Madola.  Tume hiyo sasa imekwisha undwa na ina wajumbe, wawili kati yao wakitoka katika chama cha CUF.

b)         Ili kuondoa udanganyifu katika uandikishaji wapiga kura unaotokana na kuandikisha watu wasiostahili na kuwaacha wanaostahili, ilikubaliwa kwamba sasa kuwe na Daftari la Kudumu la Wapiga kura.  Hadi tunaingia katika chaguzi ndogo za majimbo 17 ya Pemba, Daftari hilo bado halijaanzishwa.

c)         Ilikubaliwa kuzifanyia mapitio Katiba ya Zanzibar na Sheria za Uchaguzi za Zanzibar ili zikubaliane na matakwa ya demokrasi ya vyama vingi.  Katiba na Sheria hizo sasa zimekwisharekebishwa.

d)         Kamati ilikubaliana kwamba ili kuondosha upendeleo wa vyama katika kutangaza shughuli za siasa, vyombo vya Habari vya Serikali vitalitakiwa kufanyiwa marekebisho.  Hili halijafanywa, na ndio mwanzo Sauti ya Tanzania Zanzibar na TVZ vinatoa upendeleo kwa CCM na hawana habari na Muafaka.

e)         Kulikuwa na makubaliano kwamba kila chama kiwe huru kufanya shughuli zake bila kuingiliwa na vyombo vya dola.  Upo unafuu katika hili, ingawa bado kuna hitilafu katika ukamilifu wake.  Mfano mkubwa wa dosari hii ni ule ulioanza kuoneshwa na Kikosi cha Volantia wakati walipomzuia Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif katika ziara zake za kuimarisha chama katika Jimbo la Donge, mwezi wa Machi, 2002.

f)          Ilikubaliwa kurekebisha muundo wa utendaji wa Mahkama ili ziwe huru na zifuate maadili ya kazi pamoja na kurejesha heshima yake iliyopotezwa kwa kuingiliwa kutoa maamuzi yasio ya haki.  Hili limeanza kutekelezwa na hatua ya utekelezaji inaonesha dalili za mafanikio.

g)         Ilikubaliwa kwamba Serikali ifanye uchunguzi juu ya madai ya wanafunzi waliofukuzwa vyuoni na maskuli kwa kutaka kutumia haki yao ya kidemokrasia ya kupiga kura.  Sambamba na hili, madai ya kufukuzwa kazi watu waliodhaniwa kuwa ni wapinzani pamoja na wale waliovunjiwa nyumba zao na serikali mwaka 1996 (sehemu za Mtoni) bila fidia yachunguzwe.  Uchunguzi umefanywa na Tume ya Rais ya Uchunguzi, na inasemekana kazi hizo zimekamilika.  Hata hivyo wananchi hawajapewa matokeo yake na kwa hivyo hakuna hatua nyengine zaidi ya uchunguzi.

h)         Ilikubaliwa kwamba viongozi wa zamani wa kisiasa na katika serikali wapate haki za mafao yao na kupata heshima kama wanavyopewa watu wengine, bila ubaguzi wa itikadi ya vyama.  Serikali imeonesha dalili za kutekeleza hili ambalo kwa uhalisi wake ni suala la serikali na viongozi wahusika.  Suala hili lilionekana kama limemlenga Katibu Mkuu wa CUF Maalif Seif Sharif ambae alikuwa Waziri Kiongozi aliestaafu bila ya kulipwa haki zozote.  Hii ni fikra potofu.  Hata Rais Chiluba wa Zambia aliwaji kumfanyia kashfa Rais aliemrithi Kaunda.  Hakufikiri kwamba ubaya una miguu.  Sheria ile ile ndio iliyotumiwa na Rais aliemfuata Mwanawasa kumtia hatiano Chiluba.

i)          Kulikuwa na makubaliano pia kwamba vyama vya siasa viheshimu Katiba na Sheria za Nchi.  Pamoja na hili, Kamati ilitakiwa kuhakikisha kwamba vyama vya siasa viepukane na kutumia lugha za matusi na kashfa katika mikutano.  Hili kwa ujumla linakwenda vizuri ingawa ni suala ambalo kwa mtazamo wa wengi ni ”subjective“.  Ili hili lifanikiwe pia kuna haja ya wanasiasa kuanza maadili mapya ya kuwajibika ipasavyo na kuwa na uvumilivu wa kisiasa.  Hii ni muhimu kwani mara nyengine kweli huonekana kama kashfa.  Na ikifikia hatua hii, huwa hakuna upinzani.  Hata hivyo, tunakubali kwamba maneno yasio ithibati si mazuri, lakini pia inakuwa vigumu kutaja vilivyoibiwa na ukamficha alieiba katika zama za ukweli na uwazi.

Katika chaguzi zilizopia suala la Sheha kuwa kiungo wa chama badala ya heshima ya kiserikali aliyopewa lilizusha matatizo makubwa katika uchaguzi.  Hata hivyo baada ya marekebisho ya Tume ya Uchaguzi mamlaka ya Sheha ni ya ushuhuda tu na sio tena mwakilishi (agent) wa Tume.  Kwa hivyo, Sheha ambae alikuwa na kauli ya mwisho katika uchaguzi, sasa atapata „kauli ya mwisho“ iwapo tu mawakala wa CUF na vyama vingine vya upinzani wataamua kubweteka na kumpa uwezo afanye atakavyo.

Suala jengine muhimu lililofuatiliwa ni lile la uchuguzi wa Matukio ya vifo vya tarehe 26 na 27, Januari 2001.  tume ya Uchaguzi chini ya Mwenyekiti wake Brigedia Mbita iliundwa  na imewasilisha hadharani uchunguzi wake.  Taarifa hii ya Tume bado haijafanyiwa kazi na vyombo husika.  Hata hivyo, kauli ya mwisho ya Tume ni kwamba yaliyopita yamepita na watu wasameheane.  Suala la kusameheana huwa halihitaji kauli kwani hutegemea kila mtu kalipokea vipi na kalipa uzito gani.  Watu wanaotaka hupatanishwa ili wasameheane wanakuwa na tabia moja.  Kwanza mkosaji huoneshwa makosa yake na akakubali makosa, na wakati huo huo yameonesha wazi kwamba CUF ndio iliyokosa na wakati huo huo, CUF ndio inayotakiwa kusamehe.  Hii ni dosari kubwa ya Tume ya Mbita ambayo imeamua kuipa haki kisogo wakati wa kuchunguza yaliyotokea Januari 26 na 27 Januari, 2001.  Suala hili bado linahitaji mjadala ambao si kazi ya kijitabu hiki.

Sehemu 4: Hitimisho

Sisi kama waandishi wa Kitabu hichi cha matukio ya mauaji ya Januari 26 na 27 2001 tumechangia wajibu wetu wa kuikumbusha jamii nini kilichotokea katika maandamano ya amani yaliyotayarishwa na kufanywa na CUF – Chama  cha Wananchi.  Tumeyakumbuka kwa kuwa ni moja ya kumbukumbu zetu za kisiasa na tunayakumbuka kwa kuwa hatutaki yarejee tena.  Tumejitahidi kuonesha kwamba, pamoja na kuwa Zanzibar imepita katika mkondo wa historia ya ukoloni, lakini historia haiwezi kuwa chanzo cha vitisho, unyanyasaji, uvunjwaji wa haki za binaadamu pamoja na mauaji yaliyoendeshwa na CCM n dola yake tokea kuja kwa mfumo mpya wa vyama vingi.  Ni kweli kwamba yako mengi mabaya katika historia ya kutawaliwa, lakini ndio madhumuni  ya kujitawala kuondosha mabaya.  Kwa kuwa tokea kujitawala ni ASP na TANU na mrithi wao CCM ndivyo vyama pekee vilivyobakia katika madaraka, basi iwapo kuna mabaya ni vyama hivi ndivyo vinavyopaswa kkuulizwa na kuwajibika kwa kushindwa kuondosha mabaya ni vyama hivi ndivyo vinavyopaswa kuulizwa na kuwajibika kwa kushindwa kuondosha mabaya ya kihistoria.  Ni maoni yetu pia kuwa, iwapo kuna watoa hoja wanaosisitiza kuwa historia ya Zanzibar ndio sababu ya matatizo ya kisiasa ya leo, wanaamini hivyo kwa kuwa ajenda ya historia imejengwa kama chaka la kujificha madhalimu ili kuendeleza mabaya dhidi ya wananchi wa Zanzibar.

Kukosekana kwa uwanja wa haki, huru na ulio sawa katika mfumo mpya wa demokrasia ya vyama vingi ndio chimbuko hasa la matatizo na migogoro ya kisiasa iliyoibuka Zanzibar tokea kuja kwa mfumo huu.  Demokrasia ilifichwa ndani ya makoti ya Mapinduzi na Muungano na hivyo kuonekana kama kwamba, mfumo wa vyama haustahili katika nchi iliyojitawala kwa Mapinduzi.  Muungano nao haukufanya jitihada za haraka katika kusimamia na kuleta suluhisho la migogoro iliyotokea.  Ilionekana kuwa; ili kuuhami, kuuenzi na kuuimarisha Muungano unaolegalega na kufifia siku hadi siku, kulitiliwa maanani kuangalia tu na kuzipa nguvu hoja za upande wa Serikali.  Matatizo yamekuwa yakizidi kuikumba Zanzibar na kilele chake kimekuwa kikionekana siku za chaguzi.

Mtihani wa mwanzo ulikuwa katika uchaguzi wa mwanzo wa vyama vingi wa mwaka 1995 ambapo, CUF baada ya kuporwa ushindi wake, ilijitahidi kukataa kunyimwa haki zake za msingi.  Ilikataa kwa kutumia mbinu za kisiasa.   Kati ya mbinu hizi ni kugomea mijadala ya Baraza la Wawakilishi na huku uongozi wety ukihaha kutufuta suluhu ndani na nje ya nchi kwa njia ya muafaka.  Baadae, juhudi za chama chetu zilifana kwa kupata muafaka, lakini uliovizishwa na CCM ilitekeleza kila kilichokuwa wajibu kwake.  Hivyo, kwa kutotekelezwa muafaka, tulilazimika kuingia katika uchaguzi wa pili wa mwaka 2000 katika mazingira mabaya zaidi.  Hadi tulipopofika katika uchaguzi, nchi ilikuwa tayari ikiogelea katika dimbwi la zahma za machafuko na uvunjwaji mkubwa wa haki za binaadamu ulioambatana na uvurugwaji mkubwa wa taratibu za uchaguzi.  Mwishowe, ilifikia hadi kwamba, baada ya yale yalioitwa na Tume ya Uchaguzi kuwa ni matokeo, wachunguzi wa ndani na nje waliafiki kwamba hakukuwa na uchaguzi „bali ni uchafuzi“.

Si CUF ilianza na kauli ya kutaka uchaguzi  urejewe.  Jumuiya ya Kimaifa, na za Haki za Binaadamu pamoja na zile zilizoleta  Waangalizi wa uchaguzi zilikuwa wazi kwamba uchaguzi ule lazima urejewe.  Kama CUF ingekaa kimya basi ingestahiki ionekane kama kwamba iliridhika na yote waliyofanyiwa.  Tuliendelea kama mwanzo na jitihada za kuwaomba wenzetu wakae waangalie hatma  ya nchi badala ya madaraka.  Hata hivyo, kama kawaida yake CCM ilipuuza.  Ilikuwa na haki ya kupuuza kwani ilishatangaza bayana kwamba nchi iliyopatikana kwa Mapinduzi haiwzi kuongozwa kwa ustaarabu wa demokrasia ya vikaratasi.  Ndio kura ilivyoitwa, baada ya CCM „kukubali mfumo wa vyama vingi eti bila kushawishiwa“!  wimbo haunogi hadi upate ngoma.  Ndio maana maandamano ya amani tuliyoyaitisha yalikuwa na madhumuni ya kunogesha wimbo ambao sasa uligeuka na kuwa madai, tena madai ya haki ya kutaka uchaguzi urejewe.  CCM haikuvumilia kuambiwa hadharani tena wazi wazi.  Ndipo ilipoituma dola ifanye kazi chafu na ya kikatili.  Ilikatili roho za viumbe na kunajisiwa, wengine kuvunjwa viungo vya miili yao na sasa ni vilema.  Wengine walikimbia nje ya Tanzania.

Baada ya kadhia yote hiyo, chama chetu kilichagua kuendelea na madai ya haki kuwa ndio dira yetu.  Haki haipotei lakini kwa vile huchelewa basi inahiraji uvumilivu wa hali ya juu.  Tulikubali nasi kuendelea na ustaarabu wa uvumilivu japo ndio tulioonewa.  Mwishowe tukawachilia mbali yale madai ya kurejea uchaguzi na kukubali kukaa na wenzetu na kutengeneza mazingira mapya na ya kudumu kwa hatma ya nchi kisiasa, kijamii na kiuchumi.  Hii ni kusema tulikubaliana na muafaka tulioupigania kwa miaka 5 bila mafanikio.  Muafaka unatarajiwa kutekeleza mambo ya msingi ya kuifanya demokrasia ifanya kazi katika misingi ya haki na usawa.

Kwa kuwa kuna vipengele vingi vya muafaka vimekwisha tekelezwa.  Tuna matumaini kwamba twendako ndiko hasa kunakotakiwa na mfumo.  Hata hivyo, tunasikitishwa kwamba bado kuna mambo ambayo yanahitaji kutekelezwa lakini bado hayajatekelezwa.  Ingawa baadhi ya watu wanayaona madogo, lakini haya ni makubwa wasubiri tena yaliopita.  Huu si uamuzi sahihi na pengine isiwe hivyo, lakini imani za watu ndiko zinakoelekezwa.  Kazi moja kubwa ya muafaka ulikuwa ni kujenga imani na hili lilipata vipingamizi vingi kwa umma lakini mwishowe Makatibu Wakuu wa vyama walifanikiwa.

Tulikwisha jenga matarajio mazuri kwa muafaka, lakini tuna mashaka safari yetu iliyoanza vizuri si wote wanaoitakia mema.  Pamoja na mambo ya msingi yaliyokwishapatikana katika utekelezaji wa muafaka, bado kuna wasi wasi kwamba safari yetu itatiwa dosari baadae na watu wasioitakia mema Zanzibar.  Watu wa aina hii wapo na wanatumia zaidi baadhi ya vyombo vya dola ili kudhoofisha umoja wetu.  Tuna wasi wasi kuwa mpango was siri wa Serikali wa kuimarisha makambi ya askari wasio na kazi katika majimbo imekusudiwa kuongeza idadi ya wapiga kura ili kuisaidia CCM.  Hivyo muafaka upo, lakini pia ziko jitihada za kuufikisha muafaka pabaya, sio tu katika hatua za kiutekelezaji, lakini katika kufanya mambo yatakayovunja moyo na kupoteza imani za watu waliokwishaamua kukaa pamoja na kurejesha umoja.  Inasikitisha kwamba ni muhimili wa Serikali ndio unaotia wasi wasi katika safari yetu.

Mwishoni mwa miaka ya 90 Serikali ya Muungano ilijitahidi kufanya mikakati ya kuvivunja baadhi ya vikosi vya SMZ na hata kufikiria kuviunganisha vingine na vile vya Bara.  Hata hivyo, katika CCM ya awamu ya sita ya Mheshimiwa Amani, yeye kaamua kuviongeza zaidi vikosi na Serikali ya Muungano sasa haioni tena ile haja ya kuviunganisha isipokuwa kumpa baraka zaidi Rais Amani kwa kukubali vikosi hivyo vifanye kazi bega kwa bega na Polisi wa Muungano.  Hili linazusha masuala mengi ambayo kila mtu atajiuliza, lakini lina jambo moja la msingi katika Muafaka.  Nalo ni kujenga shaka.  Shaka kubwa ni kuwa kunaweza kujitokeza matatizo mengine ya magomvi na fujo iwapo juhudi hazitofanywa kuwajengea mazingira na maadili bora ya kazi zao.  Vikosi vya SMZ ni miongoni mwa ndugu zetu na watu wake.  Tutashirikiana nao kwa mazuri, lakini tutakataa kama kuna mabaya watakayoyafanya.  Tunasema hivi kwa kuwa, kwa kiasi kikubwa vikosi vilichangia kuleta maafa makubwa kwa raia siku za magomvi na migogoro.

Kasoro nyengine  kubwa iliyobakia katika mazingira yetu ya kuimarisha demokrasia inatokana na Serikali kuendelea kuhodhi vyombo vya habari.  Serikali katika mkakati wake inajitahidi kuhakikisha kwamba wapinzani hawavikaribii.  Pamoja na kuendelea kumiliki vile vyombo vya umma vya habari, lakini pia wamefanikiwa kuvirubuni na kuvitumilia vyombo binafsi vinavyoonekana vikwazo kwa Serikali inavizisha demokrasia na inapalilia kutowajibika na rushwa kwa vyombo vyake vya dola.  Vyombo binafsi vya habari vikikubaliana na maovu ya Serikali, maana yake vimekubali kutumiliwa ili kuwakosesha wananchi manufaa makubwa ya mfumo wa vvyama vingi unaosisitiza utawala bora na wa sheria pamoja a ulinzi wa haki za binaadamu kama misingi muhimu ya demokrasia.  Hali ya kumiliki habari ikiendelea inatuelekeza katika hali ile ile ya kurejesha vurugu na mauaji yaliyopita.  Hatufikirii iwapo haya yatatokea, Zanzibar itahitaji muafaka mwengine.

Twaitakia heri Demokrasia  ya vyama vingi na twaitakia heri Tanzania na hatma ya Zanzibar.  Ingawa kwa ujumla hatutarajii mabaya lakini pamoja na yote mema kuendeleza siasa za ushindani wa vyama vingi.  Waandishi wanamalizia kwa kuwatakia heri Wana CUF na Watanzania wote.  Waandishi wanategemea kwamba wanasiasa watashindana ndani na nje ya vyama kuendeleza demokrasia huku wakiamini katika maadili ya aina moja ambayo ni “shindana ushinde au ushindwe lakini mwishowe ushirikiane”.  Mwisho kabisa ni haki sawa kwa wote.

MAREJESHO

Aboud Jumbe

“The Partner  ship” Muungano wa Tanganyika Zanzibar miaka 30 ya Dhoruba, Amana Publishers Dar, 1995

Bates, M. L.

Tanganyika under British Administration 1920 – 1955.  Ph D Thesis, Oxford University, 1957.

Clayton, A.

“The General Strike in Zanzibar, 1984”, Journal of African History XVII, 3, 1976.

Duggan, W. R and J. R. Civille,

Tanzania and Nyerer: A study of Ujamaa and Nationhood, Maryknoll: Orbis Books, 1976

ESAURP

The Road to Democracy, Tema Publishers Company, Ltd, 1998.

Gaseti la Rai la tarehe 31 May, 2001.

Gray, J

History of Zanzibar from the Middle Ages to 1856, London: OUP, 1962

Othman, Haroub

“Kufifia kwa Muungano?”, waraka juu ya hali ya Kisiasa Tanzania, 1996.

Hollongworth

Zanzibar Under Foreign Office 1890 – 1913.  lond: Macmillan, 1953.

Illife, J.

A history of Dockworkers of Dar es salaam, Tanganyika notes and records, No. 71, 1970.

Kaniki, M.

