CCM yaibua mwafaka, CUF yaweka masharti

21 09 2008

Date:: 9/20/2008

Na Peter Edson

 

WAKATI Chama Cha Mapinduzi (CCM) kikisema kuwa mazungumzo ya muafaka wa Zanzibar yanatarajiwa kuanza hivi karibuni baada ya Chama Cha Wananchi (CUF) kukubali kurudi kwenye meza ya mazungumzo, chama hicho kimesema hakina taarifa.

 

Msaidizi wa Katibu Mkuu wa CUF, Ismail Jussa, aliliambia gazeti hili jana kuwa taarifa ya CCM kwamba CUF imekubali kurudi katika meza ya mazungumzo sio kweli kwasababu hawajawasiliana na CCM kuhusu jambo hilo.

 

Jusa alisema hawana taarifa zozote kuhusiana na kikao kama viongozi wa CCM walivyodai na kusisitiza kwamba mazungumzo hayo hayapo.

 

Jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Kapteni John Chiligati, aliwaambia waandishi wa habari kuwa baada ya vuta nikuvute iliyodumu kwa miezi saba sasa kuhusu mazungumzo hayo, CUF sasa imekubali kurudi mezani.

 

“Wenzetu wa CUF wamekubali kurudi kwenye meza ya mazungumzo, tunachokisubiri ni kupangwa kwa tarehe ya kuanza upya mazungumzo hayo itakayotangazwa na makatibu wakuu wa vyama hivyo viwili, Yusufu Makamba (CCM) na Maalim Seif Sharif Hamad,” alisema Kapteni Chiligati.

 

Alisema awali CCM ilipokea mapendekezo yote yaliyotolewa na chama cha CUF na kuyakubali kwa asilimia 95, lakini kukawa na baadhi ya vipengele ambavyo CCM haikuridhika navyo na ndio maana iligoma kusaini makubaliano ya muafaka.

 

Chiligati alitaja vipengele vilivyochelewesha kumalizika kwa mazungumzo hayo kuwa ni kuondolewa kwa kipengele cha kuwashirikisha wananchi kupiga kura kuhusu serikali ya mseto, kuwepo kwa Baraza la Usuluhishi, kutathimini mwenendo wa Serikali kila baada ya miaka mitano na mchakato wa kuwateuwa mawaziri kulingana na wingi wa wabunge.

 

Alisema kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) kilichofanyika mjini Butiama mkoani Mara kiliyaweka bayana masuala hayo na kuyarudisha kwa Katibu Mkuu wa CUF ili yajadiliwe, kwa kuwa yasingeweza kuimarish utawala bora.

 

“NEC ilimuagiza Katibu Mkuu kuyafikisha mambo hayo upande wa pili na kutekeleza, hivyo tunashukuru wenzetu wamekubali turudi kwenye meza ya majadiliano.” alisema Kapteni Chiligati.

 

Alisema awamu hii ya mazungumzo, itaenda sambamba na marekebisho ya Katiba ya Zanzibar endapo pande mbili zinazoshiriki mazungumzo hayo zitakubaliana na kusaini mapendekezo ya muafaka huo yatakayoanza kutekelezwa mwaka 2010.

 

“Marekebisho ya Katiba pia yatagusa mabadiliko katika sheria ya tume ya uchaguzi ili kwa pamoja viweze kwenda sambamba na mabadiliko ya uongozi wa mseto,” alisema.

 

Alisema jambo lingine ambalo litafanyika ni kuhakikisha kuwa wananchi wanaelimishwa kuhusu taratibu na kanuzi za utawala wa Serikali ya Mseto ili itakapoanza kusitokee tena usumbufu.

 

Chiligati alisema anaamini mchakato huo utafanyika kwa kasi ili kuondoa kero ya mwafaka inayogubika siasa za Zanzibar sasa.

 

Gazeti hili lilipowasiliana na Msaidizi wa katibu Mkuu wa CUF mara baada ya Chiligati kusema hayo, alisema chama chake hakina taarifa kuhusu suala la hilo. “Taarifa hizo sio za kweli, CUF hatuna taarifa wala haijawasiliana na CCM kuhusu suala la mwafaka tangu kimalize mkutano wake wa NEC,” alisema.

 

Jusa alisema CUF hakina taarifa ya kuanza kwa mazungumzo hayo yanayodaiwa kuwashirikisha makatibu wakuu wa CUF na CCM na hata kama ingekuwa na taarifa hiyo bado isingekubali mazungumzo hayo yarudishwe kwenye Kamati ya makatibu wakuu.

