Haya ni mambo ya kisheria. Suala ni: zinasimama vipi kisheria Katiba zote mbili? Hapo ndipo
penye tatizo kubwa lililojitokeza kutokana na kauli ya Waziri Mkuu Pinda. Kwa sababu, inaonekana – na wala si suala la Pinda kwa hakika – inaonekana kumekuwa na msimamo wa muda mrefu sana kwa upande wa wanasiasa na mara nyengine hata wasomi kutoka upande wa Tanganyika wanaojaribu kuleta sura kwamba vile Katiba ya Jamhuri ya Muungano iko juu ya Katiba ya Zanzibar. Na hata kauli yake, Mheshimiwa Pinda, alisema hivyo hivyo, kwamba Katiba ya Jamhuri ya Muungano ndio Katiba Mama. Sasa hapo ndipo penye matatizo, kwa sababu katiba zote hizi mbili: Katiba ya Jamhuri ya Muungano na Katiba ya Zanzibar ni katiba sawasawa. Hakuna iliyoko juu ya mwenzake.
Mahojiano kati ya Mjumbe wa Baraza Kuu la Uongozi na Msaidizi Maalum wa Katibu Mkuu wa CUF kuhusu Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa, Mhe. Ismail Jussa, na kituo cha Redio cha Zenj FM cha mjini Zanzibar kuhusiana na kauli ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kwamba Zanzibar si nchi.



Maoni