Tanganyika under Colonial Rule.  London: Longman, 1979

Kumbu kumbu za CUF – Chama cha Wananchi.

Kitabu cha Muafaka wa kisiasa baina ya CCM na CUF

Lofchie, M.

Zanzibar: Background to Revolution.  Princeton: Princeton University Press 1965.

Maliyamkono, T.

The Political Plight of Zanzibar.  Dar: TEMA Publishers Co. Ltd, 2000.

Mdundo, O.

Masimulizi ya Sheikh Thabit Kombo Jecha, DUP, 1999

REDET

Political Culture and Popular Participation, Na. 2, Redet Publication, University of Dar es salaam, 1997.

Robert V. Makaramba.

A new Costitutional Order for Tanzania? WHY AND HOW.  Tanganyika Law Society, Dar., 1997.

Ayany, Samuel G.

A History of Zanzibar: A study in Constitutional Development (1934 – 1964).  Kenya Literature Bureau, 1970

Shariff A & Ed Ferguson.

Zanzibar Under Colonial Rule.  London: James Currey, 1991

Shivji, I. G.

Law, State and the Working Class in Tanzania, London: James Currey and Dar es salaam: TPH, 1986.

Wilson, A

US Foreign Policy and Revolution: The Creation of Tanzania.  London: Pluto Press, 1989.

Bakar, M. A.

“Competition or Confrontation” in Political Culture and Popular Participation in Tanzania, REDET Publication No. 2, University of Dar es Salaam University Press, 2000.

Bakar, M. A.

The democratization Process in Zanzibar: A Retarded Transition.  Hambury: Institute of African Affairs, 2001.

Chachage, C.S.L.

Environment, Aid and Politics in Zanzibar.  Dar es salaam:  Dar es salaam  University Press, 2000.

TEMCO

The 2000 General Elections in Tanzania.  Report of the Tanzania Elections Mornitoring Committee, 2000.

Maliyamkono, T.

Tanzania on the Move.  Dar es salaam: Tema Publishers, 1997.

Mmuya, Max and A. Chaligha

Towards Multiparty Politics in Tanzania.  Dar es salaam:    Dar es salaam University Press.

Mmuya, Max and A. Chaligha

The Anticlimax in Kwahani Zanzibar; Participation and Multipartism in Tanzania.  Dar es Salaam University Press, 1993

Mmuya, M.

Tanzania; Political Reform in Eclipse; Crises and Clearages in Political Parties.  Dar es Salaam; Friedrich Ebert Stiftung

Mukandala, R.S and H. Othman

Liberalisation and Politics; The 1990 Election in Tanzania.  Dar es Salaam; Dar es salaam University Press, 1994

Okello, John

Revolution in Zanzibar. Nairobi; East African Publishing House, 1967

DIBAJI





Mauaji ya 2001: Januari 26 na 27

17 12 2008

SURA YA SABA

MAUAJI YA JANUARI 26 NA 27, 2001

Mwanzoni tuligusia historia ili tuone kama ina sababu tosha  ya kusababisha mauaji katika siasa za leo kama inavyodaiwa na baadhi ya wachunguzi wa mambo ya kisiasa na wanasiasa wa hapa kwetu.  Tumeona kwamba hili halina ukweli wowote.  Kwa kuwa sababu hii haina ukweli, basi maelezo yaliyofuata tukataja kisa na sababu hasa za mauaji yale.  Baada ya hapa tukaendelea na chaguzi za mfumo wa sasa tunaelezea namna mauaji yalivyotokea.  Tunaona kwamba ingawa mauaji haya yalifanyika Tanzania nzima, lakin yalifanyika kwa kiwango kikubwa Zanzibar na ambako Pemba yalitia for a.  si hayo tu, kwa kuwa mauaji yalianza kutokea tarehe 26 Januari 2001 siku ambayo chama chetu hakikuwa na maandamano, na kwa kuwa zaidi yalitokea msikitini, basi bado inatia wasiwasi iwapo mauaji yaliyoendeshwa na Serikali ya Tanzania yalikuwa na sababu za kisiasa.  Sasa endelea kusoma upate maelezo zaidi.

Sehemu ya 1: kwa nini Tuliamua kuandamana?

Mauaji yalitokea Tanzania nzima, hasa Zanzibar na zaidi Pemba.  Hapana shaka pamoja na kwamba mapungufu mengi yamekuwa yakichangia kuchafuka kwa mazingira ya kisiasa Zanzibar, lakini tokea kuja kwa mfumo wa vyama vingi, chaguzi zimekuja kuivisha matatizo na kuanzisha migogoro na machafuko.  Ingawa kuvurugwa kwa uchaguzi wapili wa vyama vingi ndiko kulikoleta malalamiiko yaliyojibiwa na dola kwa umwagaji damu, lakini huku pia kulikuwa mwanzo wa ishara za kutokubalika kuchezewa demokrasia kwa siku za baadae ndani ya mfumo wa vyama vingi.

Tuliona kwamba uchaguzi  wa kwanza wa vyama vingi wa mwaka 1995 ulivurugwa na sisi tukasusia kumtambua Rais wa Zanzibar aliepewa madaraka na Tume ya Uchaguzi iliyoundwa na Rais mwenyewe kutokana na wajumbe wa chama chake.  Vile vile, tulichukuwa hatua ya kutochangia miswada katika Baraza la Wawakilishi.  Huu ulikuwa ni uamuzi wa chama chetu uliokusudiwa kuinesha Tanzania na dunia jinsi ya kuchukizwa kwetu na kuvurugwa kwa maksudi misingi na maana halisi ya demokrasia ya mfumo mpya wa vyama pamoja na kupinga ukiukwaji wa hakiza binaadamu uliokithiri katika uendeshaji wa uchaguzi na vile vile wakati wa kushangilia matokeo yaliyopora ushindi wa chama chetu.

Tulitembea kote Tanzania na mwishowe katika pembe za ulimwengu kutafuta namna ya kuboresha hali ya kisiasa iliyoanza kuvurugika baada ya kuapishwa asiekuwa mshindi.  Juhudi hii ilikuwa ni ishara ya wazi ya uungwana wetu wa kuwa tayari kuvumilia kadhia yote, pamoja na kwamba ndio tulioonewa.  Tuliomba angalau tukae na wenzetu ili tujenge misingi mipya ya maelewano na umoja wa nchi yetu.  Pamoja na hili, tilikuwa pia na hoja ya kuangaliwa kwa undani sababu zilizochangia uvurugwaji wa uchaguzi ule, ili kupata fursa ya kuandaa taratibu bora zaidi kwa chaguzi zitakazofuata.

Juhudi za chama chetu kufikia lengo la makubaliano zilikabiliwa na upinzani mkali ndani ya CCM pamoja na Serikali zake mbili za Zanzibar na Jamuhuri ya Muungano.  Hii ndio maana ilituchukua karibu miaka minne toke tulipoanza kuwaomba wenzetu tukae tuzungumze, licha ya kwamba hatukuchelea hata kuwaomba wengine watukutanishe ili tuitafakari hali ya kisiasa ya Zanzibar iliyoanza kuchafuka kwa kasi.  Tulipohisi katika jitihada zetu hakuba uwezekano wa kufikana tulitegemea sana Muungano wetu utuunganishe.  Tuliamua tuijaribu ile falsafa inayoenezwa na Serikali kwamba kwa vile Muungano wetu ni wa watu wote kwa faida ya wote, basi suluhisho ya matatizo yetu yamo ndani ya Muungano wenyewe.  Hata hivyo, dhana hii haikutoa jibu la “ndio” kwa mara moja.

Ilikuwa ni mwezi wa Juni 1999 ndipo CCM hatimae ilikubali kukaa, japo “shingo begani”.  Safari yetu ya kusihi ilianzia mwezi wa Novemba, 1995, mara tu baada ya uchaguzi wa Oktoba 26, 1996.  hata hivyo, ilikuwa ni sahihi tuliposema CCM walikubali shingo begani, kwani mazungumzo yetu hayakutoa cha maana baada ya wao kukataa kutekeleza kila kipengele kilichowahusu cha muafaka wetu wa Juni 9, 1999.  haikuwa dhihaka ila kulikuwa na ukweli kwamba hata neno Muafaka walilikataa na wakasisitiza liitwe “Makubaliano”.  Hata hivyo pia walikataa kukubaliana.

Baada ya hapo tuliona, kilichobakia ni kukaa na kuangalia nini kingetokea katika uchaguzi wa pili wa vyama vingi uliotukabili siku chache tu baada ya makubaliano yaliyovia.  Huu ulikuwa ni Uchaguzi wa pIli wa vyama vingi uliotarajiwa tareh 29, Oktoba 2000.  Ingawa kilichotokea tumeshakielezea lakini matokeo ya mwisho yalikuwa, kuzidi kuvurugwa kwa uchaguzi huo kulikoambatana na uvunjwaji mkubwa zaidi wa haki za binaadamu na udhalilishaji wa daraja ya juu.  Tulilazimika kama chama chenye malengo na sera zinazokubaliwa na watu ambao ubinaadamu wao haupitani na ule wa CCM, kujitutumua zaidi na kuweka madai yetu ya kuvurugwa demokrasia bayana pamoja na kupinga udhalilishajji kwa sauti kubwa zaidi lakini kwa amani tupu.

Hili halikuwa onesho bali ni jaribio la lazima kwani wakati mwengne, licha ya kwamba jitihada zetu za kidiplomasia  zilidharauliwa kwa nje, lakini pia kwa ndani zilisutwa kwa kila aina ya kebehi.  Kwa mfano, Maliyamkono (2000) anamnukuu aliekuwa Naibu Waziri Kiongozi Mapuri (1996), na wote wanakubaliana kwamba misururu ya safari za Maalim Serif Sharif nje ya nchi baada ya uchaguzi wa 1995, zilikuwa na lengo la kukutana na aliekuwa kiongozi wa Hizbu Ali Muhsin kwa upande wa Ghuba na vivyo hivyo kwa Uingereza, alikuwa akienda ili kukutana na Mfalme Jemshid aliepinduliwa mwaka 1964.  kitabu cha Mapuri kinafundishiwa somo la Historia katika maskuli ya Zanzibar baaa ya somo hilo kufutwa kwa zaidi ya miongo miwili kwa kuonekana kwamba vitabu vya historia vilivyokuwepo havikidhi haja ya kuipotoa historia.

Kwa hivyo basi kujitutumua kulikoamuliwa na chama ni kufanya maandamano na kuwahutubia wananchi juu ya madai yetu ya kutokukubaliana na matokeo ya uchaguzi wa pili, kupinga vitendo vya ukiukwaji wa haki za binaadamu pamoja na kutaka uchaguzi uliochafuliwa urejewe.  Si zaidi ya hapo na haya yanathibitishwa na kumbukumbu za azimio la Baraza Kuu la Uongozi la Chama kama lilivyotolewa katika kikao chake cha Novemba 9, 2000 na kutiwa saini na Mwenyekiti wa Chama Profesa Ibrahim Lipumba.  Azimio hilo pamoja na mambo mengine, kuhusiana na uchaguzi wa Oktoba 29,2000 lilitamka kwamba:

?          CUF inadai kufanyika kwa uchaguzi mpya haraka:

?          Tunatamka kwamba Tume ya Uchaguzi (ZEC) iliopo sasa hivi iwajibike na Tume mpya yenye ridhaa ya vyama vyote iundwe;

?          Kwa kipindi chote kabla ya uchaguzi mpya, CUF haitamtambua Amani Abeid Karume kama Rais halali wa Zanzibar pamoja na Serikali yake.

?          Wawakilishi waliotangazwa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) na Wabunge waliotangazwa na Tume ya Uchaguzi ya Taifa (NEC) hawatashiriki kula kiapo cha utiifu maana uchaguzi huo sio halali na ulivurugwa kwa Zanzibar.

Kifungu cha 167 cha Taarifa ya Uchunguzi wa mauaji ya Tume ya Mbita kinaeleza kwamba, Tamko letu lilikuwa ndio msingi wa Chama cha CUF kuitisha maandamano ya tarehe 26 na 27 Januari, 2001.  huu ni uongo dhahiri, na baya zaidi ni kwamba uongo huu kwa vile umejitokeza mwanzoni mwa uchunguzi wa Tume ya Mbia, basi ndio sawa na msingi wa uchuguzi wake.  Tamko letu ni la maandishi na liliweka wazi kuwa Chama kingeshirikiana na watu kudai haki yao kwa njia yoyote watakayo amua.  Baada ya tamko hili ndio maana Chama kikaamua kufanya maandamano siku na tarehe moja tu, yaani Jumamosi 27 Januari, 2001.  Hili halikuwa jambo la siri na ndio maana vyombo vyote vya Habari nchini vilitoa matangazo ya kuzuia uhuru huu tena vikimaanisha siku hiyo tu na sio Ijumaa ya tarehe 26 januari, 2001 ambapo Serikali ilianza kuuwa bila sababu.

Tuna hakika Mheshimiwa Mbita anazo kumbukumbu hizi kama moja ya vielelezo vya CUF, lakini aliamua kuupotoa ukweli na kuudanganya ulimwengu.  Kwa sababu hi ya msingi ni sawa na kusema kwamba mauaji ya Januari 26 hayakuwa nya kisiasa hasa kwa vile hakukuwa na maandamano ya aina yoyote.  Yawezekana basi, kwa kuwa mauaki ya tarehe 26  yalifanyika Msikitini, pengine Serikali ilikwisha amua kuendesha mauaji kwa sababu nyengine zaidi ya siasa.  Kwa hivyo, ni shida kuamini kuwa siasa ni tatizo linaloweza kufanya maafa kama hayo kwa Zanzibar ya leo bila ya kuchanganya mambo mengine ambayo Serikali inayaelewa zaidi kuliko jamii ya Watanzania.

Tamko lilizidi kusema:

“Kwa kuwa Zanzibar ni sehemu ya jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pia CUF hakimtambui Mheshimiwa Benjamin W. Mkapa kuwa ni Rais halali wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali yake kwa sababu hawakuchaguliwa na wananchi wa Zanzibar.  Vile vile, kwa uchaguzi uliofanyika Tanzania Bara, Baraza Kuu la Uongozi linalaani vitendo vyote vya wizi wa kura, udanganyifu, na utumiaji wa nguvu za dola uliojitokeza katika hatua zote za uchaguzi huo.  Hivyo basi Chama kinawaagiza Wagombea wote waliodhulumiwa kwa njia moja au nyengine kupeleka malalmiko yao mahakamani”.  Mwisho wa kunukuu.

Tunarudia kusema kuwa, ni kufuatia Kikao hicho cha Baraza Kuu Taifa basi ndio Chama kilianzimia kufanya maandamano hayo ya Januari 27,2001 ili kuweka bayana maazimio yake na vile vile kuitumia mikutano ya hadhara kurejesha imani na kujenga matumaini ya wanachama baada ya dharuba kali ya ‘uchaguzi wa kishindo’.  Ni bahati mbaya basi, pengine Jeshi la Usalama wa Taifa lilimshauri vibaya Amiri Jeshi Mkuu kwamba maandamano yalikusudia kuondosha tawala zao za enzi na ndio hatimae wakamfikisha kutoa amri mbaya ya kuua raia zake.

Watu wakauliwa bure bila hatia na sisi tuliobaki tumeachiwa zivuka jamani, tumeachiwa mayatima jamani, tumeachiwa vilema jamani.  Tukageuzwa wakimbizi wa lazima jamani.  Mama na dada zetu waliingiliwa kwa nguvu tena hadharani jamani.  Wazee walivutwa ndevu kama siku ya Mapinduzi jamani.  Hawakujali ulemavu, uzee, utoto wa ujinsia; walipiga, walinyang’anya, walinajisi na pia kuuwa.  Hata Mwenyekiti wetu Profesa Lipumba alipigwa kwa marungu na kurudishwa rumande jamani.  Yote haya hayakuwa na bahati mbaya, ingawa pia hayakuwa na sababu za lazima kufanywa na Serikali inayosaidiwa na kutangazwa na mataifa makuu ya dunia kkuwa inaendeleza uchumi na demokrasia.  Bado tunazidi kujiuliza, iwapo waliouliwa Januari 27, waliuliwa kwa maandamano yaliyopigwa marufuku na Serikali jee, wale waliouliwa msikitini tarehe 26 kabla ya siku ya maandamano, wao walikuwa na kosa gani?  Jee ni siasa tu au kuna jengine?  Jee, huku ndiko kukubali mfumo wa vyama kwa hiari?  Tanzania twaelekea wapi?

Sehemu ya 2: Matayarisho ya Maandamano

7.2.1    Matayarisho ya awali

Kufuatia tamko la Baraza Kuu, Chama chetu kilitoa taarifa Polisi kwamba kinataka kufanya maandamano ya amani na mikutano ya hadhara siku ya jumamosi Januari 27, 2001 katika sehemu mbali mbali katika nchi.  Madhumuni yake ni kama tulivyoeleza katika muhtasari uliotangulia.  Yaani, kutamka hadharani kwa wanachama wetu, kutoridhishwa kwa chama chetu, na namna uchaguzi wa mwaka 2000 ulivyoendeshwa na namna baada ya hapo, unyanyasaji na ukiukwaji wa haki za binaadamu unavyochukuwa nafasi ya “amani na utulivu” Tanzania.  Ni haya tu basi.  Ndio maana tukawaomba waandamanaji kujifunga vitambaa vyeupe kama ishara ya amani.

Azma ya pili ilikuwa ni kuamsha hamasa za chama pamoja na kujenga imani na matumaini kwa wanachama wetu baada ya kuvunjikka moyo kutokana na uendeshwaji mbaya wa uchaguzi na mapishi ya matokeo yake.  Barua ziliandikwa na kila wilaya ya chama chetu, il kuwaarifu Polisi katika sehemu zao watupatie mapema kabla ya wiki tatu ili kuipa nafasi Serikali kupanga mipango yake ya kiusalama.  Kwa kawaida sisi huwa hatuhitaji walinzi katika mikutano yetu kwani walinzi wetu wa chama yaani Blue Guards na White Guards wanatosha kuweka hali ya utulivu katika mikutano yetu.  Wanatosha hasa kwa kuwa mikutano yetu haina fujo.  Tulitoa taarifa kwa kuwa sheria ndivyo inavyotutaka tutoe taarifa kwa Polisi si chini ya masaa 48.  Tena sheria inasema kutoa taarifa na sio kuomba ruhusa.  Kwa hivyo, anaeomba ruhusa waweza mzuia, lakini anaetoa taarifa na sio kuomba ruhusa.  Kwa hivyo, anaeomba ruhusa waweza mzuia, lakini anaetoa taarida kwa wingi waweza mshauri wakati mzuri wa kudanya jambo na sio kumzuia kabisa.  Serikali za Tanzania zimezoeza kuweka vifungu vya Katiba na sheria zinazoruhusu mambo ili kuuhadaa ulimwengu tu na inapokuja hatua ya utekelezaji, amri ya kiongozi huwa juu kuliko matakwa ya Katiba na sheria.  Ndio maana Serikali ilipozuia maandamano ilisema kwa “amri halali” na sio kwa mujibu wa vifungu vya “Katiba na Sheria”.