 

“Nani alisema hayo? Sisi hatujapata taarifa ya mdomo wala maandishi. Lakini hata kama tungepata, msimamo wa CUF sasa ni kwamba, mazungumzo hayo yamemalizika kwenye ngazi ya kamati na sasa yanatakiwa kufanywa na viongozi wakuu wa vyama hivyo yaani, Maalim Seif na Karume kwa upande wa Zanzibar au Jakaya Kikwete na Profesa Lipumba,” alisema.

 

Alisema anaamini CCM imetoa kauli kama mwendelezo wa propagansa zake kuhusu mwafaka na kamwe CUF haitakubali kutumika kwa faida ya CCM.

 

http://mwananchi.co.tz/newsrids.asp?id=7066





Mafuta Zanzibar: Hata kidogo katika kinibu tutagawana na mengine kujipaka

21 09 2008

Date :: 9/19/2008

Na Salma Said, Zanzibar

NAJMA KHALFAN JUMA

NAJMA KHALFAN JUMA

Wawakilishi wa Zanzibar wamesema “hata kama ujazo wa mafuta yanayoweza kupatikana Zanzibar ni sawa na glasi ndogo ya kupimia pombe (kinibu), mafuta hayo ni mali ya Wazanzibari watagawana ili watakaoweza wajipake mwilini”.

Kauli hiyo ilitolewa jana baada ya mshauri, David Reading, kueleza kuwa mafuta yanayowezekana kupatikana kisiwani humo ni kidogo na kupatikana kwake ni kwa gharama kubwa.

Mtaalamu huyo kutoka Uingereza aliitwa kwa ajili ya kuishauri Serikali ya Mapinduzi (SMZ) na serikali ya Muungano namna bora ya kugawana rasilimali itokanayo na gesi na mafuta.

Kauli hiyo ya Reading pia imesababisha wawakilishi kuingiwa na chuki dhidi ya Wazanzibari walio kwenye serikali ya Muungano, wakiwaita kuwa ni vigeugeu mithili ya vinyonga na wasiojali maslahi ya Wazanzibari.

Akitoa maoni yake kuhusu suala la mafuta na gesi asilia kwa mshauri huyo mwelekezi, mwakilishi kutoka Chama cha Wananchi (CUF), Najma Khalfan Juma alisema kuwa hata kama mafuta ya Zanzibar yatakuwa madogo kiasi cha ujazo wa glasi ndogo ya kupimia pombe ya haramu ya gongo (kinibu), Wazanzibari watagawana hata ikiwa kwa ajili ya kujipaka mwilini.

“Hata kama watajipaka mwilini au wengine watatumia kama dawa ya kuchulia misuli, itakuwa bora zaidi kuliko suala la mafuta kuwa la Muungano,” alisema.

Naye mwakilishi wa kuteuliwa na rais, Ali Mzee Ali, ambaye pia ni mwenyekiti wa Baraza la Wawakilishi, alisukumia shutuma zake kwa mawaziri walio kwenye serikali ya Muungano ambao ni Wazanzibari, akiwaita kuwa ni wanafiki na wanaobadilika kama kinyonga.

“Mheshimiwa mwenyekiti kuna wenzetu ambao wamo katika serikali ya Muungano. Wakija hapa (Zanzibar) wanajifanya ni watetezi sana wa Zanzibar, lakini kumbe ni wanafiki,” alilalamika mwakilishi huyo.

“Tabia ya viongozi hao haiwanufaishi Wazanzibari. Viongozi wa Zanzibar wasiwatilie maanani watu wa aina hiyo kwa kuwa wanatanguliza maslahi binafsi.

Baadaye mwakilishi huyo mteule aligeukia vyombo vya habari vya Zanzibar na kusema: “Kitu cha kushangaza ni gazeti la Asumini ambalo limesajiliwa hapa Zanzibar. Gazeti hili liliwahi kuandika makala ndefu kuelezea umuhimu wa nishati ya mafuta kuwa ya Muungano.

Jambo hili si sahihi kwani Zanzibar hainufaiki na lolote na mapato ya gesi inayozalishwa Tanzania Bara,” alisema.

“Ninalo hapa, waheshimiwa wajumbe, gazeti la Zanzibar Leo ambalo limechapisha makala kama ile iliyotolewa katika gazeti la Asumini. Sijui makala hii imepenya vipi mpaka ikatolewa humu; hilo anajua Mheshimiwa (Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Ali Juma) Shamhuna.”

Gazeti la Asumini na Radio ya Zenj FM zinamilikiwa na Kampuni ya Zanzibar Media Corporation, ambayo Mkurugenzi wake ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Muungano, Muhammad Seif Khatib.