Kutokana na barua yetu ya taarifa, Polisi walijibu baadae kwamba, maandamano yetu yalipigwa marufuku.  Hakukuwa na sababu za mapungufu ya kiusalama kama kawaida yao, maana mara nyingi pakiwa na sabau hizo basi Serikali husema pangeni siku nyengine, lakini mara hii ilikuwa ni kupiga marufuku moja kwa moja bila hoja zaidi.  Vikwazo hivi vya vyombo vya dola havikubuniwa tu, lakini ilikusudiwa kutekeleza matakwa ya kibinasi ya Amiri Jeshi Mkuu Benjamin Mkapa.  Licha ya kuwa ndo Amiri Jeshi Mkuu, pia ndie Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano; na kwa mujibu wa Baba wa Taifa katika siku za kumnadi, ndie Bwana Msafi (Me. Clean) Tanzania.  Kauli ya kupiga marufuku harakati za kisiasa alizotoa mbele ya umma wa Tanzania zikishuhudiwa pia na Jumuiya za Kimataifa mara tu baada ya kuapishwa kwa mara ya pili kuwa Rais.  Kwa ufupi alisema kwamba, mara tu baada ya kurejeshwa tena Ikulu asingependa kuona harakati za vyama vya upinzani kwani alihitaji wasaa wa kutekeleza sera za CCM kama alivyoahidi katika ilani ya uchaguzi.  Huu ndie “Bwana Msafi”  anavyotekeleza demokrasia Tanzania.

Rais Mkapa anamaliza muda wake wa Urais, lakini kwa kawaida ya mila na desturi zetu Tanzania, Rais anaeondoka madarakani ndie anaemuonesha kidole yule anaetarajiwa kuwa Mgombea katika chama chake.  Ndivyo alivyofanya Baba wa Taifa, Mwalimu na bila shaka ndivyo atakavyofanya Bwana Msafi.  Na iwapo Msafi katufikisha hapa, sijui Mtanashati atakae muelekeza kidole ataifikisha wapi Tanzania iwapo atapewa ridhaa ya watu! Sisi hatumjui ndio maana tuna wasi wasi na tunatoa wasi wasi wetu mapema sana ambapo leo  ni miaka miwili kabla ya Uchaguzi Mkuu wa Tatu wa vyama vingi wa Oktoba, 2005.  tunawajibu wa kusema hivyo kwa kuwa tunaambiwa na wana historia kuwa historia hujirudia.

Amri hii ya Amiri Jeshi Mkuu licha ya kwamba ilipingana na misingi yote ya demokrasia na haki za kujumuika, lakini pia ilishtusha kutolewa na Rais Mkapa.  Itakumbukwa kwamba, ni yeye aliemiminiwa sifa tele kutoka kwa Jumuiya ya Kimataifa na vyombo vya fedha hasa Benki ya Dunia na Shirika la Fedha Duniani kwa jitihada zake za kurejesha demokrasia, uongozi bora na kufufua uchumi, katika kipindi cha awamu yake ya kwanza (a995 – 2000).  Kauli ya Mkapa iliendana na ile “ushindi wa kishindo” katika nchi ya siasa za ushindani.  Hata hivyo, kauli ya Mkapa ilipokelewa kwa mshangao mkubwa na vyama vingine hadi wengine kufikiria kwamba ni kigugumizi cha kuteleza kwa ulimi tu.  Kwa urasmi wa vyama kutokana na kusajiliwa na Serikali na kwa umuhimu wa harakati zao za kuirekebisha, kuikosoa na kuielekeza Serikali, wengine walidhani Tais aliogopa Serikali kukosolewa.  Hata hivyo, wapinzani walidhani Rais angewaandikia rasmi katika vyama vyao kuthibitisha utaratibu huu mpya ya awamu yake.

Pamoja na vitisho na kauli kali za vyombo vya dola, sisi tuliendelea na matayarisho yetu ya maandamano kwani tulijuwa kuwa nchi hii haiendeshwi kwa amri, bali inaendeshwa na sheria.  Tulijuwa kwamba Wafalme wakivaa kofia mbili kwa wakati mmoja, hutokeza shida ya namna ya kuzidengua.  Mkapa yeye ana kofia mbili, na hivyo hatukujua alikuwa akitumia ipi wakati ule, ama ya Uenyekiti wa chama au Uamiri Jeshi Mkuu.  Tena tukumbuke kwamba Rais aliapishwa mwezi wa Novemba 2000, na sisi tulitaaribu tufanye maandamano mwisho wa mwezi wa Januari mwaka uliofuata.  Hivyo, kwa vyovyoe vile maandamani yetu hayakukusudiwa kumzuia asifanye kazi zake za Urais.

Haki ya uhuru wa mawazo na kujumuika imeelezwa katika vifungu vya 18 hadi 21 vya katiba.  Kwa mfano Kif. 20(1) cha Katiba ya jamhuri ya Muungano wa Tanzania kinasema, “Kila mtu anastahiki kuwa huru, bila ya kuathiri sheria za nchi, kukutana na watu wengine kwa hiari yake na kwa amani, kuchanganyika na kushirikiana na watu wengine, tkuo mawazo hadharani, na hasa zaidi kuanzisha au kujiunga na vyama au mashirika yaliyoanzishwa kwa madhumuni ya kuhifadhi au kuendeleza imani au maslahi yake au maslahi mengineyo”.  Ni Katiba hii ndio Rais alioikamata na kuapa kuitumikia na kuilinda.  Ndio tukasema wengi hatukuamini kuwa alikuwa hadhiri alipokuwa akitoa kauli ili.

Bila shaka maneno “bila kuathiri sheria za nchi” katika Katiba haina maana kwamba sheria ndio zilizo juu ya Katiba, lakini Sheria zinakuwepo kutandika utaratibu bora wa kuitekeleza Katiba na sio kuifanya isifanye kazi.  Na ikitokea kuna sheria huathirika kwa matakwa ya Katiba au inazuia Katiba isifanye kazi, basi sheria hiyo ni miongoni mwa sheria kandamizi (oppressive laws) ambazo Jaji Mkuu Mstaafu Fransis Nyalali alishauri zifutwe ili kuwa na mazingira bora ya kutekeleza demokrasia.  Hata hivyo, kwa kuwa Tanzania haina ukweli katika kutekeleza demokrasia ya vyama vingi, ndio maana ikakataa kuzifuta na leo inazitumia sio tu kwa kuzuia demokrasia ya kweli ya vyama vingi, bali inazitumia kwa visingizio vya kumaliza maisha ya Watanzania.  Imekuwa mara nyingi ikidaiwa na vyama vya upinzania kwamba kunahitajika angalau badi kuzifanyia marekebisho sheria za ukandamizaji lakini Serikali hujibu hakuna sheria za namna hiyo Tanzania.

Kama hii ndio imani thabit ya Serikali, basi hii na maana kwamba huku ni kukubali kwa Serikali kuwa Sheria zilizopo zintia nguzu Katiba na zaidi zinasaidia Katiba hiyo ifanye kazi.  Kwa mantiki hii, Serikali inaamini kwamba hakuna katika Tanzania, uwezekano wa matakwa na haki za kikatiba kuathiri sheria zilizopo.  Ukweli huu ndio uliotuongoza sisi katika CUF kutoa notisi ya taarifa ili kutumia haki yetu ya kikatiba tena kwa mujibu wa sheria ambayo inataka muombaji wa mkutano atoe taarifa (sio ombi) ya masaa 48 kwa Polisi kabla ya shughuli yenyewe.

Hivyo, hatukuona mantiki kwa dola kusema tulivunja sheria, ila tulijua tu kwamba vyombo vya dola vilitumika kusaidia matakwa ya CCM na kwa hili lilionekana na chama chetu kama kebehi ya mwisho ya demokrasia.  CUF kama chama kikuu cha upinzani kina jukumu tangulizi (leading role) katika jamii ili pia kulinda hadhi ya vyama vingine.  Vyama vya upinzani vyenye upinzani wa kweli hawatasahhau kujitosa na kujitoa muhanga kwa wanachama wetu katika kuitetea demokrasia.  Sote tulikwisha pigwa mweleka kwa kauli ya Mkapa, lakini baada ya maandamano tulisimama tena kwa pamoja.  Zaidi ya yote chama chetu ndicho chama mbadala kwa mujibu wa maoni ya wananchi yaliyojitokeza katika uchaguzi uliopita licha ya mizengwe yote ya CCM na vyombo vya dola ya udanganyifu katika kura.  Hivyo, tunajukumu la kuona kwamba imani hii haipotei bali inashamiri ili kupata uwezo wa kuiongoza dola.  Zote  hizi ni sababu za kuwa na haja ya kuzungumza na watu kila mara na kwa nafasi tena bila vizingiti.  Haya ndio mambo ya msingi yaliyotulazimisha kuwa na mikutano na maandamano ili  kushajiisha na ujumbe wetu upate kusikika vyama.  Hatukuwa na jengine zaidi ya hili.

Tabia za kulazimisha ushindi zina hasara zake, na zaidi ushindi wa kishindo ni “ushindi shinda” na athari zake kwa mshindi wa kishindo ni kuogopa vishindo vya baadae vya ushindi bandia. Ukweli wa ushindi wa aina hii ni kwamba, akubalipo mmoja wenu kuwa kashinda kwa kishindo, hili haliwezi kumuondoshea hofu mshindi wa aina hii ya kuwa pia anaweza kuondoshwa kwa kishindo.  Hofu ya kulazimisha ushindi huikosesha Serikali ilioko madarakani imani kwa wananchi.  Na kwa hivyo, Serikali hujizatiti kujijengea imani (confidence) kwa rungu ya dola kwani Serikali kama hii siku zote hutaka iogopwe.

Mambo mawili makubwa yalichangia kupandisha munkari kwa dola baada ya uchaguzi.  Kwanza ni ile tabia ya baadhi ya vyama kukataa maoni ya wanachama wao walio wengi juu ya nani awe mgombea.  Mgombea wa namna hii hukataliwa na wanachama wake pamoja na wale wa vyama vingine.  Anaelezimisha huwa kajifedhehesha kwani huambukia kura chache na mwishowe hutafuta wapi kwa kusukumia lawama.  Hivi ndivyo Mkapa alivyotaka kuhakikisha kwamba Mgombea wake anatawala kwa hali yoyote.  Na hili ndilo hasa lililomlazimisha ahiari kuuwa ili kunyamazisha kila kilichojitokeza kuwa ni bghudha kwa utawala wa kishindo.

Sababu nyengine ni ule ukweli kwamba Tanzania Bara nako mara hii kulikuwa kumeimarika kwa chama chetu kuwa mbele kwa utetezi wa demokrasia inayovurugwa na chama tawala na dola yake.  Kwa vyovyote vile, mtu hawezi kujenga imani kulazimisha chochote katika mfumo unaotoa fursa kwa watu kuamua wapendalo.  Ndio maana katika kumjengea imani mgombea wake, Rais Mkapa hakupata njia isipokuwa kulazimisha kama alivyolazimisha ushindi.  Mauwaji haya hatuyakumbushi kwa nia ya kuandika historia ya matukio tu, lakini kumbukumbu hii ni pamoja na tangazo la kuyalaani kwa nguvu zetu zote.  Hata katika enzi ya ukiritimba wa chama kimoja, bado bunduki haikuwahi kuitumiwa “hadhiri nadhiri” kuua raia kama ilivyokuwa Januari 26 na 27.  Aidha, haikufikapo Serikali kutumia majeshi ya nchi kutesa na kunajisi raia hata Watanzania wakahiari hifadhi ya ukimbizi kwa makundi kuliko nchi yao inayojulikana ulimwenguni kwa utulivu.

Haya ndiyo yaliyojiri chini ya utawala wa Rais Benjamin William Mkapa, ‘Bwana Msafi’.  Wakati mauaji yanatokea Rais Mkapa alikuwa nje ya nchi kwenye ziara.  Aliachia madaraka yake yashikwe kwa muda na Makamp wake, Dr. Omar Juma.  Hatukujua iwapo ukimwacia Urais mwenza, pia unamwachia na Uamiri Jeshi, lakini angalau twajua kwamba dola hua chini ya anaeachiwa madaraka.  Mauaji yalitokea wakati Dr. Omar akiwa kazini na leo “sisi sote tuna msiba kwa roho za ndugu zetu na wake waliopotea”.  Tulidhani CCM itakaa na kutoa kauli ya kukubali jukumu na kuwafariji waliobakia miongoni mwa wafiwa, vizuka na mayatima.  Hata hivyo, kubwa tuliloambiwa ni kwamba tulistahili kufa kwa kuwa hatukutii amri halali.  Watawala na baadhi ya Wanafalsafa wa Tanzania Bara, wao wanasema kwa kisingizio cha historia kuwa ni kitendo cha marudia kwa Wazanzibari kufa kwa makundi baada ya chaguzi.

7.2.2    Alkhamis tarehe 25 Januari, 2001 Dar es salaam

Kabla ya siku ya maandamano kufika, itakumbukwa kuwa Serikali ilizuia mkutano uliokuwa uhutubiwe na Mbunge wa CUF wa Jimbo la Kigamboni Mhe. Frank Magoba uliokuwa ufanyike tarehe 25 Januari, 2001, Polisi walitoa taarifa ya ghafla kuzuia mkutano huo.  Wananchi walikuwa wamefika kwa wingi kwenye eneo la mkutano na hata Mwenyekiti wetu wa Taifa Mhe. Lipumba nae pia alikwishawasili akiwa kama mgeni mwalikwa wa mkutano huo.  Baada tu ya kuwasili hapo aliona bora kuahirisha mkutano na kuwataka watu waondoke na warejee majumbani.  Ijulikane tu kuwa taarifa ya Mwenyekiti ilikuwa ni kuahirisha na sio kuvunja mkutano ule, na alifanya hivyo kwa kuwa watu wengi walikwisha ondoka.  Siku za nyuma iwapo kulikuwa na matatizo ya usalama baada ya sisi kupeleka taarifa yeu, Polisi walikuwa wakiwasiliana nasi na kutuomba tuahirishe na tupange siku nyengine.  Siku zote tulikubaliana na mashirikiano kama haya.  Katika mkasa huu, Polisi walitupillia mbali utaratibu wao wa kiungwana na wakahiari „kufanya uharibifu katika ardhi“.

Wakati wanarajea majumbani , Polisi walisimamisha msafara wa Mhe. Mwenyekiti, Mbunge na baadhi ya viongozi wetu wa kitaifa na kuteremshakwenye magari yao.  Polisi wetu, bila ya kuwauliza „kala wa la kalamu“ walianza kuwashambulia kwa marungu na watu wengi wakijeruhiwa vibaya sana.  Kitendo hiki kilifanywa na Polisi wa FFU wlaiokuwa wakiongozwa na Afisa aitwae Afande Toss na kwa kweli, mtu mmoja ambae alijeruhiwa kupita kiasi alifariki siku ya tatu yeke katika Hospitali ya Muhimbili.  Kwa jiji la Dar es salaam si rahisi hata kidogo kumtambua majeruhi mara moja katika kizaa zaa kama kile walichokisababisha walinzi wetu wa usalalma wa raia.  Baada ya mkong’oto wa kishindo viongozi wengine (akiwemo Mwenyekiti wa Taifa), Prof. Lipumba walikamatwa na kupelekwa rumande hapo Police Central wakiwa pamoja na wananchi wengine ambapo sasa jumla yao ikiwa ni zaidi ya hamsini.

Polisi baadae waliwapeleka Mahakamani suku ya Jumatatu tarehe 29 Januari, 2001.  Kitu kimoja kinajieleza.  Polisi hawa hawa wanaongozwa na Mahita mmoja na Sheria moja walichuwa hatua na kuwapelwka mahakamani mapema kidogo ikilinganishwa na Zanzibar ambako mtu humpelekwa rumande wastani wa wiki siku kabla ya kufunguliwa mashtaka.  Hatusemo kwamba siku 3 kukaa ndani bila hatia ni vizuri, lakini inaonesha namna sheria moja inavyotumika kwa kuwahudumia watu wamoja katika Tanzania moja.  Hatimae, ili kupunguza idadi ya washitakiwa katika kesi ambayo Serikali haikuwa na hamu nayo, basi Polisi walianza kuwaachilia baadhi ya mahabusu kinyemela bila ya kuwapeleka mahakamani.

Ukiachilia mbali wale wananchi waliokamatwa na kuachiliwa kinyemela siku ya pili yake na ambao hatukuweza kupata majina yao, viongozi na baadhi ya wanachama wafuatao ndio waliokamatwa na kufikishwa mahakamani:

Jadweli Na. 1: waliokamatwa na kufikishwa Mahakamani

S/No.

JINA

WADHIFA

PAHALA

1

Prof. Ibrahim H. Lipumba

Mwenyekiti Taifa

Sinza

2

Ernest J. Lyanga

Naibu Mkurugenzi

Ilala

3

Annia Said Chaurembo

Naibu Mkurugenzi wa Fedha

Kariakoo

4

Shaban Ngozi

Afisa Mipango na uendeshaji

Vingunguti

5

Hussein Ali Alawi

Dereva

Buguruni

6

Hussein H. Iddi

Mlinzi

Buguruni

7

Ali Shaali

Afisa Mnadhimu

Magomeni

8

Yussuf M. Karama

Mpiga Picha (camera man)

Temeke

9

Abuu baker Rakesh

Mwanachama

Magomeni

10

Salum Said Kikugio

Mwanachama

Tandika

11

Kassim Said

Mwanachama

Mbagala

12

Khamis Mohammed

Mlinzi

Tandale

13

Frank G. Magoba

Mbunge

Kigamboni

14

Fred Kabisama

Kaimu Katibu wa Wilaya

Ilala Vingunguti

15

Swaleh Sudi Ally

Mwanachama

Buguruni

16

Mussa Rashid

Mwanachama

Buguruni

17

Omary Ally

Mwanachama

Buguruni

  • Waliomia na kupata matibabu

Jadweii Na.2: Walioumia na kupata matibabu

S/No

Jina

Walivyoumia

1

Prof. Ibrahim H. Lipumba

Mkono wa Kulia na kuibiwa saa na Polisi

2

Ernest J. Lyanga

Kichwani (ngeo)

3

Hussein Ali Alawi

Miguu

4

Hussein Hamad Iddi

Miguu

5

Yussuf Mohammed Karama

6

Abuubakar Rakesh

Kichwani (ngeu)

7

Salum Said Kikugio

Kuvunjika mkono wa kulia

8

Kassim Swedi Kitunda

Alivunjika mguu wa kulia

9

Khamis Mohammed

Kichwani na mguuni

10

Fred Kabisama

Aliumizwa kichwani

11

Omary Ally

Aliumizwa kichwani

12

Shaban Shomari

Aliumizwa miguuni

Chanzo: Kurugenzi ya Mipango (CUF – Ofisi Kuu DSM)

*          Angalia: Abubakar Rakesh sasa ndie Mkurugenzi wa vijana    na Haki za Binaadamu, Taifa

7.2.3    Ijumaa Tarehe 26 Januari, 2001

Wakati tumeshapeleka barua zetu kungojea majibu ya Polisi wa kila wilaya, wote walijibu, tena kwa lugha inayofanana kwamba, walipiga marufuku maandamano yetu ya amani.  Vyombo vya habari baadae vilianza kunguruma kwamba maandamano yalipigwa marufuku.  Vyombo vya habari vya Dola (hasa sauti Tanzania Zanzibar) navyo vilitapika vitisho, na kejeli iliyoongeza mori na munkari kwa askari ili wafanye unyama wao iwapo tungekhalifu amri.  Sio kwamba vilisema kwa sauti ya kukhofisha watu, lakini vilisema kwa kushonganiza.  Sisi kuhusu hili la kuuliwa ovyo, hatukufikiria kwamba askari wangekuwa na ukatili wote na wakalitekeleza.  Hatukwenda kwenye vita sisi tulikuwa kwenye mstari wa uhuru wa maoni ambao ni msingi wa Katiba yetu.  Hatukutarajia hata kupigwa marungu, ingawa huu ndio mtindo wao kwetu sisi, iwe tuna kosa au la.  Ama kwa wakati ule Sauti ya Tanzania Zanzibar ndio iliyotia fora kwa kazi chafu, kama vile Radio Intarahamwe ilivyoshonganiza mauaji ya Rwanda na Burundi.  Hadi tunaandika kitabu hiki, ikiwa leo ni miaka mitatu baada ya mauaji na miaka miwili baada ya muafaka, bado vyombo vya habari vya Serikali havijabadilika hata shubiri katika majukumu yao ya kudhoofisha demokrasia nchini.  Hii ndio maana tukisema mazingira ya mateso na mauaji bado yapo huwa tunatumia vigezo kama hivyo na ingawa mifano yake iko mingi, lakini vyombo vya habari vya Serikali ndio vinavyoongoza kwa kuvizisha demokrasia.

Kwa hivyo basi, vitisho hivyo vya dola na vyombo vya habari vilianza mapema wiki nzima kabla ya siku ya mauaji.  Huku vyombo vya habari vikitoa matangazo, Polisi walianza kumiminwa na wengi wao wakitokea Tanzania Bara.  Silaha nzito nzito zilielekezwa Unguja na Pemba.  Huku askari wakiivamia miji mikuu ya Tanzania, bosi wao Mkuu Alhaj Omar Mahita, alijitutumua kwa kauli ya dhihaka akasema iwapo „CUF wao ni ngangari basi Polisi ni Ngunguri“.  Ngangari kwa CUF si chengine isipokuwa ni ukakamavu na mtu anaweza kujiuliza basi ilikuwaje Polisi wageuze taswira na maana ya bango lenye usemi wetu huu kiasi cha kufikia uamuzi wa kutekeleza sheria wakiwa na kasumba za kiitikadi za chama tawala?  Alipokuwa akimpigia kampeni Dr. Salmin, Rais Mstaafu Mwinyi, alikuwa akimnadi Mgombea Mwenza wa CCM, Dr. Omar kwamba yeye ni „Chinja chinja“, lakini Polisi hawakutoa tafsiri kwamba yeye alikuwa anahubiri hatari na mauaji.  Iweje leo basi, Mahita aitafsiri kauli ya CUF aiwache ile yenye maana  ya wazi wazi ya Mwinyii.  Sisi tulielewa kwamba pengine mafuta ya madaraka yalikuwa hayajakolea, kwani wakati ule kulikuwa na ustaarabu mwengine katika Jeshi la Polisi chini ya IGP Mahundi.

Kama utamaduni wa kazi wakati wa Ispector General Mahundi ungekuwa wa kuua kama wa mrithi wake mahita, basi alikuwa na nafasi na uwezekano mkubwa zaidi wa kuua.  Katika kipindi kile mfumo wa vyama vingi ndio kwanza ulikuwa unaingia nchini na kila mmoja aliupokea kwa namna ya ufahamu wake.  Hii ni tafauti na miaka mitano baadae ambapo watu walianza kuufahamu kwa mtazamo wa aina moja.  Wakati ule Polisi hawakuwahi kabisa kutiwa kasumba wazi wazi hata wakapoteza imani kwa ndugu zao na kuua ovyo.  Hivyo, hawakufurutu asa wakaua kama walivyofanya wakati wa Mahita.  Wengine wanadhani,pengine kwa kuwa Mwalim alikuwa hai, yawezekana ndio sababu wauaji walificha makucha yao.  Kumbe hatukujua kwamba warithi wake walikuwa wanaomba Mungu aondoke haraka ili wadhihirishe yaliyomo vifuani mwao.

Kabla ya mauaji wakubwa wa nchi walifanya kazi kubwa kusaidia mauaji yatekelezeke.  Tuna mifano ya kauli za uchochezi zilizotolewa na viongozi wakuu wa CCM kutoka pande zote za Muungano.  Mfano wa kauli hizi ni kama zifuatazo:

Ndugu Mohammed Seif Khatib, Waziri wa Mambo ya ndani wa Tanzania alifanya ziara Zanzibar na kutoa maelekezo kwa Polisi na kama kawaida yao, kukutana na viongozi wa Chama Tawala na Serikali kuweka mikakati yao sawa.

Ndugu Fredric Sumaye, Waziri Mkuu wa Tanzania naye kama kawaida yake alitoa kauli katika Bunge mjini Dodoma, sio tu ya vitisho lakini pia ya kuwamkinisha askari kwa kazi ya kuua ambayo Kamati yao ya Ulinzi na Usalama ilikwisha kaa na kuithibitisha kauli yake.  Kikao hicho kiliitisha na Makamo wa Rais, Dr. Omar Ali Juma ambae kupitia kikao hicho alitoa onyo kali la kutaka maandamano hayo na mikutano isifanyike.

Kauli nyengine kwa utngo zilikuwa zikitolewa na Wakuu wa Mikoa, Wilaya na Makamanda wa Polisi katika sehemu zao.  Wanasiasa wa Chama tawala pia nao hawakuwa nyuma kutoa maoni yao ambayo yalizidi kuwaunga mkono Polisi wafanye ambayo wengi wa wanachama hawajayaona katika  uhai wao na uzoefu wa kisiasa.

Ushahidi huu ni tosha kwamba majeshi yetu yalitayarishwa kivita na sio kuzuia fujo.  Ni bahati mbaya sisi hatukuwa na kikosi wala silaha na ndio maana hata pale Serikali walipotoa takwimu ya waliokufa basi walisema, walipoteza askari mmoja aliechinjwa kwa kisu.  Miaka ya nyuma majeshi ya CCM yaliwahi kuuchakaza mji mzima wa Shengejuu eti kwa shutma kwamba wananchi wa hapo walikuwa na silaha waliyomnyang’anya askari.  Kama hii lingekuwa kweli, basi huyo askari mmoja wanaesingizia kuuliwa na CUF asingekufa kwa kuchinja kwa kisu.

Baada ya kutolewa kauli za kuzuia maandamano ambazo zote zilikusudiwa kubinya demokrasia pamoja na kwamba zilikuwa ziko kinyume na Sheria na Katiba ya Nchi, kiburi cha Polisi kilizidi na kauli za Wakubwa wa Jeshi la Polisi zilianza kutolewa kwa nguvu na kuashiria kwamba ni Askari wenyewe ndio waliotayarishwa kuanzisha vurugu siku hiyo ya Januari 27, 2001.  Hata hivyo, juu ya vitisho vyote, wana CUF wa Tanzania nzima waliendelea na maandalizi ya maandamano na mikutano ya hadhara tu, siku hiyo ya Januari 27, na katu haikukusudiwa jambo jengine.

Wakati tunasubiri kwa hamu maandamano yetu, mara tulisikia kwamba Mheshimiwa Juma Othman Juma ambar ni Katibu wetu wa Kamati ya Ulinzi na Usalama alikamatwa na kuwekwa rumande.  Unguja, Mheshimiwa Muhammed Ali Yussuf, Mkurugenzi wa Mambo ya Nje nae alikamatwa usiku wa manane siku ya Alhamis tarehe 25 Januari.  Yeye pamoja na viongozi wengine wakuu, Mheshimiwa Ali Haji Pandu na Dk. Maulid Makame Abdalla ambao walikamatwa siku iliyofuata, wote waliwekwa rumande kitu cha Mwembe Madema kwa muda wa zaidi ya wiki mbili na baadae kupelekwa mahakamani kuanza utaratibu mwengine mrefu wa sheria za kimapinduzi.  Mtindo huu wa kukamata watu usiku ni hatua iliyochukuliwa kwa raia siku za harakati za Mapinduzi tu, lakini zilirejea tena mwaka 2000.  hatukushangaa kwani tuliambiwa Amani atakwenda hakukutuvunja moyo, tuliendelea tu na mipango yetu huku tukisubiri Jumamosi kwa hamu.  Masikini , kumbe tulishatayarishiwa karamu ya misiba.

Hata hivyo, Polisi hawakusubiri Jumamosi ifike kwani ilipofika Ijumaa ya 26 januari, 2001 mauaji yalianza.  Ijumaa kwa Waislamu ni Siku Kuu ya Ibada.  Ilikuwa ni majira ya saa saba na nusu mchana siku hiyo, ndio kwanza Waislamu wanamaliza sala zao misikitini.  Misikiti mingine ilikuwa imeshamaliza kusali na watu wako milangoni wakitakiana kheri na kuagana.  Bila shaka wengine walikuwa njiani tayari wakielekea majumbani kwani misikiti mingine hutangulia kusali kidogo.  Siku hiyo haikuwa ya maandamano kabisa, maana maandamano yalipangwa siku ya pili yake, tena barua zetu kwa Polisi zilionesha hivyo.

Siku ya Alhamis ya tarehe 25 Januari, 2001, Dr. Omar alihutubia Taifa kupitia vyombo vya habari akisema haya „…… hawa CUF ndugu zanguni hamuwajui nyie, ni wajanja sana hawa, na kwa vile wamesema watafanya maandamano siku ya Jumamosi, yawezekana wakafanya Ijumaa hawa“.  Wengi hadi leo tunajiuliza kwanini aseme moja kwa moja maelezo ambayo hayawezi kuthibitishwa na ushahidi wa aina yoyote!  Lakini hapana la ajabu sana na wala mtu hapaswi kushangaa sana kwani hapa ndipo tulipopata jibu kwa nini CCM walikuwa wakipakaza kuwa CUF ni chama cha Waislamu.  Yawezekana basi, kwa kuwa sasa wamepitisha sheria za kigaidi, siku moja wakataka kuifanyia kazi, na bila sha, kwa mantiki hiyo basi, kazi ya kwanza huenda itaelekezwa kwenye chama chetu.  Ndio maana tukasema mazingira ya kuua Watanzania bado yapo na kila uchao yanaimarishwa.

Tunasema hivi kwa sababu hapo nyuma, hata kabla ya sheria hii kutungwa, tayari CCM kwa kutumia vyombo vyake na vyama vyake tegemezi walitoa kauli kwamba CUF ni chama cha magaidi.  Hizi zilikuwa ni shutma nzito kuwasakamizia wanasiasa wenzako.  Yawezekana walifanya hivyo ili Watanzania watuogope na wao ‚waendelee kula nchi na kuwaletea wananchi maendeleo ya umaskini’.  Hata hivyo, hili tuna wasi wasi nalo kuwa ndio lilikuwa lengo, kwani tulitangazwa kuwa sisi ni magaidi hata kabla tafsiri na sheria ya ugaidi kutungwa.  Si hasha basi siku moja CCM wakatuhukumu hata kabla hatujafanya huo ugaidi waliotubebesha mgongoni.  Wanafanya hivyo il kuficha makucha yao yalioroa damu ili wajipendekeze kwa vyenye kuleta maafa kwa raia katika Afrika.  Diplomasia inageuzwa rushwa ili kutengeneza tawala zenye madhambi kwa raia.  Hatujui iwapo kweli ulimwengu waungana au wamong’onyoka.

Tukirejea habari za siku ya Ijumaa ni kwamba, majira ya kama saa nane kasorobo za mchana hivi, waumini wa dini ya kiislamu walikuwa ndio kwanza wanamalizia sala ya Ijumaa hapo katika Msikiti wa Mwembe Tanga.  Msikiti huo uko ubavuni tu mwa ofisi ya CUF wilaya ya mjini.  Wakati huo watu walikuwa wamechanganyika changanyika kwa kusalimiana na kutakiana kheri ya Ijumaa na kuagana karibu na msikiti wao.  Mara Polisi waliokuwa na silaha walifika ghafla na kuvamia kikundi kile cha waislamu.  Kikosi kile kilikuwa kinaongozwa na Ofisa wa Polisi kwa jina la Mahmoud Juma, maarufu hapa Unguja kwa jina la Mrema.  Watu walipowaona kundi hilo la Polisi wakiwa na silaha katika hali ya tahadhari walianza kufadhaika.  Ofisi yetu ya wila ilifungwa kwani tulijua pale ndio palipokusudiwa, lakini haikuwa hivyo.  Na kwa nini wakusudie wilaya wakati Makao Makuu iko karibu mita 200 tu kutoka pale!  Naam; hawakuwa na haja ya Makao Makuu wala ya Ofisi ya Wilaya na kwa hivyo hawakuwa na haja ya siasa siku hiyo.  Walikuwa na haja ya msikiti kama ilivyokuwa siku ya Mwembechai.

Hali hii ya mfadhaiko ilimshitua kila mtu na tukajua sasa ndio kishindo cha ushindi kinaaza.  Mara kufumba na kufumbua tukasikia amri kutoka kwa Mrema ikisema ‚shoot’ na punde amri ikapokewa kwa kumfayatulia mtu mmoja risasi.  Hadi leo twajiuliza hivyo ndie waliemkusudia kweli!  Maana huyu alieandguka na kufariki pale pale alikuwa ndie Imamu wa msikiti ule wa Mwembetanga.  Kwa Askari kama Mrema ndio maana hadi leo anatanua kama vile aliua tumbili tu; kwani kama ingekuwa mwnye vita ukifanikiwa kuua kamanda huwa umefanya kazi nzuri.  Ndio hivyo hivyo basi, kumuua Imam msikitini Mrema alistahili aliyopewa baada ya kitendo kile.  Imam walietunga na kumtungua na kumuua Mwanazuoni chipukizi Ustadh Juma Khmais Mohammed akiwa katika umri wa miaka 30 akiacha kizuka na familia kubwa iliyomtegemea, lakin  bila ya mtoto wa kuzaa.  Ndio mwanzo alianza kufunga ndoa jamani.  Maskini Mrema alimkata roho kufumba na kufumbua, na kufungua na baadae akarudi kwake akafura mikono damu akakaa kitako na familia yake akicheka.  Famlia ya mwenziwe ikilia na sasa inahangaika.  Ustadha Juma hakuwahi hata siku moja kuwa kiongozi wa chama chetu, lakini yawezekana kabisa alikuwa mwanacham wetu.  Na kwani kuna kosa gani? Au ndio hukumu ya kuchanganya dini na siasa inayokatazwa sana na CCM?  Haijulikani kama Ustaadh Juma aliuliwa kama mwana CUF aliekuwa karibu na Ofisi ya wilaya au walimuua kama Kiongozi wa Waislamu aliekuwa karibu na Msikiti.  CCM ndio wanaojua zaid na siku moja wataulizwa.

Kama hii haitoshi mara risasi nyengine kama mvua zikamwagwa kundini mwa watu waliokuwa wakikimbia.  Mara hii ilikuwa zamu ya Ustadh Seif Juma Said.  Huyu alianguka na kuzimia na wakadhani amekwisha.  Baadae alizinduka lakini kumbe risasi iliathiri sana mguu wake, na ilibidi akatwe.  Ni kiwete sasa, angalau yeye ana uwezo wa kumuona Mrema bado, Juma hamuoni tena Mrema ingawa kesho wataonana.  Risasi zile zilizomiminwa kama mvua katika kundi la watu ambao walikuwa wako mbioni kujisalimisha ziliangusha na kujeruhi vibaya watu wengi.  Salama iwapi tena, watu walianguka na kuwa majeruhi na wengine hadi leo ni vilema.  „Kila kitu ni cha Mungu, na kila kitu kitarejea kwake“.  Ama inaonesha kama vile waliambiwa waje waue msikitini na zaidi wamuuw Imam, kwani baada ya hapo Mrema na kikosi chake walielekea msikiti wa Mchangani na Mbuyuni.  Kama  walikuwa wakitafuta maimamu, basi bila shaka walikuwa wakiwatafuta akina Sheikh Aliani.  Lakini hakumkuta.  Zake zikeeko.  Kwa kawaida Mchangani wao saa saba huwa hawapo tena.

Punde tukasikia mlio mzito wa bunduki.  Wakatupita vijana wakihema kwa mbio.  Hawauliziki lakini baadae tukapata habari kuwa Mrema kachomoka kumwaga damu.  Hapa tukapata habari kuwa mti mmoja aitwa Hamad Said nae alitunguliwa na kufa hapo hapo.  Tukauliza ni mwanachama wa tawi gani, lakin vijana wakatujibu kwamba huyu ni mwanachama mkereketwa wa CCM.  Kwa yoyote „mwenye macho“ na anaetaka kujua ukweli sasa ataamini kwamba siku ile watu kwa misingi ya kisiasa bali walikusudiwa kuuliwa watu kwa misingi ya Uzanzibari, na kwa kuwa yalifanywa misikitini basi ni nani atakaebisha kuwa pia yawezekana mauaji yalifanyika pia kwa misingi ya Uislamu.  Ndio maana ya CCM kupandikiza chuki ndani na nje ya Tanzania kuwa CUF ni chama cha Waislamu, na kwa hivyo wakitaka kuishughulikia CUF kwanza huwenda misikitini.

Haya yakitokea chini, huko juu ya anga basi Bwana Mahita yuko na Helkopta kuangallia kama kazi yake ilikwenda vizuri.  Tuna kumbukumbu kwamba helkopta hizi zililetwa kutoka Afrika ya Kusini na zilizinduliwa kwa kuwashughulikia Waislamu Mwembechai.  Kazi ya pili ilikuwa kuwashughulikia Waislamu Mwembetanga, hatujui  jamani kazi ya tatu itakuwa Mwembe upi.  Lakini haya twende, tutafika.  Mtu atashangaa, tokea helkopta hzi kuja hapa nchini, jahazi nyingi zimezama zikitokea Tanga (kwao Omar Mahita) kuelekea Pemba (Kwao Dk. Omar) na kupoteza maisha ya mamia ya watu, lakini hatujaziona wala kusikia kwenye vyombo vya habari kwamba zimejihusisha kutoa msaada wa kuokoa maisha ya wale ndugu zao wa damu.  Si kwa sababu nyengine, ile kwa kuwa ni Wapemba, na ni wakorofi kwa kuwa wamesimama kidete kupinga udhalimu wa CCM kwa Watanzania walio wengi.  Ndio amani na utulivu hii, ndio umoja wa mshikamano.  Ndio udugu wa damu huu wa wenzetu, na si wote, lakini CCM

Matukio haya ya Ijumaa kabla ya siku ya maandamano yalitendwa na Polisi huku sababu za msingi wakizijua wao wenyewe.  Ina mahusiano gani mikusanyiko ya ibada ya dini ya Kiislam na chama cha CUF?  Ndio dhana za CCM, kwa kuwa wamesema CUF ni chama cha Kiislam na kwa sababu Uislamu ni kero kwa CCM na Serikali zake, basi naam, yachukuliwa kwamba ukiwa Muislamu ndio eti utakuwa ni CUF, na kwa hivyo ukiua Waislamu basi ndio umeua CUF, na ndio hivyo hivyo wema hautendwi kwenye Waislamu wengi kwani kwa dhana yao, ukiwatendea wema Waislam utakuwa umeitendea CUF.  Hii ndio hisia iliyojengeka kwa wenzetu na si hisi tena lakini ni mkakati unaofanyiwa kazi.  Mkakati huu siyo tu kwamba unashadidiwa na watawala wa CCM lakini pia hushereheshwa na baadhi ya wasomi wao.  Tanzania hakuna magomvi ya kidini kwani pamoja na Serikali kuwaelekeza watu katika mkondo wa misuguano ya kidini, lakini Watanzania wanazidi kuvumiliana kwa masuala haya.  Twamuomba Mungu azidi kutuepusha nayo, lakini pia atuepushw na wale watutatkiao kadhia hio.