Mwakilishi huyo alisema mara nyingi wanaojitokeza kutetea maslahi ya Zanzibar wanaonekana wanafanya kampeni ya urais kwa mwaka 2010, huku wengine wakishambuliwa kwa maneno kuwa hawautaki Muungano ama kuwa na ajenda ya siri jambo ambalo anaamini si sahihi.

Ali Mzee aliwataka wananchi na hasa wajumbe wa baraza la wawakilishi kuungana kuwa kitu kimoja katika kutetea maslahi ya Zanzibar na kuachana na watu aliowaita kuwa ‘Wazanzibari Maslahi’ kwenye serikali ya Muungano.

Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Kiongozi, Hamza Hassan Juma aliwataka viongozi wa Zanzibar kutoogopa kufukuzwa serikalini kwa kuitetea Zanzibar kwani mara nyingi mtu anapojitokeza kutetea maslahi ya visiwa hivyo, huambiwa kuwa amechafua hali ya hewa kama ilivyokuwa kwa rais wa zamani wa Zanzibar na Makamu wa Kwanza wa Rais, Aboud Jumbe Mwinyi.

“Waheshimiwa tusiogope kunyang’anywa magari,” alisema. “Wakitunyang’anya sawa, tutatembea hata kwa miguu lakini lazima tuitetea nchi yetu kwa sababu sisi tumeapa kwa katiba hii (katiba ya Zanzibar) na sio ya Jamhuri ya Muungano.”

Akichangia hoja hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais- Fedha na Uchumi, Dk. Mwinyihaji Makame alishabihiana na wenzake, akieleza kuwa katika suala la mafuta hakuna dhamira njema kwa Wazanzibari.

Mwakilishi wa Viti Maalumu (CUF), Zakia Omar Juma alisema umefika wakati sasa kwa Wazanzibari kujikomboa kiuchumi kwa kuungana kutetea mafuta yao kwani mara nyingi Zanzibar inapotaka kujikwamua kiuchumi huwekewa vikwazo na serikali ya Muungano.

Mwakilishi wa Jimbo la Ziwani (CUF), Rashid Seif alisema kwamba inaonekana Zanzibar kuna mafuta ya kutosha na ndio maana watu wa Tanzania Bara (Tanganyika) wanang’ang’ania suala la mafuta kuwa la Muungano licha ya kuwa Wazanzibari wenyewe hawataki.

http://mwananchi.co.tz/newsrids.asp?id=7063





Polisi acheni uchochezi kisiasa

21 09 2008

MEI 21, 2008

 

Na Jabir Idrissa

 

ZIPO fitna tatu kuu kwa sasa zinazohusiana na hali ya mambo ilivyo Zanzibar kisiasa kiasi cha kukumbusha mabaya yaliyotokea mara tu baada ya uvurugaji matokeo ya uchaguzi mkuu wa 1995 na 2000.

 

Fitna ya kwanza ni kuibuka upya kwa hali mbaya ya kisiasa na ya pili, ni hatua ya Jeshi la Polisi kusakama wananchi wa Pemba waliopeleka barua ofisi za Umoja wa Mataifa kushinikiza haki ya kushirikishwa kwenye uongozi wa nchi yao.

Fitna zote hizi zina wenyewe. Ya kwanza imechochewa na Chama cha Mapinduzi (CCM) baada ya kuzua hoja katika hatua ya mwisho ya kukamilisha mazungumzo iliyokuwa ikifanya na Chama cha Wananchi (CUF) kuhusu utafutaji ufumbuzi wa kudumu wa kile Rais Jakaya Kikwete alichokiita, “mpasuko wa Zanzibar.”

 

Chama hiki, kitake kisitake, kimevuruga kwa kuleta hoja isiyopata kujadiliwa katika vikao 21 walivyokaa na CUF ndani ya miezi 14 ya majadiliano yaliyoanza kutokana na agizo la Rais Kikwete la 30 Desemba, 2005.

 

Imethibitika hoja ya Kura ya Maoni haikuwahi kuwasilishwa hata mara moja vikaoni. Inapotokea chama cha rais aliyeagiza mazungumzo ya kutafuta ufumbuzi wa tatizo la kisiasa, ndio kinavuruga mambo, hiyo huwa ni fitna.

 

Hilo moja. Lipo la pili: kwamba ni CCM kilichokacha mchakato wa mazungumzo na CUF baada ya kutoa marekebisho ya makubaliano badala ya kuidhinisha na kurudisha rasimu waliyokubaliana.

 

CCM walipokutana Butiama, kilichotarajiwa kufanyika ni kile kilichofanywa na wenzao CUF 17 Machi, 2008 mjini Zanzibar: kuidhinisha makubaliano na CCM yaliyoandaliwa katika rasimu ya muafaka.

 

Maamuzi yao yakawa ni kurekebisha makubaliano yaliyofanyiwa kazi kwa vikao 21. Hii ni fitna ndani ya ile fitna ya kwanza ya kuzua hoja mpya.

 

Baada ya hapo, kumeibuka upya siasa chafu na kauli za kushutumiana zinazojulikana wazi kuwa chanzo cha kuchafuka hali ya hewa Zanzibar.

 

Kwa hivyo, CCM hawajarudisha rasimu ya muafaka ambayo ingeandaliwa vizuri ili iwe Muafaka wa Tatu na muongozo wa ufumbuzi wa mgogoro wa kisiasa unaoikabili Zanzibar kwa zaidi ya miaka 10 sasa.

 

Ndio kusema dhamira ya Rais Kikwete haijatimia. Kwa sababu haijatimia, na kwa kuwa utekelezaji wa muafaka ilikuwa ndio matumaini ya wananchi ya kuondokana na mgogoro, unajichimbia mtafaruku.

 

Mtafaruku umeibua hisia za chuki, hasahasa kwa wananchi wa Pemba. Hawa wamekuwa wakiamini ndio wanaoumia zaidi na siasa chafu zinazojichimbia Zanzibar, wameamua kutafuta namna ya kujitoa katika tanuri la dhiki.

 

Njia za kujitoa humo ni nyingi. Nyingine za kisiasa ambazo zinaendelezwa na CUF, nyingine za kijamii kama zilizotajwa na mbunge mmoja za wananchi wa Pemba kugoma kupeleka mazao ya chakula Unguja.

 

 

Hatua ya wazee 12 kuandika barua na kuipeleka ofisi za Umoja wa Mataifa, Dar es Salaam, ni njia nyingine. Hii si ya kisiasa japo inaweza kuonekana hivyo.

 

Wazee hawa ni raia katika nchi huru. Wana haki kudai wanachokiamini ni haki. Kudai haki hufanywa kwa njia nyingi; wao wametumia hii inayoshirikisha taasisi ya kimataifa. Wanachokifanya ni kutoa maoni yao baada ya kuona mchafukoge unaendelea kutokana na muafaka kukwama.

 

Waliamini ungesainiwa na ukaanza kutekelezwa, siasa chafu zingeondoka na kuleta uongozi mzuri ambao matokeo yake ni kuondoka zile dhiki na chuki zinazowaandama.

CCM imefuta matumaini yao. Wafanyeje kama raia wenye haki ya kikatiba ya kuishi kwa amani, utulivu na utengamano wa kweli si wa hisia?

 

Lazima washinikize mabadiliko. Kupeleka barua inayofahamisha Umoja wa Mataifa kuwa hawawezi kuendelea hivyo na wanaomba msaada kwa taasisi yenye dhamana ya kulinda haki za wamataifa wote duniani, ni shinikizo halali.

 

Mwaka 1967, Rais Julius Nyerere aliunga mkono kampeni ya wananchi wa Biafra, nchini Nigeria, kutaka kujitenga. Alipeleka jeshi kule kwenda kusaidia wapiganaji wa kundi la MASSOB (Movement for Actualisation of the Sovereign State for Biafra) likiongozwa na Ogumu.

 

Ogumu na Yakoub Gowon aliyekuwa Rais wa Nigeria wakati huo, leo ni wajumbe wa Baraza la Ushauri la Serikali ya Rais Al Yaradua wa Nigeria.

 

Wabunge wa Mtwara waliwahi kuitaka Serikali iwaachie wajiunge na Msumbiji ambako ni karibu nao kwa kuwa serikali yao haitaki kuwajengea miundombinu ya kurahisisha shughuli zao za maendeleo. Hawakukamatwa.

 

(Marehemu) Sebastian Kinyondo alipokuwa Mbunge miaka ya 1990, aliwahi kuitaka serikali iwaachie wananchi wa Mkoa wa Kagera wajiunge na Uganda kwa kuona serikali yao haitaki kuwapatia huduma za jamii kama vile umeme na usafiri wa uhakika. Hakukamatwa.

 

Wabunge 55 waliounda kundi maarufu likiitwa G55 waliichagiza serikali mwaka 1994 wakitaka irudishwe Tanganyika ili wawe na haki kama walivyo Zanzibar. Hawakukamatwa.