Baada ya kumaliza kuwashughulikia Waislamu kwenye ibada yao, sasa ndio walianza kuwashughulikia Watanzania kama wana CUF.  Na tunataka ieleweke hivyo kwamba shughuli ya Ijumaa ilikuwa tafauti tena sana na shughuli iliyofuatia.  Mauaji ya Mwembetanga na Mbuyuni hayana uhusiano wowotena siasa na kwa maana hiyo, mauaji ya wanachama wa CUF yaliyotokea baada ya siku hiyo.  Hata hivyo, sisi kama chama kinachopigania haki za binaadamu yanatugusa sana mauaji haya, na kwa hivyo ni misiba yetu ya kuhuzunisha kweli kweli.  Hivi ndio sahihi kwani katika misikiti huwa hatajwi Lipumba  wala Seif.  Anaetajwa mule mara nyingi kwa baadhi ya misikiti ni Sheikh Amani Abeid Amani Karume, ili apate maisha bora na fadhila za Ijumaa.  Ndivyo baadhi ya Masheikh wanavyoamini.  Na pengine yawezekana basi, kwa kuwa Mwembetanga hawana utaratibu wa kumtaja kiongozi, hii pekee yaweza kuwa ndio sababu ya kukumbushwa.  Tunazidi kutoa ushahidi kwamba Ustaadh Juma na wenziwe walipotezewa maisha kwa sababu ya Uislamu na sio kwa sababu ya uwanachama wao wa CUF.  Mungu awalaze peponi.

Kwa hivyo, kuanzia hapo askari Polisi waliendelea  kuwakamata viongozi wa juu wa Taifa na wa Wilaya ya Mjini na kuwaweka rumande.  Tulifikiri iwapo Polisi walikuwa wakiuwa CUF, basi na hawa wasingerudi rumande.  Huu ni ushahidi mwengine kuwa mauaji ya Ijumaa ya kabla ya maandamano, hayakukusudiwa CUF.  Baadhi ya viongozi aliokamatwa mkesha wa tarehe 27 ni viongozi wa Taifa na wa Ofisi ya wilaya.  Baadhi yao ni: Mhe. Mohammed Iddi Makame (Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa), Mhe. Masoud Khamis (Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa na Wanawake wilaya ya Mjini), Mhe, Fat –hiya Zahran (Mjumbe wa Mkutano Mkuu Taifa), Mhe, Mohammed Ali Shamte (Mwandishi wa Kamati Tendaji), Mhe. Zahor Tamal (Ofisi katika Kurugenzi ya Mpiango) na Mhe. Fatma Said (Sekreteri wa Ofisi ya Wilaya ua Mjini).  Hawa,, tunasema ndio waliochukuliwa na kuwekwa ndani kwa imani zao kama wanaCUF na yawezekana ilifanywa hivyo ili kupunguza nguzu za maandamano ya tarehe 27 Januari, 2004.

Ama kuanzia hapo tena hali ya nchi ilivurugika na Polisi hawakuwa wakiongozwa tena na sheria kama vile bosi wao walivyoacha hekima na busra na badala yake kuongozwa na kibri na jabza.  Kamata kamata na kupiga watu ovyo ilikuwa ndio hali iliyotawala miji yote Tanzania.  Wakati wote huu tulikuwa Makao Makuu, Mtendeni kupotea habari kutoka kila pembe ya nchi.  Ole wako, uwe na rangi nyeupe kidogo au ndevu.  Ukiweza kuvutwa kama vile mkulima anavyonyoa mahindi mabichi.  Haikuwa bahati mbaya hii, ndio kukumbushia ya 1964, ndio maana ya Mapinduzi Daima; ndio namna ya kudumisha ushindi wa kishindo na ndio kuwajengea heshima na kuwaenzi Mzee Karume na Mwalim Nyerere.  Lakini si tuliambiwa?  Ndugu Amani, huyu ndie mwenzetu, ni mwenetu, atakwenda mwendo kama wa babaake.  Sadakta, kwani baada ya mwezi mmoja tu wa kuingizwa madarakani mauaji haya yalikuja kuthibitisha maneno ya mpiga debe wake maana hata babaake ndivyo alivyo anzia.  Kwa kifupi sana hivyo ndivyo ilivyokuwa kabla ya siku ya maandamano

Sehemu ya 3: Maandamano ya Amani Januari 27,2001

7.3.1    Maandamano Dar es Salaam

Serikali hii haina washauri wazuri, na CCM nayo, kwa kuwa maamuzi yao hata yawe ya kisiasa, lazima kwanza yapate baraka ya vyombo vya dola basi mara nyingi dola ndio inayoanza kuvurunda.  Na kwa sababu rushwa ya vyombo vya dola hutegemea kwa kiasi kikubwa wingi na uzito wa fitna, basi vyombo hivyo vya dola hutaka kuhakikisha kwamba kile walichoshauri kwa Serikali kinatokea vile vile.  Hii ni kusema, ikiwa wametia fitna kwamba maandamano yatakuwa na fujo, basi ni lazima kila kitu kitafana lakini fujo itokee.  Ndio maana mara nyingi wamekuwa wakiwashauri CCM wasishughulike kwani CUF ni mali ya Lipumba, Mloo na Seif.  Na ndio vivyo hivyo walipowashauri kwamba wakikamatwa viongozi wakuu wa CUF na kufunguliwa kesi ya uhaini basi CUF nayo itamalizika.  Walisahau kwamba ikiwa CCM ina wenyewe, CUF ni Chama cha Wananchi.

Ilikuwa asuhubi mapema Januari 27 kama tulivyopanga, wananchi wa jiji  kuu la Dar es Salaam walimiminika kwa wingi katika sehemu tulizopanga maandamano yafanyie.  Tatizo tulilolipata pale ni kwamba mgeni rasmi alikuwa awe Mwenyekiti wetu Profesa Lipumba, lakini ndio bado alikuwa rumande anashikiliwa tokea siku ile ya Alhamis.  Pamoja na yeye, viongozi wetu wengi walikuwa bado wako rumande.  Ingawa kuwakosa viongozi hawa kulikusudiwa kushusha ule msisimko na hamasa lakini hali haikuwa hivyo.  Wanachama waliongeza kasi ya ungangari na maandamano yalifana sana.  Wananchi waliweza kufika kwa wingi katika viwanja vya Kidongo Chekundu ambapo tulipaamua kabla.

Baadae ya kufika kule Kidongo Chekundu, Polisi wa FFU wakiwa na vifaa vyote vizito vya kuzuia fujo na kuua walifika na kuanza kumpiga kila mtu aliyeonekana kwenye eneo hilo na katika barabara iliyokaribu na hapo.  Hii haikuwa kuzuia fujo, kabisa.  Katika vurumai hiyo jumla ya 99 walikamatwa.  Baadae wengine waliachiwa lakini wengine 40, akiwemo mwanamke mmoja aliyekuwa mgombea Udiwani katika kata ya Upanga Magharibi walifikishwa mahakamani.  Orodha kamili ya waliofikishwa mahakamani ni kama hii hapa chini.

Jadweli No. 3: Waliokamatwa na Kufikishwa mahakamani Dar

S/No.

JINA

ATHARI

MAELEZO

1.

Hamza Lema

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Rukia Moh’d Ali

Kipogo na kupoteza fahamu

Shitaka la kuandamana

1.

Salim Said Kibwena

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Coolnine Yahya

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Said Hassan

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Ramadhan Amran Moh’d

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Frank Martin Raphael

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Twalib Abdalla

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Mrisho Juma Upatu

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

James Ali

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Mussa Mwinyijuma Kishashu

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Athuman Juma

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Waziri Juma Kijembe

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Salum Rashid Kipara

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Nassor Suleiman Chambuso

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Shokate Suleiman

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Omary Ali

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Hussein Juma Kidesu

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Moh’d Abdalla Ali

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Jumanne Membe

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Suleiman Salum

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Abdul Shaaban

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Rajab Phillemon

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Kiasi Mtipa

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Said Alisi

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Wilson Francis

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Ramadhan Kaziba

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Yussuf Abdalla

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Juma Yahya Kijazi

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Jarome Dioniz Mishi

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Madarizir Rajamula

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Waziri Mhina

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Abdalla Halfan Hamad

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Mussa Hamad Mtani

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Philipo Joseph

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Moh’d Shomari Pazi

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Rwebangira Kataraia Cleofasi

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Kazembe Rashid

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Nassor Ramadhan

Kipigo

Shitaka la kuandamana

1.

Hassan Kiswagale

Kipigo

Shitaka la kuandamana

Wakati huo huo, tulipokea taarifa kuwa yule kijana aliepigwa siku ya tarehe 25 Januari alikuwa akiitwa Jaffar Said na alifariki siku hiyo ya tarehe 27 Januari, 2001 na kuzikwa kijijini kwao Tanga.

7.3.2    Maandamano ya Tanga

Maandamano yalifanyika katika Mkoa wa Tanga.  Halikadhalika, mamia ya wananchi walihudhuria na kushambuliwa na Polisi.  Baada ya kipigo hicho,, wengine walikamatwa na kuwekwa rumande kabla ya kufikishwa mahakamani.  Watu hawa ndio waliokamatwa na kushtakiwa:-

Jadweli No. 4: Waliokamatwa na kushtakiwa Tanga

S/No.

JINA

WADHIFA

MAELEZO

1

Adellastella Mkilindi

Katibu wa wilaya

Shitaka la kuandamana

2

Rashid Jumbe

Mjumbe, Baraza Kuu Taifa alipigwa sana

Alipigwa na kushtakiwa kwa kuandamana

3

Suleiman Muro

Shitaka la kuandamana

4

Moh’d  Khamis

diwani

Shitaka la kuandamana

5

Omar Aden

Shitaka la kuandamana

7.3.3    Maandamano Jimbo la Mwibara

Katika Jimbo la Mwibara taarifa tulizozipata ni kwamba Bwana Laurenti Mayenjwa alipigwa na Polisi hadi kufa.

7.3.4    Maandamano Lindi

Lindi nako kulirindima kwa maandamano, wanachama walihamasika na kuitikia wito wa chama chao.  Viongozi wetu wa wilaya ndio wa kwanza kukamatwa na kushtakiwa.

Jadweli No. 5: Waliokamatwa na kushtakiwa LIndi

S/No.

JINA

WADHIFA

MAELEZO

1

Mhe. Moh’d Mussa Barwan

Mwenyekiti wa CUF wilaya

Shitaka la kuandamana

2

Mhe. Abubakar Twahir

Katibu wa CUF wilaya

Shitaka la kuandamana

7.3.5    Maandamano Bunda

Bunda haikuwa nyuma kwa maandamano.  Huko wanachama walichachamaa na kuhamasika kikweli kweli kama kawaida ya dola, waliwakamata viongozi wetu mashuhuri na kuwapeleka mahakamani.

Jadweli No. 6: Waliokamatwa na kushtakiwa Bunda

S/No.

JINA

WADHIFA

MAELEZO

1

Mhe. Ernest Binna

Katibu wa wilaya

Shitaka la kuandamana

2

Mhe. Manyama Makunja

Mkurugenzi Vijana CUF wilaya

Shitaka la kuandamana

3

Mhe. Kukiko Maginda

Mwanachama

Shitaka la kuandamana

7.3.6    Maandamano wilaya ya Kaskazini B

Wanachama wa Kaskazini B, Unguja nao walijitokeza kuandamana kuunga mkono kauli na wito wa Chama chao.

Jadweli No. 7: Waliokamatwa na kushtakiwa katika maandamano ya wilaya Kakazini B

S/No.

JINA

WADHIFA

MAELEZO

1

Ramadhan Ali

Mwenyekiti wa wilaya

Kuandamana

2

Abdi Salum Ali

Katibu wa wilaya

Kuandamana

3

Ali Haji Ali

Kiongozi

Kuandamana

4

Ali Abdi Ali

Kiongozi

Kuandamana

5

Moh’d Kombo

Kiongozi

kuandamana

7.3.7    Maandamano wilaya ya Kati

Polisi wakiwa na magari ya dereva walifika vijijini na kumkamata Mheshimiwa Ali Khamis Ali ambae alikuwa Kaimu Mkurugenzi wa Mipango na viongozi wengine wa CHama katika wilaya

Viongozi hao waliotajwa walipokamatwa walipelekwa na kufunguliwa kesi katika kituo cha Polisi cha Mahonda.  Kama kawaida ya Polisi wetu, utaratibu wa kisheria wa kimahakama ukavunjwa hali iliyopelekea kupata usumbufu mkubwa hapo kituoni.  Baada ya wiki moja watuhumiwa waliachiliwa bila ya kufunguliwa shitaka lolote.  Ilikusudiwa tu polisi wapitishe ada yao ya kuendeleza uvunjwaji wa Haki za Binadamu kwa kuwakamata watu bila kosa na kuwarundika rumande.

7.3.8    Maandamano Mjini Unguja

Wanachama wetu na wapenzi wakajitokeza kwa wingi sana kuitikia wito wa chama chao na walielekea pale palipotayarishwa kwa kuanzia maandamano.  Kawaida hua tunaanzia kwa Biziredi.  Pamoja na Polisi kuweka udhibiti mkubwa pamoja na vizuizi vingi vya njiani, takriban mji mzima, bado watu walimiminika kama kawaida ya mikutano yetu.  Palikuwa na vikosi vya CCM.  Polisi, FFU, KMKM, Askari Magereza, JKU pamoja na vikosi maalim vya Volantia na Umawa.  Wakiwa na bunduki, mawe na mapanga walikuwa wakiyashambulia makundi ya watu ambao walikuwa wakielekea kwenye maandamano ambai wamejifunga vitambaa vyeupe wakionesha ishara ya amani.  Hata hivyo, hawakujali ishara ile ya kitambaa cheupe na waliendelea kuwasakama wanachama wetu kwa kila aina ya adhabu.

Hapo ndipo vurugu lilipoanzia na vurumai lilikuwa kubwa kwani makundi ya askari yalizidi kumiminika na kutesa kwa zamu kwa mashirikiano mazuri.  Waliwarushia risasi wanachama wetu ambao walikuwa hawana cha kujibu isipokuwa kurudi nyuma na kukimbia.  Baadhi ya njia na maeneo muhimu ya kuelekea Biziredi kama vile Mfereji wa wima baina ya Mwembe mamba na Hospitali ya Utapoa iliopo Mikunguni palikuwa na makundi makubwa ya Polisi waliokuwa wakiwashambulia wa nguvu sana wanachama wetu na katika eneo hilo wanachama wetu wawili walikufa hapo hapo na huku watu wengi walijeruhiwa kwa risasi.  Baadae maiti hizo zilipelekwa Hospitali ya Mnazi mmoja.

Baada ya wanachama wetu kwa maelfu kuona kuwa hujuma hizo zilikuwa zikiongezeka, huku vifo vikianza kutokea na udhibiti wa askari ukizidi wanachama wetu walibadili mwelekeo na kubuni njia za kuyaendeleza maandamano hayo bina ya kupafikia pale ilipoamuliwa awali, yaani kwa Bizeredi.  Maelfu ya wanachama wetu walifanikisha pale walipoandamana katika njia kuu ya Daraja Bovu na kwa huku  mjini wengi wao walijikusanya Mtendeni Makao Makuu ya CUF na kuelekea Darajani ili kwenda katika viwanja vya Mkutano vya Malindi.  Lakini hii pia haikusaidi kwani huku wakiandamana kwa amanni na mabango yenye kuonyesha malalamiko yao, Polisi waliwatawanya waandamanaji wetu kwa risasi za moto na hapo hapo walimuua Mwanachama wetu mmoja kwa kumpiga risasi ya kichwa.  Huyu akiitwa Mwalim Nassor.  Huyo ndie shahidi mkuu kwani ndie alieshikilia bango la maandamano wakati akiuliwa.

Baada ya mwanachama huyu kufa hapo hapo, wengi wengine walijeruhiwa hali ambayo ilileta fadhaa kubwa kwa wananchi walioshiriki katika maandamano na raia wengine wanaoishi maeneo ya karibu.  Huku fadhaa ikizidi, polisi walizidisha risasi za moto na za machozi na idadi ya majeruhi ilikuwa kubwa sana.  Askari walipoona watu wengi walikwisha changanyika walichukuwa hatua ya kupitisha mabomu ya machozi ndani ya majumba.  Walisahau kwamba ndani ya majumba walikuwemo pia watoto wachanga, watoto wadogo, kinamama waja wazito na vikongwe wa kike na wa kiume na wagonjwa wa maradhi mbali mbali.  Na kwa kuwa hujuma za raia zilifanywa hata kwa raia ambao hawakuwa katika maandamano, hili nalo linatoa ushahidi kwamba CCM iliwatumia askari kufanya unyama mkubwa na uvunjaji wa haki za binaadamu kwa raia walio huru katika nchi yao kwa kisingizio tu cha siasa.  Na hapa wengi wanajiuliza, jee hawa ni askari wa Taifa hili hili au ni majeshi ya uvamizi.  Watu wengi waliathirika sana na kupata maumivu makali na afya zao kudhoofishwa na wengi walipoteza nuru ya macho kwa mabomu.  Katika Mkoa wa mjini waliojeruhiwa ni wengi sana kiasi kwamba hatukuandika majina makusudi ili kuepusha kuwaacha baadhi yao.  Tulisikia idadi ya waliojeruhiwa vibaya sana kufikia 3600.  tunawashukuru wote waliofanikisha huduma kwa majeruhi.

Tulikuwa kabla ya hapo tuna kituo cha huduma za Afya chini ya usimamizi wa Dr. Juma Ameir Muchi na wasaidizi wake Bw. Nassor Khalid na madaktari wengine kadhaa.  Wote tuliwashukuru na tunaendelea kuwashukuru sana kwa kutoa msaada usiosahaulika katika maisha ya kisiasa Zanzibar, ingawa kwa ujumla tunaishukuru Kurugenzi nzima ya haki za Binaadamu ya CUF chini ya Mkurugenzi Mheshimiwa Hamad Masoud Hamad na Naibu wake Mhehimiwa Lyanga kwa mashirikiano na kazi nzuri licha ya kutokwa na nyenzo.