 

Mchungaji Christopher Mtikila anaamini mpaka leo yeye ni Mtanganyika na angependa itambuliwe hasa Tanganyika ipo. Pamoja na Jamahuri kumfungulia kesi mbalimbali, hakuna kesi kwa hilo. Hajawahi kukamatwa.

 

Leo Polisi wa Tanzania wanakamata wazee wa Pemba wanaodai haki ya kushirikishwa katika uongozi wa nchi yao. Wangekuwa wabunge, wangedai haki hiyo bungeni, wangekuwa wanasiasa wangedai haki hiyo kwenye jukwaa la kisiasa. Hawa ni raia tu, wameandika barua na kuipeleka Umoja wa Mataifa, tena mchana kweupe.

 

Kitendo cha Polisi kuwakamata wazee hawa na kuwaandalia kesi si kitisho peke yake, ni fitna ya nguvu.

 

Nini kama si fitna kugonga milango ya nyumba zao usiku wa manane wakati hawana silaha? Nini maana yake kuwatoa mkuku kutoka vitanda walivyolala na wake zao wakati si magaidi?

 

Nini maana ya kuwachukua hadi Unguja na Dar es Salaam na kuwaficha kwa siku kadhaa huku wakiwahoji kama vile ni watuhumiwa ujambazi? Haya wangefanyiwa majambazi ningefahamu, wangefanyiwa waleta madawa ya kulevya na majangili ningefahamu. Wanyonge wanaodhalilika nchini mwao wanapodai haki ya kikatiba kwa amani, wametenda kosa gani?

 

Polisi imeleta fitna isiyo sababu. Inakamata raia anayetoa maoni yake badala ya kumjengea mazingira mazuri ili asahau anachokidai. Halafu Inspekta Jenerali Said Mwema anakataa kwamba Polisi ni wanasiasa. Anakataaje au anataka ushahidi wa Mnyamwezi?

 

Ni kauli tu lakini haina nguvu. Polisi waliingilia siasa siku zote huko nyuma kama alivyodhihirisha Omar Iddi Mahita kabla hajastaafu. Alijiita ngunguri na hata boti ya Polisi ikapachikwa jina hilo.

 

Aliisakama CUF na kukamata viongozi wake hadi kutungiwa kesi ya uhaini. Alitia chokochoko chama hicho kisichaguliwe maana kiliingiza mabomu kupitia mkoani Mtwara pamoja na visu kabla ya uchaguzi wa 2005.

 

Viongozi wa Polisi muache siasa. Nilidhani tatizo lilikuwa Mahita, kumbe kiti cha IGP. Niliandika sana makala, kupitia safu ya Waraka kutoka Unguja, kabla ya uchaguzi wa 2005 nikiwalaumu Polisi kwa uovu huu. Nilisihi wabadilike ili waheshimike kuwa walinzi wa kweli wa raia na mali zao. Hawakusikia wakasaidia kuvuruga uchaguzi, wakaua.

 

Nasikitika narudishwa kulekule kutokana utendaji wao. Hivi Watanzania wanaotoka Pemba wamekosa nini? Likizuka la ugaidi wao, likija la uhaini wao, likija la mpasuko, wao. Niliamini tu watakamatwa baada ya kusikia Waziri wa Nchi, ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Muhammed Seif Khatibu akisema kudai kujitenga ni “uhaini.”

 

Vitisho dhidi ya raia Zanzibar huanza hivyo. Hutokea tukio na kada wa CCM akatoa kauli ambayo vyombo vya ulinzi na usalama huichukua ni amri. Inapokuwa wahusika ni wafuasi wa upinzani, inajengwa kesi.

 

Hizi zote ni fitna. Lengo lake ni kukengeuka tatizo la msingi linaloikabili nchi, Muafaka, ili kulaghai wananchi kwa kupakaza ubaya wanaopigania haki zao.

 

Polisi hawajawahi kukamata wabunifu na wasambazaji wa vikaratasi vinavyoeneza chuki dhidi ya wanaokandamizwa.

 

Hawajawahi hata mara moja japokuwa wanawafahamu wanaoendesha operesheni hii ya kishetani. Siku zote makamanda husema “tunachunguza.” Sawa waendelee kuchunguza kama walivyofanya kwa ile milipuko ya kishetani baada ya uchaguzi wa 2000.

 

Wameshindwa hadi leo kumshitaki askari wa KMKM aliyemuua mwanafunzi wa shule ya msingi Ng’ombeni mjini Mkoani wakati wa kuandikisha wapiga kura.

 

Hawa ndio walewale waliokuwa wakiandaa mabomu ya petroli na kuwasha kwenye maeneo mbalimbali mjini Zanzibar na kwenye makanisa ili kujenga chuki na kupata sababu ya kukamatwa wafuasi wa upinzani. Polisi mtajifunza lini?

 

http://www.halihalisi.co.tz/08/05/21/4.php





TAHARIRI: Rais Kikwete chukua nafasi

21 09 2008

MEI 21, 2008

 

KATIKA safu hii wiki iliyopita, tulitaka vyama vya CCM na CUF virudi mezani ili kukamilisha mchakato wa utekelezaji wa muafaka uliofikiwa baada ya miezi 14 ya majadiliano.

 

Lakini wakati tukihimiza hilo, tunasikitika kuona wanatokea watu wanatoa kauli zinazodisha malumbano na kuchochea chuki na uhasama dhidi ya viongozi wa CUF.

 

Hawa si wengine, bali ni viongozi waandamizi wa Umoja wa Vijana wa CCM (UV-CCM) na  kitengo cha propaganda cha chama hicho.

 

Kila mmoja anajua kwamba Zanzibar kuna tatizo kubwa la kisiasa. Kama tunataka kutazama mambo kwa maslahi ya taifa, basi hakuna anayebisha.

 

Na hilo ndilo lililomsukuma Rais Jakaya Kikwete kumaliza tatizo alipoahidi kutafuta njia ya “kuupatia ufumbuzi wa kudumu mpasuko wa Zanzibar.”

 

Ahadi hiyo ilihalalisha kuanza mchakato wa majadiliano. Ni wazi CCM na CUF vimeshaafikiana, isipokuwa, tofauti zimekuja katika namna ya kutekeleza yale yaliyokubaliwa.

 

Katika hali kama hiyo, hatudhani kama ni busara kutokea Watanzania, tena viongozi wa juu wa CCM, wakathubutu kutoa kauli za kejeli, chuki na uhasama, dhidi ya CUF na rais kwa ujumla.

 

Kusema kwamba CCM kukubali kukaa mezani na CUF ni fadhila tu kwa chama cha upinzani na kwamba Rais Kikwete hana uwezo wa kumaliza mgogoro huo bila ya kushirikisha vikao vya chama chake, ni dharau kwake na kubeza kile anachokisimamia.

Rais anayo mamlaka tena makubwa, hasa ukizingatia kwamba alipotoa ahadi ile aliitoa kama kiongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Baadaye amekuja kuvikwa na uenyekiti wa taifa wa chama chake. Hayo ni mamlaka.

 

Anajua vizuri sababu ya kuahidi alichoahidi. Anajitambuwa kwamba kuwa kwake kiongozi wa ngazi ya juu nchini kwa muda mrefu kumempatia uzoefu wa kutosha wa kuujua mgogoro wa Zanzibar na athari zake.

 

Tukubaliane kuwa hali ya kuaminiana, japo kwa kiwango kidogo, iliyokuwepo kwa Kamati mbili za mazungumzo, imetoweka na msimamo wa CUF kutotaka tena kukaa na CCM, ni ushahidi tosha kwamba bado Zanzibar inasumbuliwa na mgogoro na lazima umalizwe.

 

Sawa, hawawezi kukaa tena na CCM, lakini na umma hauwezi kuendelea kuona nchi inarudi katika machafuko kama ilivyokuwa huko nyuma. Tunataka wote wanaohusika kuheshimu matakwa ya wananchi na muafaka uheshimiwe na kusainiwa haraka iwezekanavyo.

 

Katika hili, hatuoni njia ya kupita, isipokuwa Rais Kikwete kuchukuwa nafasi yake kama kiongozi mkuu wa taifa, kuelekeza na kuagiza cha kufanywa kwa maslahi ya taifa. Lazima tuondoke tulipo na twendeni mbele!

 

http://www.halihalisi.co.tz/08/05/21/2.php





Siasa-mzaha zinazidisha tu mgogoro Zanzibar

21 09 2008

MEI 14, 2008

 

INASIKITISHA sana kuona jitihada zilizochukuliwa na vyama viwili hasimu katika siasa za Zanzibar, zimeishia.

 

Inasikitisha sana kuona tulipo ni kama vile hakuna kiongozi wa kutoa muongozo ili Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Wananchi (CUF), viondoke vilipokwama na kuendeleza mchakato wa utekelezaji wa makubaliano waliyoyafikia.