Hospitali ya Serikali ya Mnazi mmoja ilizuiwa isihudumie majeruhi.  Tulilazimika kuwapeleka majeruhi lakini hawakuwa wakihudumiwa kwani haukuwa ukatili wa madaktari bali ulikuwa woga wa kupoteza kazi.  Nao tunawashukuru kwani walihisi na mara nyengine kujali shida zetu, lakini dola ilijizatiti kukandamiza hadi mwisho.  Ni vyema tu kufahamu kwamba wakati wote haya yanatendeka wasimamizi wakuu walikuwa ni Jeshi la Polisi na Inspector General Omar Mahita alikuwa juu akiranda na helkopta ya Afrika ya Kusini ili kusaidia kwa maangamizi pale ambapo palikuwa na upinzani.  Kama tulivyosema hatukujitayarisha kwa fujo wala mapambano na kwa hivyo, hatukutoa upinzani wowote.  Kabla ya kuelekea Pemba, sasa tunawauliza wasomaji jee hivi ndivyo ilivyofanywa katika machafuko ya Juni, 1961 chini ya utawala wa madhila wa kifalme?  Jibu, hapana.  Basi ingawa Mkoloni mbaya lakin CCM imekithiri kwa unyanyasaji.

Tukio jengine baya lilitokea katika maandamano ya Mjini Unguja ni  pale askari Polisi walipokwenda katika nyumba ya Bwana Mtumwa Haji Mati wakuvunja mlango na kuingia ndani.  Mule ndani waliwanyanyasa watoto wake na baadae wakampiga Mtumwa hasi akawa taabani.  Hapo wakamchukua hadi rumande wakati anamwagika damu.  Familia yake iliomba apelekwe hospitali, lakin polisi walimzidishia kipigo cha mbwa dume hadi akapoteza fahamu.  Kutokana na hali hii mbaya, Mtumwa alifariki tarehe 16 Februari, 2001.  aliacha vizuka wawili, Amina Khamis na Tatu Mosi pamoja na mayatima kumi na moja.  Haji, Tama, Khamis, Khalfan, Shaib, Awadh, Ibrahim, maryam, Mwanaharusi, Hafsa na Husna.  Kitendo alichofanyiwa Mati hakufanyiwa mtu siku za siasa za ukoloni.

Sehemu ya 4: Maandamano Pemba

Kwa maumbile ya kisiwa cha Pemba kijiografia, ni vigumu kuwashirikisha watu katika maandamano pahala pamoja hasa katika hali isiyokuwa ya kawaida.  Maandamano kwa upande wa Pemba yalipangwa kimikoa iko kuepusha misururu mikubwa ya wanachama.  Serikali ilikusudia tokea siku ya nyuma kuyafanya maandamano yetu kuwa si ya kawaida kwa kuwa walitangaza kuyazui.  Kama tungekuwa na nia mbaya ya kufanya fujo na mauaji, basi tungewaita watu wote sehemu moja kupata wingi wa watu.  Kwa kuwa hatukuwa na nia mbaya ndio maana iliamuliwa kuwa kwa Kaskazini  maandamano yafanyike Wete na Micheweni, na kwa Mkoa wa Kusini basi wilaya ya Mkoani ijiunge na wilaya ya Chake chake kwa maandamano yaliyopangwa kuanzia Machomane Chae chake hadi viwanja vya Tibirinzi.  Wilaya zote zilikamilisha lengo kama walivyopangiwa na kwa kweli maandamano hayo yaliitikiwa kikweli kweli licha ya mauaji yaliokwisha tokea Dar es Salaam na Zanzibar.  Wanachama wetu walipata habari mapema kupitia Radio za BBC na Ujerumani pamoja na utaratibu wetu wa ndani wa mtandao maarufu wa „Radio Kifua“.  Pamoja na hayo hatukushituka wala kuogopa.

Kama tulivyosema awali jiografia ya Kisiwa cha Pemba ni ya aina  yake kwa Zanzibar, kwani kule kazi ya Polisi kuzuia watu huwa rahisi kwani bara ipitayo magari ni moja tu kuingia kila mji wa wilaya.  Katika hali kama hiyo, waandamanaji nao walipata shida kubwa ya kujikusanya kwa vile kila njia kubwa ilikuwa na vikwazo zaid ya vitatu.  Hata ukisema upite maporini ili kuwepa askari basi ukizukia juu unakutan kikwazo chengine.  Hali hii ni mbaya zaidi kwa wilaya ya Mkoani hasa kwa majimbo ya Mkoani, Mkanyageni na Mtambile.  Hata hivyo, pamoja na yote hayo wananchi walijitokeza kwa maelfu kutoka kila jimbo kwa nia ya kuandamana kwa amani.  Kabla hatujatoa tathmini ya kila wilaya basi kuna msanii katuomba tufupishe yaliyotokea kwa beti hizi za ushairi wa kuhuzunisha sana.

7.4.1    Shairi

Ilienea maafa jamii Pemba nzima

Watu wengi walikufa Baba na akina mama

Hapakua takhfifa bali yekuwa nakama

Kieleacho huzama kizamacho kikazuka

Kizamacho kikazuka kieleacho huzama

Na kile kilo anguka baadaye husimama

Si kazi kubadilika mabaya yakawa mema

Kieleacho huzama kizamacho kikazuka

Wingwi hadi Micheweni ilikithiri nakama

Ilikuwa tafrani hapakuwa na salama

Basi Wete Utaaani wakipigwa kama Kima

Kieleacho huzama kizamacho kikazuka

Mkanjuni na Madungu kulikuwa kukivuma

Watu kupigwa marungu na risasi iko nyuma

Hukumu iko kwa Mungu Ghafuru ndiye Rahima

Kieleacho huzama kizamacho kikazuka

Akikujia Polisi huna pumzi wahema

Aifyatua risasi na bebeti akuchoma

Katu hupati nafasi utapigwa kama ngoma

Kieleacho huzama kizamacho kikazuka

Dola iliiingia hofu aibu hata kusema

Dola kubwa maarufu kwenda pigana na chama

Dola haikusadifu kwa dalili ishakwama

Kieleacho huzama kizamacho kikazuka

Kweli ilipodhihiri wakubwa wengia homa

Wenyeviti Zanzibari wakataraji ujima

Wakakodi maayari kutoka Dar es salaam

Kieleacho huzama kizamacho kikazuka

Watu wakidhalilishwa na kuvunjiwa heshima

Pigo na kuhangaishwa hashimna Mahshuma

Baadaye kufikishwa korti kwenye mahakama

Kieleacho huzama kizamacho kikazuka

Kidogo nitaeleza kuficha kweli si vyema

Wala sitayanyamaza nitayasema daima

Kubwa lilojitokeza ni chuki na uhasama

Kieleacho huzama kizamacho kikazuka

Alohai duniani ajue kuna kiama

Alofika kaburini na hesabu iko nyuma

Moja kwa moja motoni kama hakufanya mema

Kieleacho huzama kizamacho kikazuka

Kila mtu ajijue asijione mzima

Uzima una mwishowe na tena una alama

Jepesi huwa ni jiwe laini huwa ni chuma

Kieleacho huzama kizamacho kikazuka

Mengineyi siyasemi hadi tamati wa tamma

Nafunga wangu ulimi nafika pakusimama

Kenda imekuwa kumi upepo sasa wavuma

Kieleacho huzama kizamachp kikazuka.

Kwa kuyapa mapana maelezo ya msanii huyu kuhusu mambo yalivyokuwa basi tunachukua nafasi kueleza kwa ufupi sana hali ya kila wilaya, Pemba

7.4.2    Wilaya ya Wete

Tokea usiku wa manane wa kuamkia mkesha wa maandamano askari walikwishaweka vikosi na vifaa vyao barabarani katika maeneo tofauti ambayo yangetokea watu kwa kuja kujikusanya palipo kusudiwa kuanzia maandamano.  Katika eneo la Madenjani hadi Chwale ilikusudiwa kuwashambulia watu waliotoka Ole, Kangagani, Kiuyu, Kambini, Mchanga mdogo, Chwale, Kojani na Kiungoni.  Humu walijua kuwa ndimo mwenye hazina ya wanachama wetu wengi.  Kwa hivyo, askari hapa walikuwa wengi na wengine walioneka katika vichaka mbali na barabara wakiwa tayari kuchukuwa amri za kuua kutoka kwa wakubwa wao.  Halikushitua wanachama wetu hili kwani Dar es Salaamu na Unguja walikwishaua na tulikuwa hatuwajui kwani walikuwa ndugu zetu kutoka Tanzania Bara, ingawa pia walikuwepo Wazanzibari tena wengine kutoka Pemba.

Kikosi cha pili kiliwekwa Limbani ili kushambulia watu waliotokea Kisiwani, Piki, Matuuni, Mzambarauni, Pandani, Machengwe na Tungamaa.  Kikosi chengine kilikuwa Kizimbani kuwashambulia watu waliotokea Kizimbani, Kwale na Pandani.  Na kikosi chengine kilikuwa Bopwe kushambulia watu waliotokea Gando, Junguni, Ukunjwi, Chanjaani Madaniwa na Raha.  Hivyo, ni kusema kwamba Wilaya nzima ya Wete ilikwisha zungukwa na askari wakiwa katika mavazi ya kivita kabisa.  Wakati wote tokea kuelezea taarifaa hii hatukuwataja kabisa Jeshi la Wananchi (JWTZ), lakin hapa sasa tunaanza kuwataja.  Kwa wao kuingilia mwisho katika kisiwa cha Pemba, yawezekana fitna ilikuwa kali zaidi.  Tulisema yaelekea walielezwa kwamba sisi tutakuwa na vita na pengine tutakuwa na majeshi kutoa nchi za nje wakitusaidia.  Hivi ndivyo viongozi wa CCM walivyo wakiwaambia wananchi kuwa sisi tunatumiliwa na watu wa nje.

Kwa Wete, mauaji yalianza Limbani ambapo waandamaji pamoja na kuwaona wenzao watatu wameshauliwa ghafla mbele yao, hawakurudi nyuma bali walizidisha mori na kusonga mbele kiasi ya kuwafanya askari wakimbie kidogo baada ya kumalizikiwa risasi.  Baadae waliongezwa askari waliofika kwa magari baada ya kuwasiliana na kuomba msaada na vifaa.  Hapa ndipo majeshi ya ulinzi nayo yalipoingilia na kuanza kuwashambulia raia bega kwa bega na Polisi.  Huku yakitokea haya ardhini, angani helikopta ilikuwa ikiranda na kunyesha „mvua ya risasi“.  Baada ya muda Polisi waliweza kuwakimbiza misituni kundi la waandamanaji waliotokea upande wa Limbani kuja kuungana na wenzao wa Mjini.

Kwa kuwa hatukuwa na silaha yoyote basi hapakuwa na askari alieshambuliwa na kujeruhiwa au kuuwawa, kama ilivyothibitishwa na Serikali zote mbili kwamba walipoteza askari mmoja tu aliekufa kwa kuchinjwa.  Pamoja na taarifa hii CUF inakanusha kwa nguvu zote kwamba haikuhusika na kifo cha huyo askari mmoja iwapo alikufa kweli.  Maandamano yetu yalitangazwa na vyombo vyote kwamba yalikuwa ya amani na ndio maana isingestahiki kwa waandamanaji kuwa na silaha.  Matukio matatu ya kushtusha yalitokea hapo katika mauaji ya Wete.  Kwanza, baada ya watu wote kukimbia, askari walikuwa wakipita kila nyumba na kupiga risasi madirishani.  Katika mbinu hii ya kivita waliofundishwa, bila shaka nchi za ng’ambo, walipita kwenye nyumba moja na kumuona kijana ambae alikuwa kaketi barazani akipumzika.  Bila kumuuliza walimfyatulia risasi na kumkata roho hapo hapo.  Huyu ni kijana Salum Masoud Al – Miskry ambae alifika Pemba wiki moja kuangalia wazee wake akitokea Sweeden ambako anaishi tokea mwaka 1985.

Pili, askari walikwenda kwenye nyumba nyengine na kuwaona watu wakiosha maiti na kuwakung’uta risasi na wawili wakafa na maiti wao.  Kilichostaajabisha ni kwamba walipiga „radio call“ na papo hapo gari ikafika na kupakia maiti, na hatujaziona hadi hii leo.  Tukio la tatu ni kule kumpiga mama mmoja ambae alikuwa migombani kajilaza ili askari wapite wasimuone na baadae akimbie.  Huyu walimpiga risasi ya matako hakufa lakini ilichana kuanzia nyuma hadi mbele ya sehemu zake za siri.  Na kwa CCM, huku ndiko kuwapenda wanawake.  Kwa ujumla basi takwimu sahihi ya maiti waliowashuhudia wao tu ni 26 kwa Wete.  Wako waliopigwa na helkopta na kufa, lakini hawa walikuwa misituni wakikimbia mauti, ingawa huko Mahita aliwafuta.  Mji ulizizima na waliokuwa na kamandi ni askari ambao walikuwa wakipita kila kona ya mji na kuchukua na kamandi ni askari ambao na watu waliokuwa wakichunguza kwa makini mwenendo wa askari hao watii kwa CCM na Dola lakini makatili kwa raia wasio na hatia.

Wananchi watakumbuka kwamba mara tu  baada ya aliekuwa Mwenyekiti wetu wa mwanzo, mkongwe wa siasa Mapalala kukiasi chama chetu alitumiwa na dola kubuni na kusambaza uongo kwamba Libya inatusaidia kupanga njama za kumpingua Dr. Salmini.  Basi yawezekana usalama wa Taifa waliishauri Serikali vibaya na kuwaona Wapemba wanahitaji kushughulikiwa zaidi.  Vile vile Pemba ilishughulikiwa sana kuliko sehemu nyengine kwani tumeshaona mpishi wa historia, Profesa Mmuya alivyosema, it is conceded by CUF leaders and the members a like that Pemba is the preasure centre and the rest are action zones, [Mmuya, 1998:37].  Maana yake ni kwamba, inachukuliwa na viongozi wa CUF pamoja na wanachama kwamba, Pemba ndipo pahala pa shindikizo na sehemu nyengine hufuata  tu kwa vitendo.  Kwa kuwa vitendo vya unyanyasaji na mauaji (vya Polisi) vilianzia unguja na Dar es salaam tarehe 26 Januari kabla ya Pemba, basi hapa unaonekana uongo na fitna za kifalsafa ambazo husinginiziwa historia.  Ingetarajiwa pale pahala pa shindikizo ndipo kungekuwa mwanzo wa matukio hayo ya kutisha kama yanavyotabiriwa na mchunguzi aitwae Profesa.

7.4.3    Wilaya  ya Micheweni

Askari waliweka kizuizi kimoja tu kabla ya kufikia kituo cha Polisi cha Wilaya.  Kizuizi kilikuwa Kilindini kwenye mpaka wa Micheweni na Konde, katikati ya msitu wa Micheweni katiya njia inayotoka Mjin Wingwi na kwenda kituo cha polisi, kizuizi kikubwa kiliwekwa mita 10 kutoka kituo cha polisi.  Na hapo ndipo walipouliwa watu wengi.  Baada ya kutoa amri Mkuu wa Wilaya Ramadhan Juma Shaibu ambae pia yeye mwenyewe ni Ofisi wa Polisi.  Kwa kawaida Wakuu wa Wilaya na Mikoa ni Majeshi, Polisi na Usalama.  Hizi ndizo nafasi walizotengewa na Baba wa Taifa.  Kwanza majeshi yalikuwa katika siasa wazi wazi kwa muda wote wa kipindi cha mfumo wa chama kimoja.  Baada ya Tume ya Nyalali kupendekeza kuwatoa katika siasa, basi shea yao ya uongozi iliongezwa katika Mikoa na Wilaya ingawa pia wanaweza kuwa Wabunge.

Kwa hivyo, maendeleo ya Mkoa ni pamoja na kuimarisha ulinzi na ikaonekana kuwa na viongozi walio malinza ni bora kwa kuimarisha ulinzi na usalama.  Hii ndio maana basi majeshi wengi (kama si wote) ni wanasiasa kuliko hata Wabunge wengine, na ndio sababu wanashindwa kuwa waadilifu wa kazi zao, kwa kuwa maadaili ya kiulinzi yamechanganywa na siasa.  Hivyo basi ukali wao wa kuvita huanzia kufanya mazoezi juu ya migongo ya Wazanzibari, hasa Wapemba; maana ndivyo wanavyo ambiwa asubuhi na jioni na hata na Amiri Jeshi mwenyewe kwamba Wapemba ni maadui na hawaitakii mema nchi hii.  Kwa hivyo, askari hawakufanya kosa, walikuwa wakitekeleza “amri halalli” ambayo huanzia kwenye Kamati ya Ulinzi chini ya Mwenyekiti wake Rais wa Jamhuri, Mheshimiwa Ben Mkapa.

Tukirudi basi, katika mfululizo ule wa risasi ulitokea pale penye kizuizi cha kwanza jumla ya watu 10 walikufa kufumba na kufumbua.  Mkimbizi mmoja alieleza kamsikia Ramadhani, Mkuu wa wilaya ya Michweni, akisema “mwasubiri nini kama hamjaua”.  Na kule Wete pia kulikuwa na Mkuu wa wilaya akiitwa hivyo hivyo Ramadhan lakini baba yake ni Feruzi.  Huyu ndie alietoa amri kwa askari ambae alimuua Shahidi wa kwanza wa demokrasia marehemu Omar Ali wa Shumba Mjini mwaka 1992, wakati akipachika bendera ya kwanza ya CUF Kaskazini.  Baada ya kufanya kazi zao vizuri, Ramadhan wote wawili sasa wamepimzishwa kazi ya Ukuu wa Wilaya kama kawaida yao hawaachishwi ila hupewa uhamisho na kurudia kazi zao za ulinzi.  Baadhi ya askari wa Zanzibar ambao walilazimishwa kuuwa na wakauwa baba na mama wa wenzao, hawa wamechukuliwa na kufichwa Bara.  Yule alieuwa vizuri zaidi yuko Arusha kwenye mandhari safi ya hewa baridi.

Alipokalia kiti Bwana Amani Karume, aliamua kuwabakisha kazini Wakuu wote wa Wilaya lakin baada ya kama miezi sita hivi Ramadhan wote wawili akawaondoa.  Hii ni hukumu ya kimya kimya kwa zile wilaya zilizouwa kupita kiasi lakini alie akisimamia mauaji Mahita, tunaambiwa na Mbita tumsamehe.  Hii ni dhihaka, na iwapo hili litekelezwe Tanzania basi lianzie kwenye Mahkama ya Kimataifa ya Mauaji Rwanda na Burundi kule Arusha ili iwe mfano sio tu kwa Zanzibar lakin kwa Afrika nzima.  Tunawaka Watanzania waelewe kwamba huu tunaoueleza leo ndio ukweli na ukweli unauma lakini haumi kuliko risasi zilizoondosha ndugu zetu.  Jambo moja la kuhuzunisha hapa Wilaya ya Micheweni lilitokea kama ilivyokuwa kule Wete.  Msitu wa Maziwa Ng’ombe ulikuwa na sehemu chafu kupitika.  Hapa palipotea watu wengi.  Helkopta ilikuwa ikiwamwagia risasi watu waliokuwa wakikimbia ovyo kujisalimisha.  Wengi waliokuwa wakipita sehemu chafu ni wale watu wa vijiji jirani wasio na uzoefu wa sehemu hizi.

Baada ya helkopta kuona kwamba hakukuwa na watu wengi tena barabarani na misituni, bosi alishuka Wapemba waliokwisha kata roho.  Pia walioondosha maiti na sisi hatukujua wapi walienda nazo.  Tulizungumza hapo awali kuwa kulikuwa na kaburi la siri lakin Serikali haikutaka awali pafanyike uchunguzi kwani wakati ule siri ingefichuka.  Sisi hatumshangai Mbita kwa kusema hakuona makaburi ya halaiki, huu si utamaduni wao CCM.  Na kwa kweli haitafika siku CCM na Serikali zikaungama kukubali kuwa Zanzibar kuna makaburi ya halaiki na siri, hadi pale siku watakapoonesha makaburi ya akina Kassim Hanga wenziwe.  Jee haya hayako, na iwapo haya hayako wao wako wapi?