 

Inasikitisha kuona vyama hivi vimeacha kusimama katika ukweli au vinaudhihaki na kuendeleza malumbano ambayo kwa namna yeyote hayajengi, zaidi ya kuonyesha jinsi viongozi wa vyama hivi wasivyowajibikaji kwa maslahi ya taifa.

 

Lakini inasikitisha zaidi kuona matamshi ya viongozi wa vyama hivi tangu pale muwafaka ulipogota, hayaelekei kwenye momentamu waliyofanikiwa kuijenga kabla ya kuanza kujadiliana yale waliyoafikiana kama ajenda.

 

Nimeanza hivi makusudi maana hali ya mchafukoge inazidi kushamiri kinyume na matarajio ya wananchi wa Zanzibar, Jamhuri ya Muungano, na ulimwengu kwa ujumla.

 

Niliposikia viongozi wa juu wa CCM wameitisha mkutano na waandishi wa habari Jumapili 11 Mei, niliamini kwamba wanania ya kutegua kitendawili walichokitega kutokana na maamuzi yao walioyafikia katika vikao vyao vilivyofanyika Butiama, mkoani Mara.

 

Lahaula! Si kwamba sivyo tu, bali ukweli ni kwamba wametengenezea wigo wa kuhifadhi mtego wao. Wamezidisha tu lawama dhidi ya wapinzani wao na kuendeleza upotoshaji mambo.

 

Kama wanavyofanya CUF kuzunguka nchi katika wanachosema “kuweka shinikizo” ili CCM warudi kusaini Muwafaka, wameuzidisha utata.

 

Lakini wakati muafaka umekwama, inasikitisha kuona yale matumaini ya kutatuliwa kwa mgogoro wa kisiasa unaolazimishwa kuwepo kwa sababu za kisiasa zisizozingatia uendelevu wa sehemu muhimu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, yamebezwa.

 

Hilo ni moja. Linalonikereketa kwa sasa ni kuona panaendelea kukosekana mtu wa kutoa muongozo wa kuondoa mkwamo, badala yake tunasikia kelele na kuendelea kutazama wakati kuna giza nene. Ndio, tupo kizani.

 

Hapana wa kumtia shemere hapa isipokuwa Rais Jakaya Kikwete, mwenye dhamana mbili kwa suala hili. Ya kwanza ni ya kuwa kiongozi wa jamhuri, lakini ya pili, ni ya kuwa ndiye aliyeahidi Watanzania na Ulimwengu kuwa atasimamia kupatikana “ufumbuzi wa kudumu” wa alichoita “mpasuko wa Zanzibar.”

 

Lakini simshangai na sababu ninazo: yeye ni kada mzuri wa CCM, chama kikongwe ambacho kinaamini kiko katika harakati za ukombozi wa kinaowaongoza badala ya kuwajenga kihali.

 

Ninachoweza kusema zaidi kumhusu Rais ni kwamba lazima achukue nafasi yake kama kiongozi mkuu wa kila kitu; Taifa na chama tawala, kuondoa hofu za watu zinazozidi kujengeka kutokana na kuona mgogoro wa Zanzibar haujapatiwa ufumbuzi alioahidi.

 

Katika hali iliopo, rais hakupaswa na wala hapaswi kwa namna yoyote ile, kusimama kama kiongozi wa CCM, chama chenye maslahi makubwa na matamanio ya kuendelea kuongoza Tanzania ndani ya mfumo wa vyama vingi.

 

Anapaswa kusimama kama Baba wa Taifa, si baba wa CCM. Haitakiwi afikirie nini chama atokacho kitakosa au nini cha wapinzani wake kitapata iwapo makubaliano yaliyofikiwa yataanza kutekelezwa.

 

Kwanza muhimu Rais atambuwe anapaswa kutenda kwa morali uleule aliokuwa nao wakati akiahidi, kupitia hotuba ya ufunguzi wa Bunge aliyoitoa 30 Desemba 2005, kuwa atahakikisha “mpasuko wa Zanzibar” unapatiwa ufumbuzi wa kudumu.

 

Pili, atambuwe ahadi hiyo ingalipo na inasubiri kutimizwa. Utamaduni unaoaminika kwa watu wanaofikiri vizuri, ni kuwa mtu anayetimiza ahadi huitwa muungwana, kinyume chake huchukuliwa mnafiki.

 

Ieleweke Watanzania wanaojua Rais wao ameahidi kushughulikia mgogoro unaoendelea kuitafuna Zanzibar hadi kuirudisha miaka 100 nyuma kimaendeleo, wanasubiri atangaze ufumbuzi si mkwamo.

 

Hivi Rais anajisikiaje katika wakati huu ambapo mkwamo wa dhahiri wa utekelezaji makubaliano yaliyofikiwa na vyama vilivyoshiriki majadiliano, unazidi kuimarika?

 

Akiamua kuendeleza “siasa” badala ya “kutoa muongozo” usozingatia mawazo mgando, ajue kuwa hajasaidia mkwamo kuondoka.

 

Kila ninapofikiri naona CCM na CUF vimechoka kufikiri. Vimeamua kurudi vilikokuwa kabla ya kuanza kukaa mezani na kuzungumza.

 

Tatizo liliopo ni kuwa CUF wanajiona walikuwa na haki ya kueleza wanachama wao waliyoafikiana na wapinzani wao, CCM, iwe walishakubaliana nao au laa kuwa yaliyojadiliwa yafikishwe kwa wanachama.

 

Vivyo hivyo kwa CCM. Nao wanajiona walikuwa na haki ya kujadili makubaliano waliyofikia na wapinzani wao, CUF, na kuyatolea maamuzi, yakiwepo mapya.

 

Wala sioni kama ni muhimu kulaumu hatua ya makubaliano yaliyofikiwa kutangazwa kwa umma, kama ambavyo sioni ni tatizo kujadili makubaliano na kuyatolea maamuzi, muradi umma upewe ushahidi wa hoja za vyama hivi.

 

Kwamba uko wapi ukweli kuwa ajenda ya tano ya mazungumzo; ihusuyo “Utaratibu wa Utekelezaji na Programu ya Utekelezaji wa Makubaliano” haijajadiliwa.

 

Na uko wapi ukweli kwamba ajenda hiyo imejadiliwa na rasimu ya Muafaka imeandaliwa na kama CUF walikuwa na haki ya kuyatangaza haya kwa wanachama wao.

Tukieleweshana haya, tuchunguze mantiki ya hoja mpya ya CCM kutaka suala la mabadiliko ya mfumo wa utawala lazima lifikishwe kwa watu ili waliamue kupitia kura ya maoni.

 

Hakuna historia ya kura ya maoni kutumika kwa makubaliano ya amani yaliyofikiwa baada ya kuwepo mgogoro wa kisiasa. Hatujaona hili Burundi, Sudan, Angola, Afrika Kusini na kwa jirani, Kenya.

 

Masuala ya utawala huamuliwa na Bunge la Taifa husika wakati kura ya maoni hutumika pale panapohusu mabadiliko ya Katiba ya nchi hasa iwapo kuna upinzani miongoni mwa wana wa taifa husika.

 

Iwapo CCM imekubali “kimsingi” makubaliano iliyofikia na CUF, kura ya maoni inasaidia vipi kuendeleza utaratibu wa kuyatekeleza? Kenya palikuwa na kambi inayotaka katiba mpya na nyingine inayoikataa kwa kuona haikidhi matarajio ya Wakenya. Hapa Kura ya Maoni ilikuwa muhimu.

 

CCM imeridhia makubaliano yaliyofikiwa kutokana na mazungumzo yaliyoanzishwa na kiongozi wao mkuu ambaye ndiye Rais wa Watanzania. Sasa hoja ya Kura ya Maoni ambayo haikupata kujadiliwa pamoja na wenzao imetoka wapi?

 

Yanayofanyika ni mazonge matupu yasiyosaidia isipokuwa kuharibu kazi nzuri iliyokwishafanywa. Na Rais na CCM yake inafaa wakumbuke kuwa vyama hivi vina wafuasi wengi kwa hivyo kazi iliyokuwa inafanywa na wajumbe wake, Kamati ya Makatibu Wakuu, ilikuwa inaaminika kwa wafuasi wao.

 

Haiwezekani tuone hatua zinazobeza kazi hiyo iliyogharimu mamilioni ya shilingi kama posho za wajumbe na malipo ya gharama za chakula, malazi na makazi ya wajumbe waliokuwa wakijadiliana.

 

Je ni busara kudharau fedha hizi za Watanzania masikini? Hata kidogo. Hebu kila upande urudi kwenye “utu uzima” na kuacha “siasa-mzaha.” Bila ya masharti, kila chama kirudi mezani na kuanza walipofikia.

 

Kama ajenda ya tano haikujadiliwa, kama wanavyodai CCM, ijadiliwe lakini nao lazima waache kushikilia hoja mpya ya Kura ya Maoni. Hatuna njia ya mkato ila kwenda mbele.

 

http://www.halihalisi.co.tz/08/05/14/12.php