Hivi ndivyo CCM inavyowapoteza Wazanzibari, na ndio maaana halisi ya “Mapinduzi Daima”.  Ilikadiriwa basi, baada ya wale 11 wa uhakika, wapo wengine kama 31 walihofiwa ama kufa au kupotea.  Hesabu hii ilipatika wiki moja hivi baada ya kuendesha sensa ya siri katika wilaya nzima.  Na iwapo kuna Mtanzania anasema CUF inatia chumvi au uchochezi (kwa maana hizi ndizo lugha za CCM wakificha madhambi yao) basi wailaumu taarifa ya Shirika la Kutetea Haki za Binaadamu la Human Right Watch ambayo ilitoa matokeo ya uchunguzi wake mara tu baada ya mauaji.  Taarifa hiyo iko katika nyaraka mbalimbali zinazotunzwa na chama.

7.4.4    Wilaya ya Chake chake

Chake chake kulikuwa na vizuizi vitano.  Kizuizi cha kwanza kiliwekwa Mkanjuni ili kuwazuia watu waliotokea Ziwani, Kidemeni, Mchanga wa Kwale, Semewani, Mavungwa, mbuzini, Niyapi, Kwale, Gombani, Ng’ambwa na Mkoroshoni.  Kizuizi cha pili kiliwekwa Machomane ili kuwazuia watu waliotokea Vitongojji, Wawi, mgogoni, Furaha, Mvumoni, Pujini na Vikunguni.  Kizuizi cha tatu kiliwekwa Shamiani ili kuwazuia watu ambao wangetoka sehemu za Mkoani ili kuja kujiunga na wenzao kwa kujipanga Mkanjuni na kuelekea Tibirinzi.  Vile vile kulikuwa na kizuizi kwenye makutano ya barabara itokayo Vitongoji na Mgogoni ili kuwazuia awote ambao wangetoka Pujini, Mtangani na Chambani.  Kulikuwa na kikosi cha askari polisi na jeshi katika sehemu za Chanjaani kuzuia watu ambao wangetoka sehemu za Chanjamjawiri na kuendelea.

Pamoja na askari kutumia silaha na nguvu za kupita kiasi ili kuwadhuru wanaandamanaji, lakini watu hawakurudi nyuma waliendelea kusonga mbele.  Polisi waliposhindwa kuwazuia waandamanaji waliomba msaada kwa kambi ya Jeshi ya Vitongoji na mara tukawaona Polisi, FFU na JWTZ wakiwa sambamba na kuanza kupiga risasi za moto.  Kama kkawaida, juu kulikuwa na helkopta ikipita hadi karibu ya mabonde ya nyuma ya nyumba za Serikali za machomane.  Juu ya majumba hayo kulikuwa na askari ambao walitoa mawasiliano moja kwa moja kwa askari popote katika Mji wa Chake, hasa kwa vile ukikaa juu ya nyumba zile unaona karibu mji mzima.  Mara moja Helkopta ilikuja karibu sana na mava yaliopo kwenye kituo cha mafuta cha Sahrif Kassim.  Askari walitoka mlangoni na kutengeneza bunduki ili wapige lakkini halafu ikaruka biila kuangusha risasi plae.

Watu waliokuwepo kwenye mava mara wakasikia risasi.  Wakatikiri ni za machozi wakataka kutoka mavani kuelekea Tibirinzi moja kwa moja.  Walikuwepo vijana waliokuwa wakijua milio ya risasi na hawa wakawazuia wenzao wasitoke.  Mra tukasikia mamaangu wee! Mtume!  Mara kimya, watu wameingia misituni, lakini wengine walikwisha kufa zamani.  Pale vurumai jengine lilitokea sehemu za misituni kukimbia helkopta na Polis wakawakurupusha ili warudi kule kule na hapo watu wengi walipigwa risasi wakafa na wengine kujeruhiwa.  Taarifa ya wilaya ilionesha kwamba Chake chake walikufa watu 13 na wengine wengi walijeruhiwa.  Kuanzia hapo watu walianza kutawanyika na baada ya kusafika hapo ndio askari wakajikumbusha shughuli ya kimapinduzim kubaki wanawake na watoto wao tena mbele ya waume zao.  Askari walishangaza sana kwani watu wengi waliokuja kwa maandamano walitoka sehemu mbali mbali, na Machomane walikutana tu.  Hata hivyo baada ya watu kukimbia ghadhabu za askari walizitoa pale Machomane.

7.4.5    Wilaya ya Mkoani

Kama tulivyosema awali wanachama wa wilaya ya Mkoani walitakiwa wafike Chake kujiunga na wenzao wa kule na kuendelea na maandamano.  Hali ya kijiografia ndio iliowafanya watu wengi wa Mkoani kutoweza kufika Chake.  Ili watu wa Mkoani wafike Chake, ni lazima kutumia usafiri wa magari.  Kwa kuwa huwezi kufika Chake bila kupita Mtambile ambako kuna kituo cha Polisi, hii iliwafanya watu wengi wasifike.  Hata hivyo, wako watu wengine walifika Chake kwa kupita maporini.  Wengine walitueleza kwamba iliwalazimu kulala Chake chake ili kuwahi.  Na ushahidi ni kwamba kuna orodha ndefu ya watu waliojeruhiwa na humo tuliona majina ya watu kutoka Kengeja, Kiwani na sehemu nyengine.

Hata hivyo, kwa kuwa mpango wa mauaji na kujeruhi ulikuwa umepangwa tayari na CCM na dola yake, basi watu wa wilaya ya Mkoani hawakukwepa virungu ingawa hawakuuliwa hata mmoja.  Siku ya pili yake, wakati hakuna tena dalili ya maandamano, askari waliweka vizuizi katika sehemu za Mtambile na Changaweni.  Kwa Mtambile ndio waliambiwa kuwa hapo kulikuwa na Hizba na Shirazi, basi hapa waliwaandama watu wenye ndevu na kuwavuta.  Ilikuwa akipita mtu mwenye ndevu anaitwa Sefu; huyu anavutwa chini na juu, lakini ukiwa huna ndevu unaitwa Mkapa; utasalimika.  Iliendelea hivi kwa karibu wiki tatu.  Watu wanashushwa kwenye magari na kupekuliwa hadi sehemu za siri, mke na muume bila kuchagua.  Mzee mmoja licha ya kwamba walikuwa na vyama vilivyopinduliwa, lakiini hawakupata shida kama ya siku ile.

Wakati huku askari wananyanyasa hakukuwa na namna ila kupita na kuwapeleka wagonjwa hospitali kuu ya Mkoani.  Kule watu wa Mkoani ndio waliokuwa na kazi kubwa ya kuwahudumia wagonjwa kwa kuwapatia chakula na madawa.  Shukrani ziwaendee kwa kazi kubwa ya kusaidia chama.  Hata Makao Makuu walifurahi sana kwani hakukuhitajika msaada mkubwa kutoka kule.  Watu wenyewe wakiongozwa na kijana aitwae Meneja Asaa walifanya kazi hiyo ngumu.

Sehemu ya 5: Matokeo Baada ya Maandamano

Maafa ya mauaji na majeruhi yaliyotokea kwa wilaya zote zilizofanya maandamano ni makubwa.  Idadi inayooneshwa ni ya wale waliopatikanwa kuzikwa na majeruhi kutibiwa.  Itachukua muda mrefu kwa ulimwengu kupata idadi halisi na habari kamili ya vitendo vingine vya uvunjaju wa haki za binaadamu vilivyopitishwa na vyombo vya ulinzi, kama ambavyo Tume ya Mbita  ilishindwa.  Kuna habari walizotuletea wenzetu wa Dar kuwa wakati wa mauaji Zanzibar, manuwari ndogo za kijeshi ambazo hukaa Kigamboni ziliwahi kuteremsha masanduku ambayo yalifanana kama yale yanayotumiwa kwa kuchukulia maiti.  Wao walifikiri kwamba nao askari walikufa wengi, lakini baada ya kusikia kuna askari mmoja tu kafa kwa mujibu wa taarrifa za Serikali, basi pengine hali hii inatoa dalili kwamba pengine zilikuwa maiti za Wazanzibar zilikimbizwa ili kukwepa ushahidi wa wazi.  Huu ndio mtindo wa Zanzibar tokea Mapinduzi kwa ndugu na jamaa waliopotea.  Tunadumisha mapinduzi kwa kazi kama hii iliyoanzishwa na wazee wetu.

Tatizo jengine kubwa tulilopata ni la wakimbizi.  Kwa mara ya kwanza Tanzania ilijitia aibu kubwa ya kuwa na wakimbizi nje ya nchi makundi kwa makundi, hasa kutoka Zanzibar.  Suala hili liliiweka Serikali njia panda na ndio maana lilifanywa kila liwezekanavyo, lakini suala la wakimbizi lisitokee.  Katika kuhakikisha hili ndipo helkopta ilipotumiwa kuwaangamiza watu waliokuwa wakisafiria madau kwenye nchi ya jirani, Kenya.  Bada ya kuzamisha jahazi moja taarifa zilienea nje na ndani na ndio wakasimamisha ukatili huu wa dhahiri.  Kwenda Mombasa ilikuwa ni lazima kwani wagonjwa wengi walikoseshwa huduma kwenye hospitali za serikali na hakuna hospitali za binafsi kisiwani Pemba.  Sisi tulikuwa na hofu kwamba kwa siasa za Afrika Mashariki, watawala wana tabia ya kusaidiana ili kuziweka tawala zao bila ya bughudha.  Hii ndio maana, Tanzania na Kenya zilitiliana mkataba wa kubadilishana wakimbizi wakati wa jaribio la kuangusha serikali ya Tanzania miaka ya sabiini.  Hata hivyo, wakimbizi wetu walipata mashirikiano mazuri kutoka kwa Serikali na wananchi wa Kenya.  Tunalishukuru Shirika la Ukimbizi la Umoja wa Mataifa (UNHCR) kwa huduma nzuri, pamoja na matatizo madogo madogo ambayo yanavumilika.

Kwa ujumla idadi ya vifo na majeruhi kwa wilaya za Pemba ni kama itavyoonekana hapa chini, ingawa idadi hiii haikuweza kuwaingiza wale wanaohofiwa kufa kwenye mapori na wengine bahrini wakati wakielekea Mombasa kwa ukimbizi na matibabu.  Kwa kweli suala la ukimbizi lilisababisha kutopata takwimu sahihi ya waliokufa, lakini vile vile, unyanyasaji wa karibu mwezi mzima baada ya mauaji ualisababisha mtu asiweze kufanya uchunguzi wa kina.  Aidha katika mazingira haya, mtu angefikiriwa kakimbia kumbe ameshakufa.  Taarifa zilizopatikana ni zile tu zilizoshuhudiwa na vijana wetu wa Blue Guards wakati wa kadhia hii.  Vile vile kuna watu wengi waliokufa siku za baada ya marukio haya, lakini bado sababu ni zile zile za unyanyasaji wa majeshi kwa raia wao zilizotokana na matukio ya siku za mauaji.  Pamoja na yote hayo majeshi yetu yalipora mali na vyakula kama ilivyokuwa siku za vita vya Ugandana Tanzania.  Hatukutaja habari ya mali kwani roho na damu vilikuwa bora zaidi kutupotezea muda kuelezea kuliko mali.

7.5.1    Takwimu za maafa

Jadweli Na 8: Takwimu za maafa

Wilaya

Waliouliwa na kutambuliwa

Waliohofiwa kufa/kutooneka tena

Majeruhi

Vilema

Wete

16

13

109

37

* Micheweni

11

17

203

42

Chake

6

5

67

21

Mkoani

-

-

16

-

Unguja

10

-

178

35

**Bara

3

-

85

-

Jumla

46

35

658

135

•           Micheweni kuna maiti mmoja hakutambuliwa na maiti mmoja (Mohd Amour) alikutwa ufukweni baada ya siku sita.  Hii ilithibitisha kwamba wako watu wanaohofiwa kufa majini au katika mapori au katika mazingira ya kutatanisha.

**    Wawili walikufa Bara, na mmoja (Mariam Kyango)   alifia Mbeya baada ya kuondolewa Zanzibar akiwa taaban.  Huyu ni wa tatu.

7.5.2    Majina ya Marehemu

Jadweli Na. 9: Majina ya marehemu

S/No.

MAREHEMU

WILAYA

1

Mjaka Salim Ali (Kiuyu)

Wete

2

Hassan Omar Hassan (Mtambwe)

Wete

3

Haji Kombo Ali (Mchanga Mdogo)

Wete

4

Said Abdalla Suleiman El Ruweihy

Wete

5

Ahmed Said Othman El Khaif

Wete

6

Kombo Ali Abdalla (Aliuliwa akienda shamba)

Wete

7

Salum Juma Salum (36, Chasasa; aliuliwa wakati akimuosha maiti Kombo Ali)

Wete

8

Moh’d Masoud Seif El Miskry

Wete

9

Juma Bakar Juma

Wete

10

Haji Muslim

Wete

11

Salum Masoud El Miskry (aliuliwa akiwa nyumbani akiangalia maandamano, alikuja kutoka Sweden ili kuoa)

Wete

12

Haji Kombo Ali

Wete

13

Abdalla Moh’d Salum El Mazrui

Wete

14

Abdalla Moh’d Abeid

Wete

15

Mjaka Ali Msonga

Wete

16

Ali Omar Kibabu (Mtambwe)

Wete

17

Mchande Saidi Mchande (35, Msuka)

Micheweni

18

Hemed Saidi Omar El Kindy (45, Wingwi)

Micheweni

19

Ali Juma Makame (40, Mjini Wingwi)

Micheweni

20

Abdalla Hamad Rajab (30, Kinyasini)

Micheweni

21

Khatib Omar Othman (30, Wingwi)

Micheweni

22

Haji Hassan Makame (30, Tumbe)

Micheweni

23

Moh’d Amour Salum El Khaif (26, Kinyasini)

Micheweni

24

Aliripotiwa na Polisi na hakutambuliwa jina

Micheweni

25

Mbarouk Kh. H (20, Wingwi)

Micheweni

26

Hemed S. Omar (36, Njuguni Wingwi)

Micheweni

27

Ali Haji Kombo (44,Mtoni)

Chake Chake

28

Malik Mbarouk Hamad (25, Mvumoni)

Chake Chake

29

Said Moh’d Kassim (30, Gombani)

Chake Chake

30

Habib Salim Kassim (30, Furaha)

Chake Chake

31

Ali Juma Ali (Machomane)

Chake Chake

32

Said Kombo Haji

Chake Chake

33

Ali Haji Mdungi (53, Magogoni)

Unguja

34

Mwalim Nassor Mwalim (31, M’kwerekwe)

Unguja

35

Abdalla Said Moh’d El Ghassany (37, Magomeni)

Unguja

36

Mtumwa Haji Mati (57, M’makumbi)

Unguja

37

Gharib Salim Hamad El Mindhir (26, Hurumzi)

Unguja

38

Kombo Rashid Ali (32, Daraja bovu)

Unguja

39

Hamad Said Hamad (58, Jang’ombe0

Unguja

40

Juma Khamis Moh’d (32, El Jahadhmy)

Unguja

41

Haji Ali

Unguja

42

Bakar Ali Hamad (25, Misufini, kafia mikononi mwa Polisi, Ng’ambo)

Unguja

43

Maryam Kyando (alikufa kijijini kwao Mbeya, baada ya kupigwa na Polisi, Zanzibar)

Mbeya

44

Jaffar Said (Kafa siku 2 baada ya kipigo)

Tanga

45

Laurenti Mayenjwa

Mwibara

7.5.3    Vizuka (wajane) na Mayatima

Ifuatayo chini ni idadi ya wanawake waliouliwa waume zao pamoja na mayatima wao:

Jadweli Na. 10: Waliouliwa Waume zao na mayatima

S/N      MAREHEMU/KIZUKA          WILAYA         KIJIJI  YATIMA

S/N

MAREHEMU/KIZUKA

WILAYA

KIJIJI

YATIMA

1

Ustadh Juma khamis Mohammed/Biubwa

Mjini

Mkamasini

Hana

2

Ali Juma Makame/ Fatma K. Makame na Mwanakhamis

Micheweni

Mjini/Wingwi

Mwamize A. Juma (16), Sharif A. Juma (13), Salim A. Juma (miezi 4), Hadiya A. Juma (5)

3

Kombo Rashid Ali/Time Khamis na Amina Said

Micheweni

Micheweni

Rashid k. Rashid (7) Time K. Rashid (5), Asha K. Rashid (2), Zawadi K. Rashid (3)

4

Abdalla Hamad Rajab/ Asha M. Omar na Bitumu A. Moh’d

Micheweni

Kinyasini

Hassan A. Hamad (miezi 6), Pili A. Hamad (7), halima A. Hamad (6), Time A. Hamad (2)

5

Hemed Said Omar/Maryam A. Omar na Maram A. Nassor

Micheweni

Wingwi

Sada H. Said (14), Mboga H. Said (8), Salama H. Said (12), Juma H. Said (15), Wardat H. Said (7)

6

Khatib Omar Othman/ Mwajuma Shaaban

Micheweni

Wingwi

Khadija Khatib Omar (3), Sabra Khatib Omar (1)

7

Hamad Said Hamad/ Salma O. Mbwana

Mjini

Jang’ombe

Hussein H. Said (17), Fatma H. Said (6), Hafsa H. Said (4)

8

Mtumwa Haji Matti/ Amina Kh. Shaaban na Tatu Mosi

Mjini

Mwembe Makumbi

Khalfan M. Haji (13), Abdulwahid M. Haji (7), Shaib M. Haji (10), Hafsa m. Haji(3), Husna M. Haji (3), Mwanaharusi M. haji (10), Ibrahim M. Haji (7).

9

Abdalla Said Moh’d/Fatma Aman Hamad

Mjini – Unguja

Magomeni

Nasra A. Said (13), said A. Said (11), Latifa A. Said (10), Khadija A. Said (7), Ali A. Said (5), Kauthar A. Said (3), Safia a. Said (1), fadhila A. Said (2)

10

Mwalim Nassor Suleiman/Rukayya Abdalla

Mjini Unguja

M’kwerekwe

Nassor M. Nassor (2), Maryam M. Nassor (miezi 2)

11

Mjaka Salim Ali/Fatma Ali Hamad

Wete

Kiuyu

Hamad Mjaka Salim (10), Mwanaisha M. Salim (8), Ali M. Salim (7), Salim M. Salim (4), Rehema M. Slaim (miezi 3)

12

Salum Juma (Fundi)/Shufaa A. Moh’d

Wete

Chasasa

Juma S. Juma (11),  Fatma S. Juma (9), Ahmed S. Juma (7)

13

Ahmed Said Othman/Khadija Ali Othman (Siti)

Wete

Mtemani

Rahma A. Said (17), Said A. Said (15), Aziza A. Said (13), Maryam A. Said (1)

14

Abdalla Moh’d Salim

Wete

Kizimbani

Walid A. Moh’d (8), Nasra A. Moh’d (7), nasria A. Moh’d (7)

15

Haji Kombo Ali/Fatma H. Moh’d

Wete

M’mdodo

Riziki Haji Kombo (16)

16

Ali Haji Kombo/Dalila Moh’d Ali

Chake chake

Shamiani

Maryam A. Haji (7), Seif A. Haji (8), Moh’d Ali Haji (12), salum A. Haji (10), Yahya A. Haji (14), Mustafa A. Haji (miezi 3)

17

Habibu Salum Khamis/Bimkubwa Moh’d Khamis

Chake chake

Furaha

Nasra Habib Salum (3), Husna H. Salum (2), Warda H. Salum (1), Haytham H. Salum (miezi 6)

18

Said Moh’d Kassim/Zuhura N. Humud

Chake chake

gombani

Nayrat Said Moh’d (3), Ahmed S. Moh’d (1)

19

Ali Haji Mdungi/Maryam Nyange na Maryam Said

Magharib Unguja

Magogoni

Issa A. Haji (13), Salum A. Haji (11), Mwajuma A. Haji (15), Khadija A. Haji (9), Said A. Haji (6), Mgeni A. Haji (2), Is – hak A. Haji (1)

Angalia: marehemu wasioorodheshwa hapa hawana au hawakuacha vizuka.

Katika stilahi, neno “Binaadamu” au “Mwanadamu” ni “tamyizi”, yaani upambanuzi au sifa ya kumtafautisha baina yake na viumbe wengine.  Kwa maana hiyo binaadamu ni aina ya kiumbe – kiumbe mwanadamu kwa lugha nyengine “human being”. Na inapoondoka sifa hii ya ubinaadamu (humanity) ukabali neno “kiumbe” kwa lunga nyingine “being”, kiumbe hiki huwa hakina tafauti na vitendo vya viumbe wengine na hata mara nyengine kuzidi.  Ni kwa kuikosa sifa hii ya ubinaadamu (humanity) yaani UTU kwa maana ya huruma kwa wengine, ndio katika jamii ya wanyama, mwenye nguvu ndiye mwenye haki na wa chini ndiye anamiwaye hata kama ndiye mwenye haki.

Katika jamii ya majibwa kwa mfano, yule mnyonge akionekana kaokota mfupa basi hupigwa na mwenye nguvu, na endapo atapiga mayowe ya kuomba msaada basi wakija wenye nguvu wengine na kumkuta chini akipigwa, basi wale wengine hawaulizi bali hujiamulia tu kuwa wa chini ndiye mkosa na kwa hivyo ndiye anamiwaye zaidi.  Matendo ya Polisi waliyofanya Tanzania dhidi ya raia baada ya kuyavunja maandamano sio kwamba yalikosa kabisa ubinaadamu bali vilikuwa ni vitendo vya unyama wa jamii ya majibwa waliopata amri ya “Shike” kutoka kwa mambwana zao.

Bado tunasema mawili zaidi.  Kwanza mauaji yaliitwa na chaguzi mbovu na sio historia.  Pili na mwisho, maneno haya ya ukweli mtupu yatauma, lakini kwa vyovyote maumivu yake hayatafikia yake ya risasi zilizowapiga wazee, baba, mama na watoto wetu.  Aidha maumivu ya maneno haya hayarafikia yale maumivu ya kunajisiwa wake na dada zetu kama mithili ya mnyama wa Serengeti.  Sisi tunaendelea kuvumilia lakini kamwe hatusahau.  Tunatarajia pia anaeguswa na maneno haya ya ukweli na yeye atavumilia. Ndivyo, tulivyo aswa na Tume ya Mbita kuwa tuvumiliane.

SURA YA NANE





Mauaji ya 2001: Uchaguzi wa Oktoba 2000, Bara

17 12 2008

SURA YA SITA

UCHAGUZI WA PILI WA VYAMA VINGI: TANZANIA BARA, OKTOBA, 2000

Tulishindwa kuishawishi Serikali kutunga Katiba mpya ya nchi itakayowahusisha wananchi, na pia tulishindwa kuilazimisha Serikali kuunda tume mpya za uchaguzi Bara na Zanzibar zenye uwakilishi wa ridhaa na kukubalika kwa vyama vyote vya siasa.  Hii pekee ilitosha kutuelewesha kwamba uwanja wa siasa haukuwa sawa.  Wakati hili tukilijuwa tuliingia katika uchaguzi na matumaini kuwa tungeweza kushiriki uchaguzi huo kwa kuzuia aina zote za wizi wa kura zilizotayarishwa na CCM.  Hata hivyo, wizi na ukiukwaji wa sheria za uchaguzi ulianza tangu wakati wa uandikishaji.  Matokeo ya mwisho ni kwamba haki haikutendeka na kwa kweli haikuonekana kutendeka kwa Bara na Zanzibar.  Uvurugaji wa uchaguzi wa mwaka 2000 ulikithiri kuzidi hata ule wa uchaguzi wa mwanzo, 1995.  hatukujuwa kuwa wakati sisi tulikuwa tunajitayarisha kwa uchaguzi wa kidemokrasia, kumbe wenzetu walikuwa wakijitayarisha kwa uchaguzi wa kishindo.  Hivi ndivyo kwa muhtasari hali ilivyokuwa Tanzania Bara.

Sehemu ya 1: Uandikishaji wa wapiga kura

Zoezi la uandikishaji wa wapiga kura lilikuwa na dosari kubwa kwani lilitawaliwa na ujanja, wizi na ukiukwaji mkubwa wa sheria za uchaguzi.  Udanganyifu huo ulipangwa vizuri na CCM kiasi tulishindwa kuugundua awali na kwa hivyo tulipotanabahi na kuanza kulalamika mawakala wetu walikuwa wakitimuliwa na askari ambao kama kawaida walikuwepo kulinda amani na kuhakikisha kwamba CCM haiachii madaraka hata ikishindwa.  Yako matatizo mengi katika uchaguzi wa Bara lakini kwa muhtasari tunagalie baadhi tu ya dosari za wazi za uchaguzi wa 2000.

6.1.1    Vituo Bubu

Kwanza tulibaini kuwa kulikuwepo na “vituo bubu” vingi vya kutuibia kura.  Hivi ni vituo visivyoonekana lakini huwa vinatumiwa kuingiza kura ambazo taarifa zake ni sawa na kura za vituo vingine vya kawaida kwa kila kitu.  Vituo bubu havikuingiwa na watu wengi lakini masanduku yake yalikuwa na kura nyingi kama vituo halisi.  Kwa mujibu wa takwimu tulizonazo, Dar es Salaam pekee kulikuwa na vituo bubu 518 ambavyo kwa makisio ni sawa na wapiga kura hewa 1555,445.  Kwa Tanzania Bara nzima kulikuwepo na vituo Bubu 4831 ambavyo vinafanya idadi ya wapiga kura hewa kuwa ni 1,449,300.  Kura hizi ndizo zilizowawezesha wagombea wa CCM kuwashinda wagombea wa upinzani “kwa kishindo” kama wanavyosema wao wenyewe.  Ili kuwe na uwezekano wa kutumia mkakati huu wa kura bubu, basi idadi ya watu waliojiandikisha siku zote hutangaza kubwa kuliko ile halisi, na ile inayozidi hujalizwa na wapiga kura hewa.

6.1.2    Wizi na kusambaa ovyo kwa shahada

Kwa kawaida Tume ya Uchaguzi ya Taifa huainisha idadi ya kura (Fomu Na. 1) katika Fomu Na. 13 iitwayo “MGAWANYO WA FOMU NAM 1”. Hii ni shahada ya kupiga kura ambayo imeainishwa ndani yake, idadi ya vitabu na mtiririko wa namba (serial number) zake vilivyogawanywa katika kila Mkoa na Jimbo.  Tuligunduwa kuwa, Katika sehemu kadhaa za vituo vya kupiga kura orodha wa idadi ya vitabu haikulingana na mtiririko wa namba.  Kwa hivyo, wizi wa kura ulisababishwa na kusambaa ovyo kwa shahada zakupigia kura.

6.1.3    Kuzuiliwa kupiga kura watu wenye shahada halali

Zoezi la kuendesha kampeni za nyumba kwa nyumba za CCM lilisaidia kupata na kuratibu namba za shahada za kupigia kura (Fomu Na 1) na hivyo kuwezesha kuchapishwa kwa shahada zingine za bandia zinazofanana na hizo.  Katika hali hiyo wapiga kura halali wenye shahada hizo zilizonukuliwa awali walishindwa kupiga kura kwa kuwa shahada bandia zilikwishatumika kabla hata wao hawajafika vituoni kupiga kura.  Wizi wa aina hii uliofanyika nchi nzima ulipunguza sana kura za CUF na wapinzani na kuongeza sana kura za CCM.

6.1.4    Matokeo kutangazwa bila kujumlisha kura

Katika majimbo mengi, kwa mfano Kondoa, Sumue, Morogoro, Nzega na Bukene matokeo yalikuwa yakitangazwa bila hata ya kukamilika zoezi la kujumlisha kura kinyume na sheria na kanuni za Uchaguzi.  Mkakati huu ilitumika baada ya Tume kuwaibia CCM kura nyingi.

6.1.5    Usambazaji Kinyemela wa vifaa vya kupigia kura

Sehemu nyingi vifaa hivi vilisafirishwa siku ya mwisho kabisa tena usiku sana kwa magari ya binafsi na ya Serikali yasiyokuwa na alama za Tume ya Uchaguzi (NEC).  Vifaa hivyo vilifikishwa kwenye nyumba za watu binafsi, au za viongozi wa Serikali za mitaa, wilaya au Mikoa au wa CCM, na vilipokewa bila mawakala kushirikishwa.  Sehemu zilipofikishwa vifaa kinyemela zilitumika shahada za wizi.

6.1.6    Masanduku ya kura kuhaulishwa mbali na vituo vya kura

Hii ni njia nyengine iliyotumika kuiba kura nyingi.  Katika sehemu kadhaa, kabla na hata baada ya kuhesabu kura, masanduku ya kura yalihamishwa kutoka kwenye hata vituo vya kupigia kura au kuhesabu kura au kujumlishia kura kwa sababu mbalimbali za udanganyifu.  Kama ikitokea wakala wa upinzani kukataa, mabavu na vitisho vilifanya kazi.  Uhamishaji huo haukusindikizwa wala kushirikisha mawakala wa vyama vyote vya siasa husika.  Udanganyifu mwingi ulitokea wakati wa uhamishaji masanduku ya kura, kwa kubadilishwa masanduku yenye kura bandia kwa yale yenye kura halisi.

6.1.7    Mawakala kutopewa Fomu Na. 13 na Na. 16

Katika kata nyingi mawakala walikuwa hawapewi fomu hizi za kuandika idadi ya kura zote, na za kuandikia malalamiko ambazo msimamizi naye alitakiwa ashuhudie kwa kutia saini.

6.1.8    Vitabu vya karatazi za kupigia kura vyenye mashaka

Kulikuwepo na baadhi ya vitabu vya karatasi za kupigia kura ambavyo vilishikizwa hovyo hovyo (poor binding) na hii inaashiria kuwa huenda vitavu hivyo vingine vilifumuliwa badala ya kutoka kuchapishwa.  Hivyo ni kusema wizi wa kura kushirikisha pia kampuni ambazo hutumiwa kuchapisha kura.

6.1.9    Kujiingiza kwa serikali na vyombo vya dola

Cha cha mapinduzi na serikali yake pamoja na vyombo vyake vya dola vilizna kuvvipakazia matope vyama vya upinzani hususan CUF, ili kuhalalisha utumiaji wa vitisho na mabavu.  Majeshi ya nchi hasa Polisi wa kawaida na FFU walikuwa na mkakati wa kuweka watu kokoroni hovyo hovyo.  Mkakati huu wa kuwaweka watu ndani bila kesi ulianza siku kadhaa kabla kupiga kura.  Kukataa kukubali Katiba ya kidemokrasi, kuunda Tume za Uchaguzi zilizo huru na zenye uwakilishi kutoka vyama vya siasa na kuwapa Watanzania wote vitambulisho rasmi vya uraia yote ni mambo yaliyoisaidia na yataendelea kuisaidia sana CCM.

Kadhalika watu binafsi hasa matajiri waliichangia CCM kwa hali na mali, kwa hiari na kwa kulazimishwa.  Matajiri wanapobainika kuwasaidia vyama vya upinzani wanaitwa na kutishwa.  Wakati wa uchaguzi kodi kuingizwa katika mkondo wa rushwa na wafanyabiashara wanaoisaidia CCM wao hupunguziwa ushuru au hata kuufanya uwanja wa siasa usiwe huru na sawa hasa siku za uchaguzi.

Sehemu ya 2: Pingamizi wakati wa uteuzi

Tume ya Uchaguzi ya Taifa ya CUF ilipokea taarifa ya pingamizi kwa wagombea wetu wa nafasi za Ubunge zipatazo 8 kutoka majimbo 8 kati ya majimbo 88 tuliyoshiriki.  Majimbo hayo ni:

1          Jimbo la Kilindi                         -           Tanga

2          Jimbo la Bunda                         -           Mara

3          Jimbo la Chalinze                                  -           Pwani

4          Jimbo la Baki                                        -           Dodoma

5          Jimbo la Kondoa/Kaskazini      -           Kondoa

6          Jimbo la Mbinga Magharibi       -           Ruvuma

7          Jimbo la Kyela                          -           Mbeya

8          Jimbo la Lindi Mjini                              -           Lindi

Katika nafasi za Udiwani Tume ilipokea pingamizi 20.  Moja kati ya sababu za pingamizi zilizowekewa wagombea wetu ni kuwasilisha fomu zilizoambatanishwa na picha za rangi badala ya zile picha za rangi kwa mujibu wa maelekezo ya awali ya NEC na mabadiliko kuhusu picha yaliyotolewa na NEC yalichelewa kuwafika wagombea jambo ambalo liliwasumbua sana wagombea wetu.  Kwa hivyo, mazingira hayo yalisababisha baadhi ya wagombea wetu kukosa haki ya kuteuliwa  kwa wakati au kukataliwa kabisa.  Ipo mifano kadhaa.  Lakini pingamizi zilizowekwa na wagombea wa vyama vya upinzani dhidi ya wagombea wa CCM hazikupewa uzito unaostahiki na mwishowe zilipuuzwa kabisa.  Kwa hali hiyo basi inaonesha kiasi gani Tume ya Taifa ya Uchauzi isivyokuwa huru na jinsi isivyotenda haki kwa vyama vyote vya siasa vilivyoshiriki uchaguzi, izipokuwa iliependelea CCM tu, wazi wazi.

Sehemu ya 3: Matokeo ya uchaguzi

Kwanza uwasilishaji wa matokeo haukuwa mzuri kama ilivyotarajiwa.  Ulikuwa ukifanywa kinyemela nyemela.  Pili mawakala walikatishwa tamaa kutokana na matokeo yaliyokuwa yakijitokeza kinyume na yaliomo katika rekodi zao.  Wengine hawakujali kuwasilisha matokeo kwenye kata zao, na baadhi yao hawakupewa fomu za kuonesha matokeo.  Kwa kasoro zote hizo vyama vya upinzani viliathirika sana na hivyo Chama cha CUF ndio kikaambulia majimbo mawili tu ya ushindi wa Ubunge yaani:  Jimbo la Kigamboni, Dar es salaam na Jimbo la Bukoba Mjini kwa Tanzania Bara.

Kupinga matokeo mahakamani  ni haki ya mwananchi yeyote aliyedhulumiwa au kupokonywa haki yake.  Kama sio kikwazo cha dhamana ya milioni tano kwa ubunge na laki tano kwa udiwani, ingekwa sahihi wote ambao hawakuridhika na matokeo kwenda mahakamani.  Lakini  hili halikuwezekana.  Dhamana imewekwa wazi kuliko uwezo wa Mtanzania wa kawaida ili kuwanyima haki wazalendo.  CCM hukata rufaa kwani hupata udhamini wa matajiri ambao wanaendelea kuwasaidia kuendeleza madhambi ya demokrasia.

6.2.1.   Vyombo vya Habari katika Uchaguzi

Kwa kweli kila mtu anajuwa nafasi ya vyombo vya habari katika uchaguzi na jinsi vilivyojishughulisha katika kututangaza vibaya na kutuchafulia hadhi katika jamii.  Kwa kiasi fulani magazeti ya binafsi yalijribu kutoa taarifa na habari zetu ambazo tulikuwa tukiwapa.  Hata hivyo mara nyengine waandishi walipata habari potofu kutoka kwa watu wasiokitakia mema chama chetu.  Kwa kusahau au kudharau maadili na wajibu wao wa kuwa kioo kwa jamii, vyombo vinginne kama vile : RTD, TVT,Radio Uhuru, Magazeti yote yanayomilikiwa na Serikali, vyomvo vilivyomilikiwa na wafanyabiashara maarufu ambao wamekuwa wapiga debe wakuu wa CCM, Magazeti binafsi yanayomilikiwa na CCM, vyote vilishirikiana kikamilifu kudhoofisha nafasi yetu ya ushindi katika uchaguzi, lakini pia ilichangia uichochea na kuichonga dola makali ili izidi kuikandamiza CUF na wanachama wake.

Mazingira haya mabaya ndio baadae yalioacha dukuduku nyoyoni mwa watanzania walionyimwa haki ya uchaguzi kwa upande mmoja, na kwa upande mwengne kuifanya dola kujitayarisha vibaya kwa lolote ambalo lingetokea hata kama lingekuwa kutoka kwa wapinzani.  Kwa kuwa haya pia yaliivisha mgogoro, basi ni dhahiri kwamba yalichangia mauaji ya tarehe 26 na 27 Januari, 2001, kwani hata baada ya uchaguzi, vyombo vya habari tulivyotaja vilichangia sana kushajiisha vitendo viovu vya Serikali za Chama Tawala na vyombo vya dola katika nchi.

Tunachozidi kusisitiza baada ya taarifa hizi za chaguzi za vyama vingi ni kwamba bado upo uhusiano wa kutosha kati ya chaguzi hizi ambazi hazikuendeshwa kwa “haki na huru” na migogoro iliyofuata baadae na hatimae mauaji ya kutisha ya tarehe 26 na 27 Januari, 2001.  Na kwa hivyo basi, sababu za kihistoria ambazo zimetegemewa sana na Serikali ni dhaifu mno kuhusishwa na mauaji hayo.  Hivyo ni kusema, kutotokea tena kwa mambo kama hayo kunahitaji uendeshaji chaguzi katika mazingira ya haki na huru.  Haya yatapatikana iwapo pamoja na mambo mengine Tume ya Uchaguzi ya Taifa itawakilishwa kwa maoni ya vyama vingi; na vile vile iwapo sheria za uchaguzi zitaboreshwa.  Pamoja na yote hayo, vyombo vya dola na vile vya habari viachane na misimamo yao ya kuipendelea CCM kwa kuvihujumu vyama vya upinzani, tabia ambayo hujenga mazingira ya kutoaminiana na chuki ambavyo mwishowe huzaa magomvi na kuchafua amani na utulivu katika nchi.

Baada ya kuonesha nini zilikuwa sababu za mauaji ya tarehe 26 na 27 Januari, 2001 sehemu inayofuata itaelezea namna mauaji yalivyotokea.

SURA YA SABA